Waziri wa Fedha akiri udhaifu Bandari


Waziri wa Fedha, Saada Mkuya akijibu hoja za taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali iliyowasilishwa bungeni, mjini Dodoma jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
Dodoma. Waziri wa Fedha, Saada Mkuya amesema, Serikali itabadilisha kanuni kwa malengo mahususi ya kudhibiti misamaha ya kodi.
Waziri Mkuya alisema hayo bungeni jana alipokuwa akijibu hoja zilizowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe kuhusu Ripoti ya Ukaguzi Maalumu wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Alisema Serikali itapitia misamaha ili kuhakikisha ile isiyokuwa na tija inaondolewa.
Akizungumzia suala la wafanyakazi wa Mamlaka Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kujilipa posho za safari kiasi kikubwa, Mkuya alisema walikuwa wakijilipa tangu Septemba mwaka 2009 bila kupata kibali cha Msajili wa Hazina kitu ambacho ni kinyume na utaratibu.
“Hivi sasa tunaidhinisha sisi wenyewe na mashirika yote ya umma yanatakiwa kupata kibali cha Msajili wa Hazina,” alisema.
Waziri Mkuya alisema ili kuhakikisha kunakuwapo na ufanisi katika hilo, watendaji wote wa Msajili Hazina wataondolewa kwenye bodi za mashirika ambako ni wajumbe ili kusiwe na mwingiliano wa kimasilahi.
Kuhusu tatizo la mtaji katika Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), alisema Serikali inalishughulikia na kwamba italipa deni la Sh22.5 bilioni zilizoelezwa na kamati.
Kuhusu deni la mashirika ya hifadhi za jamii ambalo Serikali inadaiwa, Waziri Mkuya alisema Serikali ina mpango wa kuuza bondi zake ili iweze kulipa deni hilo lakini akasema hiyo itakuwa baada ya kupeleka waraka wa kusudio hilo kwenye Baraza la Mawaziri.
Serikali za Mitaa
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia akijibu hoja za Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) alisema hatua mbalimbali zimechukuliwa katika mikataba ambayo haina masilahi kwa halmashauri.
Pia, alisema ili kudhibiti ununuzi usiozingatia sheria katika halmashauri, Serikali imeandaa mafunzo kwa wanunuzi wote ili wajue Sheria za Ununuzi na wale wasiozingatia watachukuliwa hatua.
Alisema kutokana na matatizo katika halmashauri mbalimbali nchini, Serikali imewavua madaraka wakurugenzi 21, wakurugenzi watano wamefikishwa mahakamani, 27 wamepewa onyo, pia watumishi 233 wamefukuzwa kazi na 277 wamefikishwa mahakamani, huku 10 kesi zao zimekwisha na wengine wamefungwa na wengine kulipa faini.
Alisema kuhusu udhaifu mkubwa katika ukusanyaji wa mapato wameanzisha utafiti wa vyanzo vipya kwa kuanzisha kodi ya majengo katika halmashauri, ushuru wa nyumba za kulala wageni ambao hapo nyuma haukuwapo.
Waziri Ghasia alisema katika kuzingatia ununuzi wa umma, Serikali itaziwezesha sekretarieti za mikoa kusimamia na kufuatilia miradi yote ili kuhakikishwa inatekelezwa.
Kuhusu mishahara hewa, Waziri Ghasia alisema sasa hivi suala hilo limedhibitiwa kwa kuwa mamlaka za Tamisemi zinatakiwa kuwasilisha majina ya watumishi waliopo kila mwezi ili watumiwe fedha zao moja kwa moja.
Baada ya majibu hayo, Spika Anne Makinda alitoa nafasi ya kujadiliwa kwa ripoti hizo na kumpa nafasi Mbunge wa Ilala (CCM), Mussa Azzan Zungu ambaye alianza kuzungumzia suala la TPA na kupongeza watu kupunguzwa vyeo na akaanza kuzungumzia suala la Uda lakini alizuiwa na Spika kwa madai kwamba kuna kesi mahakamani kuhusu shirika hilo.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju alishauri Bunge kutokujadili suala hilo kwa kuwa kuna mashauri matatu mahakamani jambo lililomkera Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee ambaye alisimama na kupinga hoja ya AG. Baada ya maelezo hayo Spika aliahirisha Bunge.
Powered by Blogger.