Mawaziri wapya watinga ofisini na rundo la ahadi


Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage
Dar es Salaam. Mawaziri waliobadilishwa wizara na Rais Jakaya Kikwete, wameingia ofisini na kuahidi kutumia muda mfupi uliobaki kuendeleza yale yaliyoachwa na watangulizi wao.
Mabadiliko hayo yalifanyika baada ya mawaziri wawili kujiuzulu kutokana na kashfa ya akaunti ya Tegeta Escrow. Ni Profesa Sospeter Muhongo wa Nishati na Madini na Profesa Anna Tibaijuka wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Rais Kikwete alimteuwa George Simbachawene aliyekuwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuchukua nafasi ya Profesa Muhongo na Lukuvi aliyekuwa Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge akimrithi Profesa Tibaijuka.
Simbachawene alifika wizarani hapo Saa tano asubuhi na kupokelewa na wafanyakazi wa wizara hiyo waliojipanga katika mistari miwili, huku yeye akipita katikati yao.
“Tutaendeleza pale walipoishia wenzetu, tutahakikisha umeme unaendelea kusambazwa nchini kwa kutumia Wakala wa Umeme Vijijini (Rea), mafuta nayo tutashirikiana na (Ewura) Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji kuona bei zinashuka kulingana na bei za soko la dunia.”
Aliongeza: “Gesi nayo tutahakikisha inatumika na kuwanufaisha Watanzania, hususan itakapoanza kutumika kuzalisha umeme katika Kituo cha Kinyerezi.”
Naye Mwijage alisema: “Nimeletwa katika wizara ambayo nina uzoefu nayo kutokana na kuwa katika sekta ya nishati tangu mwaka 1984, hivyo kama ni mchezo umepata mchezaji.”
Kwa upande wake Waziri wa Ardhi, Nyumba na maendeleo ya Makazi, Lukuvi alisema: “Uamuzi ya kutatua migogoro ya ardhi haihitaji fedha, hivyo watendaji wanatakiwa kutumia akili ili mwananchi aweze kupata haki zao za msingi.”
ADVERTISEMENT
Awali, aliyekuwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi, Profesa Anna Tibaijuka amekabidhi ofisi kwa waziri Lukuvi, huku akimkabidhi miradi ambayo hajaitekeleza katika kipindi chake cha uongozi, ikiwamo mradi wa mpango mji wa Dar es Salaam.
Alisema miradi hiyo ameitekeleza kwa kiasi kikubwa, huku mingine ikiwa na changamoto na kumtaka waziri Lukuvi kutumia akili ya ziada kuikamilisha.
Hata hivyo, Tibaijuka alisema mipango miji haijapewa umuhimu na kuitaka Serikali kuangalia upya suala la upangaji miji.
Tibaijuka aliitaja miradi mwingine ni mradi wa Mji wa Kigamboni unaohitaji Sh14.6 bilioni kukamilika, Sera ya Watumishi wa Sekta ya Ardhi na Sera ya ubia na Serikali kumiliki mashamba makubwa.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anna Kilango alisema ingawa wizara hiyo ina changamoto zake, atahakikisha kuwa utekelezaji unafanyika kwa kuzishirikisha sekta zote.
“Suala la elimu siyo la waziri pekee, kuna wadau wa elimu, taasisi, walimu wenyewe na wakurugenzi,” alisema.
Kilango alisema anafahamu changamoto za kada hiyo kwa sababu amewahi kufundisha na kuahidi kuzifanyia kazi.
Imeandikwa na Ibrahim Yamola, Pamela Chilongola na Laura Paul
Powered by Blogger.