ACT sasa kwachafuka, waanza kufukuzana

Mwenyekiti wa ACT,Kadawi Limbu
Dar es Salaam. Chama cha ACT-Tanzania kimewasimamisha viongozi wa chama hicho ambao ni Mwenyekiti wa muda Kadawi Limbu na Naibu Katibu Mkuu (Bara), Leopold Mahona na kikimvua madaraka Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana, Grayson Nyakarungu.
Hatua hiyo imejitokeza baada ya maazimio ya Halmashauri Kuu iliyokutana kujadili agenda za nidhamu ya mwenyekiti, kupokea na kupitisha mwongozo na kanuni za uchaguzi pamoja ushiriki katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Katibu mkuu wa chama hicho, Samson Mwigamba alisema jana kuwa maazimio ya mkutano huo yaliwachagua Shaaban Mambo kuwa mwenyekiti wa muda, Mohamed Masaga, Naibu katibu mkuu na Hassan Abdalah Omary kuwa mwenyekiti mpya wa vijana.
“Mkutano wa jana (juzi) ulikuwa na wajumbe 65, lakini kura 57 zilipendekeza Limbu na Mahona wasimamishwe katika nafasi zao kwa muda,” alisema Mwigamba na kuongeza kuwa: “Kwa mujibu wa katiba ya chama, Kifungu cha 27(f) kinasema halmashauri ina mamlaka ya kuwasimamisha kwa kipindi cha miezi sita, baada ya hapo watakuwa na haki ya kugombea tena nafasi zao pindi uchaguzi utakapoitishwa.”
Alipoulizwa kuhusu uamuzi huo kama wameshawapatia na kuwajulisha wahusika, Mwigamba alisema tayari taratibu zote zilishafanyika.
“Kwanza tuliwapa nakala ya mashtaka pia tukawaita kwenye mkutano ili kuwapatia nafasi ya kujitetea. Limbu alikataa kujieleza,” alisema Mwigamba.
Hata hivyo, chama hicho kwa siku za hivi karibuni kimekuwa katika mvutano kati ya Limbu na viongozi wenzake, hasa katibu mkuu, akidaiwa kuhujumiwa na vyama vikubwa vya siasa.
Akizungumzia uamuzi huo, Limbu alisema siyo sahihi kwani mkutano huo hauna mamlaka ya kumwondoa kwenye nafasi yake bali ni kamati kuu tu ndiyo ina uwezo huo.
“Sheria ya vyama vya siasa ndiyo inatoa mamlaka. Wajumbe waliokaa hatuna uhakika kama wamefikia akidi ya 65 kama tulivyoelezwa,” alisema Limbu.
Powered by Blogger.