Watayarishaji filamu nao waibuka


Chiki Mchoma
Dar es Salaam. Lile sakata la kushushwa kwa bei za filamu, limeingia katika sura mpya baada ya watayarishaji wa filamu nchini kujitokeza na kutoa malalamiko yao kwa Bodi ya Filamu, kuhusu kutoshirikishwa katika vikao vinavyoendelea.
Bodi ya Filamu kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda na Biashara, TRA, TBS, imekuwa ikifanya vikao vya ndani zaidi ya viwili sasa na wasambazaji wa filamu ili kuzungumzia suala ya bei ya filamu.
Mtayarishaji wa filamu Mike Sangu aliliambia Mwananchi kuwa kitendo cha bodi hiyo kuendesha kikao pasipo wao kushirikishwa, kimewaumiza na kwamba wanahitaji haki itendeke ili biashara ya filamu isonge mbele kwa manufaa.
“Tunaiomba serikali kupitia vyombo vyake vyote vinavyoshiriki haya masuala ya filamu, kusifanyike mkutano wa aina yoyote ile kuzungumzia bei ya filamu bila kushirikisha maprodyuza, sisi ndiyo wenye filamu na ndiyo tunaotengeneza sasa iweje tusishirikishwe,” alisema Sangu na kuongeza:
“Inashangaza ikiwa msambazaji atapanga yeye bei, badala ya sisi ambao ndiyo wazalishaji, kwa sababu tungeweza kusambaza wenyewe, lakini tunawauzia wao ili wafanye biashara, hivyo lazima na sisi tujue nini kinaendelea, kikao cha pili tulipata taarifa juu juu kupitia watu tuliamua kuhudhuria ili kujua bei wanazopanga na sisi tuwauzie kwa bei gani, badala yake tulifukuzwa na kikao kikavunjika.”
Mwongozaji na mtayarishaji filamu Chiki Mchoma naye alisema kumekuwa na upotoshaji kwamba msambazaji mkubwa ndiye aliyeamua kushusha bei ya filamu, lakini wao ndiyo waliomtaka afanye hivyo.
ADVERTISEMENT
“Kuna mkanganyiko wa bei kutoka kwa msambazaji mpaka kwa mlaji ndiyo umesababisha migogoro hii, ilianzia kwetu baada ya kuona hali halisi ya mfumo wa bei ya filamu bado haukui, soko linazidi kuyumba tuligundua kwamba wizi wa filamu umekuwa ndiyo mtihani wetu, tukaona kuna kila sababu ya kuhakikisha tunaudhibiti, tulimuomba msambazaji mkuu ambaye ni Steps Entertainment kuhakikisha kwamba anatafuta mbinu mbadala,” alisema Mchoma.
Alipoulizwa kuhusu sakata hilo, Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu na Ukaguzi wa Michezo ya Kuigiza Tanzania, Joyce Fisoo alisema hawajawatenga watayarishaji, bali walizingatia upande mmoja kwanza kwa kukaa na wasambazaji ili maamuzi yatakayofikiwa wayatangaze kwa wasanii wote kwa ujumla.
“Tunapoendesha vikao vinavyohusu masuala ya filamu, huwa tunafanya kwa makundi, sasa suala linalowahusu wasambazaji, hatuwezi kukaa na watayarishaji lazima tutashindwa kufikia muafaka, sisi hatubagui mtu bali kila mwana tasnia huwa tunakutana naye na kuzungumza naye,” alisema Joyce.
Alisema suala la kibiashara limewafanya wazungumze na wafanya biashara ambao ni wasambazaji, bali watayarishaji nao wangeshirikishwa baadaye.
“Kikao cha wiki jana tulikaa na Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda na Biashara, TBS, TRA, Cosota na wengineo ili kufikia muafaka. Kikao cha juzi hakikuwa cha kupanga bei bali kilihusu maadhimio ya kikao kilichofanyika Desemba 30 mwaka jana,” alisema Joyce.
Alisisitiza kuwa watayarishaji bado wana nafasi yao na wataitwa ili kutoa ushauri wa nini kifanyike kuhusu sakata hilo, kwani serikali ilihitaji kupata taarifa kutoka upande wa wasambazaji kwanza.
Powered by Blogger.