Watu 300 wahofiwa kula sumu Bulyanhulu

Shinyanga. Zaidi ya watu 323 wakazi wa Kijiji cha namba 9 katika Kata ya Bulyanhulu wilayani Kahama mkoani Shinyanga, wanahofiwa kula sumu kali aina ya sodium cyanide inayotumiwa katika Mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu unaomilikiwa na Kampuni ya Acacia.
Hali hiyo imetokana na mvua kubwa kunyesha na kubomoa bwawa kubwa la ndani ya mgodi huo wa Bulyanhulu, ambalo hutunza sumu hiyo na kusababisha maji hayo kutiririkia kwenye bwawa la nje linalotumiwa na wananchi.
Ofisa Uhusiano wa Kampuni ya Acacia, Necta Foya alisema jana kuwa, maji hayo yalibomoa pia bwawa la nje na kwenda vijijini.
Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya alisema baada ya maji hayo yanayosadikiwa kuwa na sumu kubomoa bwawa la nje yalisambaa pia kwenye mashamba ya watu.
Mpesya, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kahama, alisema katika eneo hilo takriban hekta 15 za mpunga zimeathiriwa na sumu hiyo, zikiwamo bustani za nyanya.
Mpesya alisema ili kunusuru maisha ya wananchi hao, huduma zote za maji ya kunywa mifugo na binadamu kwenye visima na mabwawa zimefungwa na tayari mgodi huo umevuta kwa muda maji ya bomba ambayo sasa wananchi hao wanayatumia.
ADVERTISEMENT
Hata hivyo, Mpesya alisema tayari watalaamu wa afya na mazingira wamechukua sampuli ya maji hayo pamoja na nyanya kwenye bustani inayodhaniwa kunyonya maji yenye sumu hiyo na kupeleka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali
Pamoja na hali hiyo, jana wananchi wote wanaoishi eneo hilo walipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Kahama kupimwa afya zao, zoezi ambalo hadi tunakwenda mitamboni lilikuwa likiendelea kufanywa na madaktari wote kutoka halmashauri tatu za Wilaya ya Kahama.
Alisema uamuzi huo wa kuwapima wananchi unatokana kuhisi kuwa wametumia maji yaliyochanganyika na sumu hiyo.
Pia, Mpesya alisema kamati yake ilikubaliana watu hao wapimwe wakati hatua nyingine zikiendelea kufanywa ikiwa ni pamoja na kusubiri majibu kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kujua sumu hiyo imeingia kwenye eneo hilo kwa kiasi gani.
“Tumeliona hilo tukasimamisha shughuli zote katika eneo hilo zikiwamo za kilimo na baada ya kupata hali halisi ya madhara yaliyojitokeza kwenye eneo hilo, ndiyo hatua ya kuwalipa fidia wanachi hao zitafuata,” alisema Mpesya.
Powered by Blogger.