Lipumba apandishwa kizimbani,augua ghafla

Wafuasi wa CUF wakimuonyesha Mwenyekiti wao, Profesa Ibarahim Lipumba jeraha la Abdul Kambaya alipokwenda kuripoti katika Kituo cha Kati Cha Polisi, Dar es Salaam jana,  Kambaya alijeruhiwa juzi wakati Polisi wakizuia maandamano, Mtongani juzi. Picha na Anthony Siame
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kushawishi wafuasi wake kutenda kosa la jinai.
Wakimsomea shtaka linalomkabili, mawakili wa Serikali Joseph Maugo na Hellen Moshi walidai jana kuwa kati ya Januari 22 na 27 katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam aliwashawishi wafuasi wake kutenda kosa hilo kinyume cha sheria.
Baada ya kusomewa, Profesa Lipumba ambaye anatetewa na mawakili; Mohammed Tibanyendera, Peter Kibatala, Hashimu Mziray, Fred Kiwelu na John Malya alikana shtaka hilo na kudai kuwa ni la uongo.
Upande wa mashtaka uliieleza Mahakama kuwa upelelezi wa kesi haujakamilika na kuiomba ipange tarehe nyingine.
Mawakili hao wa Profesa Lipumba waliiomba Mahakama impatie mteja wao masharti ya dhamana yenye nafuu. Hakimu Mfawidhi, Isaya Arufani alimtaka Profesa Lipumba kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika kila mmoja akiwa na barua na kitambulisho kila mmoja kusaini hati ya dhamana ya maneno yenye thamani ya Sh2 milioni.
Profesa Lipumba alikamilisha masharti hayo na kuachiwa huru saa 9:42 alasiri.
Baada ya Lipumba ya kuachiwa huru, wafuasi wake waliokuwa wamefurika mahakamani hapo walianza kuimba nyimbo za chama chao huku wakisema rais, rais, rais. Akiwa nje ya viwanja vya Mahakama, Profesa Lipumba aliwataka wafuasi hao kuondoka katika eneo hilo la Mahakama kwa ustaarabu na kwamba Jumapili atatoa taarifa katika Viwanja vya Manzese na kuwataka wananchi kwenda kujiandikisha kwenye Daftari la Wapigakura.
ADVERTISEMENT
Lipumba awasili polisi
Jana, saa 4.05 asubuhi, Profesa Lipumba aliliripoti katika Kituo cha Kikuu cha Polisi Dar es Salaam, muda mfupi baada ya wafuasi wengine 32 wa chama hicho kufika kituoni hapo kuhojiwa.
Kiongozi huyo na wafuasi hao walikamatwa na polisi juzi na baadaye kuachiwa huru na kutakiwa kuripoti jana.
Profesa Lipumba alimaliza kuhojiwa saa 5:20 asubuhi na kutoka nje ya kituo hicho na kuanza kuwaeleza wanahabari jinsi jinsi polisi walivyokiuka taratibu kwa kumkamata na kumdhalilisha wakati alikuwa akiwazuia wanachama wa CUF kutofanya maandamano.
Kitendo hicho kiliwafanya polisi kumchukua kwa mahojiano zaidi, wakieleza kuwa kauli zake zinaweza kuchangia kuvuruga upelelezi wa kesi inayomkabili.
   Augua ghafla
Saa 7.00 mchana alitolewa kituoni hapo na kupelekwa katika Zahanati ya Umoja wa Mataifa (UN), Kinondoni baada ya hali yake kubadilika ghafla wakati akihojiwa.
Alikaa katika hospitalini kwa dakika 39 na kuchukuliwa moja kwa moja hadi katika Mahakama ya Kisutu.
-
Powered by Blogger.