UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI

SURA YA NNE

            Uhakiki ni kazi au kitendo cha kutafakari, kuchambua na kufafanua kazi ya fasihi ili kuweka bayana maadili na ujumbe uliomo katika kazi ya fasihi. Hivyo mhakiki sharti asome kazi ya fasihi andishi au kusikiliza masimulizi kwa makini ili aweze kuyahakiki
            Mhakiki ni mtu anayejishughulisha na kazi za kisanaa hususan za kifasihi za wasanii asilia. Mhakiki ni mchambuzi na mfafanuzi wa kazi za kifasihi. Ni jicho la jamii kwani ndiye agunduaye mazuri yaliyomo katika kazi hiyo, hali kadhali mabaya (hatari) yaliyopo katika maandishi hayo kwa jamii husika .
            Mhakiki ni bingwa wa kusoma na kuchambua vipengele vya fani na maudhui katika maandishi ya fashihi. Kwa mantiki hiyo mhakiki ni chombo madhubuti cha jamii inayohusika cha kuleta maendeleo katika jamii. Kwa kuzingatia haya anawajibika kuwa mwaminifu, mkweli, asiyeogopa kuweka wazi ubaya uliomo katika maandishi ya mwandishi asilia, na asiyependelea waandishi Fulani Fulani kwa sababu zisizona maslahi kwa jamii. Pamoja na hayo uhakiki wa kazi za fasihi unaambatana na mambo yafuatayo:
(a)Kuisoma kazi ya fasihi kwa makini na kuielewa
(b)Kuchambua vipengele vya fani na maudhui katika kazi hiyo
(c)        Kueleza ubora na udhaifu wa matumizi ya vipengele vya fani na maudhui katika kazi hiyo.
Kwa mujibu wa maelezo hayo ni wazikuwa mhakiki anabeba dhima zifuatazo:
1.Kuchambua na kuweka wazi funzolitolewalo na kazi ya fasihi.
2.         Kuchambua na kufafanua taswira (picha za kisanii) zilizotumika katika kazi ya mwandishi.
 
3.         Kumshauri na kumtia moyo mwandishi ili afanye kazi bora zaidi (hivyo mhakiki                pia ni mwalimu wa mwandishi)           
4.         Kumwelekeza na kumchochea msomaji kusoma na kupata faida zaidi ya ambayo               angeipata pasipo dira ya mhakiki (mhakiki ni mwalimu na daraja kati ya                     mwandishi na jamii)
5.         Kuhimiza na kushirikisha fikra za kihakiki katika kazi za fasihi.
6.         Kukuza kiwango cha utunzi na usomaji wa kazi za fasihi.
           
7.         Kutafuta na kuweka sawa nadharia za fasihi teule.
8.         Kuthamini na kuheshimu kazi za waandishi kwa kuzitendea haki
VIGEZO VYA UHAKIKI
            Kwa kuzingatia kwamba fasihi husawiri jamii katika mfumo mzima wa maisha ya jamiii hiyo mathalani shughuli zinazofanywa katika jamii husika, basi si budi kuzingatia yafuatayo katika kupima kazi ya fasihi:
(i)         Ukweli wa mambo yanayoelezwa – mhakiki kama hakimu na daraja atajiuliza, je,               ni kweli yaliyoelezwa katika kazi hiyo yanatendeka? Kama anahakiki habari             kuhusu ubakaji au rushwa – Anapaswa kujiuliza, Je ni kweli mambo hayo yapo                     katika jamii ya Tanzania?
(ii)        Uhalisia wa watu, mazingira na matukio katika jamii. Hapo mhakiki analinganisha wahusika wa  kazi husika na watu halisi ili kuona kama jamii zungumziwa ina watu wanaotenda kama wahusika waliotumika. Mfano habari inaeleza kuwa mganga wa kienyeji aliwapaka dawa watoto wakawaona wachawi,             mhakiki anaweza kujiuliza kama kweli hilo linaweza kutokea katika jamiii husika.
(iii)       Umuhimu wa kazi hiyo kwa jamii husika lazima uzingatiwe. Jambo linalozungumzwa linaweza kuwa la kweli na linalihalisika lakini lisiwe na umuhimu mkubwa katika jamii kiasi cha kuvuta utayari wa jamii hiyo.                 
            vigezo hivi ndivyo vitumikavyo kupimia vipengele vya maudhui,(dhamira, ujumbe, migogoro, mafunzo na falsafa). Na vipengele vya fani, (muundo, mtindo, matumizi ya lugha, wahusika, na mandhari)
            Kwa mfano;
Hadithi inayosifu maisha ya vijijini na kuwashauri vijana wasikimbilie mijini, lazima ipimwe kwa kuzingatia ukweli uliopo vijijini. Mhakiki atajiuliza maswali ya dhamira, mafunzo, migogoro, ujumbe na falsafa kama haya:- Je, ni kweli kuwa wanavijij wana maisha bora kuliko mjini? Je, wanavijiji wanahuduma za lazima kama hospitali zenye waganga na dawa? Je, wanavijiji wana maji salama kwa ajili yao, mifugo na mazao yao? Je, mazao ya wanavijiji yananunuliwa kwa fedha taslimu na mapema? Je, wanavijiji hawa bughudhiwi na wezi, waporaji n.k?
            Hali kadhalika mhakikia atajiuliza  maswali kadhaa kuhusu kukimbilia mijii, kwa mfano; Je kijana anapokimbilia mjinii ana uhakika wa kupata kazi? Je, kazi kama kuuza machungwa au karanga mijini ni shughuli inayoweza kumkimu huyo kijana? Na Je, vijana wasio na kazi mijini hawalazimiki kuiba au kufanya uhalifu mwingine?
Hatimaye mhakiki atajiuliza maswali kuhusu ufumbuzi unaopendekezwa na mwandishi katika kazi yake, mfano tunaozungumzia mhakiki atajiuliza, je, mwandishi anashauri nini licha ya kusema vijana wabaki vijijini? Je, ni mambo gani anayopendekeza mwandishi kuhusu kuinua shughuli za kiuchumi vijijini? Je., suluhu la mwandishi (mapendekezo) linawezekana (ni yakinifu) au ni la kinjozi tu (la kidhanifu). Msingi wa maswali yote haya ni kujaribu kutambua ukweli, uhalisi na umuhimu wa kauli za mtunzi.
Katika uhakiki wa fani, vipengele vya fani huangaliwa jinsi vilivyotumika na kupima usahihi wake kimatumizi, na hapa maswali huweza kuwa hivi:
-Je, kazi husika ina muundo gani?
-Wahusika wamechorwaje?
-Je, wahusika wanahalisika katika jamii husika?
-Je,mpangilio wa maneno unavutia wahusika?
-Matumizi ya tamathali mbali mbali yanatosheleza haja?
-Misemo na methali zilizotumika zinafaaa hapo zilipotumika au zimepachikwa tu?
VIPENGELE VYA FANI NA MAUDHUI KATIKA KAZI ZA FASIHI ANDISHI:
Riwaya na tamthiliya:
A. Maudhui.
            Maudhui katika kazi ya Fasihi ni jumla ya mawazo yote yanayozungumziwa pamoja na mtazamo wa mwandishi juu ya mawazo hayo. Maudhui hujumlisha mawazo, pamoja na mafunzo mbali mbali yaliyomsukuma msanii hadi kutunga kazi Fulani ya Fasihi.
Vipengele vya maudhui:
1.         Dhamira
                        Hili ni wazo kuu au mawazo mbali mbali yanayojitokeza katika kazi ya fasihi ambayo mwandishi huyajengea hoja. Dhamira hutokana na jamii na zipodhamira kuu na dhamira ndogo ndogo. Dhamira kuu ni zile za kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni. Dhamira kuu ndicho kiini cha kazi ya fasihi na dhamira ndogondogo ni zile zinazoambatana na dhamira kuu.
2. Migogoro  
Migogoro ni mivutano na misuguano mbali mbali ambayo huibuliwa na mwandishi katika kazi ya fasihi. Mgogoro kati ya wahusika ama vikundi vya wahusika, familia zao matabaka yao n.k. Migogoro hii mara nyingi hujikita katika mahusiano ya kijamii na ndipo tunapata migogoro ya :
            (a)        kisiasa
            (b)        kiuchumi
            (c)        kiutamaduni
            (d)       kinafsia (kifikra)
3.         Ujumbe na maadili
            Ujumbe katika kazi ya fasihi ni mafunzo mbali mbali yapatikanayo baada ya kuisoma kazi ya fasihi. Ujumbe huwa sanjari na maadili mbali mbali ambayo mwandishi amekusudia jamii iyapate.
4.         Mtazamo
Ni hali ya kuyaona mambo katika maisha kwa kuzingatia mazingira             aliyonayo msanii mwenyewe. Wasanii wana mitizamo ya aina mbili:
(a)Mtazamo wa kiyakinifu – mtazamo huu ni ule wa kuyaangalia mambo    waziwazi na kuyaelezea kwa jamii kupitia kazi za kifasihi. Msanii anayeunga mkono mtazamo huu huutazama ulimwengu au mazingira yanayomzunguka binadamu kisayansi na hivyo huelezea mambo katika uhalisia wake.
            (b)        Mtazamo wa kidhanifu – msanii mwenye mtazamo wa kidhanifu hujadili mambo na kuyatolea masuluhisho yaliyoegemea katika kudhani tu pasipokuzingatia uhalisia wa mambo. Huchukulia ulimwengu kama kitukinachobadilika kulingana na matakwa ya Mungu
5.         Falsafa:
Huu ni mwelekeo wa imani ya msanii. Msanii anaweza kuamini kuwa,        mwanamke si kiumbe duni kama wengine wanavyoamini au, kwa wale wapinga usawa, wanaweza kuwa na falsafa ya kumwona mwanamke kuwa kiumbe duni au chombo cha starehe.
            Hivyo falsafa inatakiwa ichambuliwe kwa kuzingatia jinsi kazi hiyo ilivyoutazama ulimwengu na kuueleza ukweli juu ya mambo mbali mbali na ukweli huo lazima uhusishwe na binadamu.
6.         Msimamo:
Hii ni hali ya mwandishi kuamua kushikilia na kutetea jambo Fulani bila                 kujali kuwa jambo analolishikilia linakubalika au la.
            Misimamo ya mwandishi huweza kuwekwa katika makundi (kategoria) matatu:
(a)Msimamo wa  kimapinduzi – mwandishi mwenye msimamo huu huyajadili masuala / matatizo yanayoihusus jamii yake na            kuonesha bayana – mbinu (njia) za kuondokana na matatizo hayo
(b)Msimamo usio wa kimapinduzi,  mwandishi mwenye msimamo huu huwa na asili ya woga inayomfanya kuyajadili mambo kwa kufichaficha na hivyo kushindwa kuleta athari chanya katika mapinduzi.kutokana na kutoonesha bayana masuluhisho ya matatizo aliyoyajadili.
           
7. Mtazamo
Ni jinsi msanii anavyoyatazama mambo katika ulimwengu wa kifasihi. Hapa tunapata mitazamo ya aina mbili.
(a)          Mtazamo wa kiyanifu ambao unaegemea katika kuyajadili mambo kiuhalisia, msanii mwenye mtazamo huu hujadili mambo kama yanavyojitokeza katika jamii. Kwa ujumla mtazamo huu hushadadiwa sana na wanasayansi ambao huhitaji kuthibitisha kila kitu kisayansi.
(b)          Mtazamo wa kidhanifu, huu una misingi yake katika kudhani kuwa Mungu ndiye suluhisho la kila kitu hivyo waandishi wenye mtazamo huu hujibainisha wazi kupitia kazi zao hasa kwa kujadili mambo kiujumlajumla mathalani “kuon a kuwa mapenzi bora ndiyo suluhisho la matatizo katika jamii” huu ni mtazamo wa kidhanifu.Wengi wa wanadini hufuata mtazamo huu.
B: Fani
Fani katika fasihi ni ule ufundi wa kisanaa anaoutumia msanii katika kufikisha ujumbe wake kwa jamii inayohusika.
VIPENGELE VYA FANI
1.         Muundo
Ni mgawanyo, mpangilio na mtiririko wa kazi hiyo kwa upande wa visa      na matukio. Ni jinsi msanii wa kazi ya fasihi alivyoifuma, kuiunda na kuunganisha tukio moja na lingine, sura moja na nyingine, ubeti na ubeti, na hata mstari wa ubeti na mwingine.
AINA ZA MIUNDO:
(a) Muundo wa moja kwa moja/msago
Huu ni muundo wa moja kwa moja ambao matukio huelezwa kwa kuanza  la mwanzo hadi la mwisho. Kwa mfano, mhusika huzaliwa, hukua, huchumbia au huchumbiwa, huoa au huolewa, huzaa watoto, huzeeka, hufa. Riwaya ya  “Kuli”imetumia muundo huu. Katika riwaya tunamwona Rashidi, akizaliwa, akiwa,           anaanza kazi, anaoa, anaanza harakati za kudai haki za makuli namwisho anafungwa.
            (b)        Muundo wa kioo/rejea
Huu ni muundo unaotumia mbinu rejeshi ambayo huweza ama         kumrudisha nyuma msomaji wa kazi ya fasihi katika mpangilio wa matukio yake au kuipeleka mbele hadhira ya kazi hiyo. Riwaya ya “Zaka la Damu” imeutmia muundo huu.
           
            (c)        Muundo wa rukia
           
                        Huu ni muundo ambao visa na matukio hurukiana. Katika muundo huu kunakuwa na visa viwili ambavyo hurukiana katika kusimuliwa kwake, na mwisho visa hivi huungana na kujenga kisa kimoja. Mfano Njama.
2.         Mtindo:
           
                        Mtindo katika kazi ya fasihi ni ile namna ambayo msanii huiwasilisha kazi yake kwa jamii. Ni upangaji wa fani na maudhui katika kazi ya fasihi kwa njia ambayo hudokeza upekee wa mwandishi.
            Dhima ya mtindo:
·         Humwezesha msomaji kujua hisia za mwandishi juu ya aliloliandika.
·         Hudokeza kiasi cha hisia na mwamko wa wahusika katika hadithi.
·         Kuonesha mtiririko (muwala) wa matukio.
·         Kuumba ulimwengu ambao utabeba maono ya msanii. Lengo ni kuepusha mifarakano inayoweza kujitokeza. Kwa mfano, katika riwaya ya “Kusadikika” ambayo imeumbiwa ulimwengu ulioko angani na nchi inayoelea.
Katika mtindo huangaliwa:
-Matumizi ya lugha
-Nafsi zilizotumiwa
-Matumizi ya monolojia (maelezo/ masimulizi) na dialojia (majibizano).
-Mbinu ya kutumia tanzu nyingine za fasihi simulizi
-Matumizi ya hadithi ndani ya hadithi
-Matumizi ya barua n.k.
Jambo la msingi katika mtindo ni lugha, na ndiyo inayotofautisha fasihi na sanaa nyingine kama vile uchoraji, uchongaji, usukaji, ufinyazi n.k. Msanii wa fasihi chombo chake (nyenzo) ni lugha.
3.         Wahusika:
            Wahusika ni watu, vitu ama viumbe waliokusudiwa kubeba dhamira mbalimbali kwa lengo la kuwakilisha tabia za watu katika kazi ya fasihi.
Aina za Wahusika:
(a)        Wahusika Wakuu:
            Hawa ni wale ambao wanajitokeza kila mara katika kazi za fasihi, hutokea tangu mwanzo hadi mwisho. Wahusika hawa hubeba kiini cha dhamira kuu na maana ya hadihti yote. Vituko, visa na matendo yote hujengwa         kuwahusu au kutokana nao. Mara nyingi jambo hili limewafanya wahusika wakuu wa kazi ya fasihi wawe “midomo” ya wasanii, na pia vipaza sauti vya watunzi wa kazi za fasihi. Wahusika wakuu hasa wameelezwa kwa  mapana na marefu juu ya maisha na tabia zao ili kuukamilisha unafsi wao.
(b)        Wahusika wadogo / wasaidizi
            Hawa hujitokeza hapa na pale katika kazi ya fasihi ili kuukamilisha ulimwengu wa kazi hiyo. Hawa husaidia kuijenga dhamira fulani katika kazi ya fasihi na hasa hubeba dhamira ndogo na kwa minajili hiyo huitwa wahusika wadogo ingawa wakati Fulani husaidia kujenga na kuikamilisha dhamira kuu.
(c)        Wahusika wajenzi:
            Hawa ni wahusika ambao wamewekwa ili kukamilisha dhamira na maudhui Fulani, kuwajenga na kuwakamilisha wahusika wakuu na wasaidizi. Wahusika wakuu na wadogo huweza kuwekwa katika aina tatu:
            (i)         Wahusika Bapa;
Hawa ni wahusika ambao hawwabadiliki kitabia wala          kimawazo kulingana na mazingira au matukio ya wakati wanayokutana nayo. Wahusika bapa huweza kugawanywa kwenye makundi mawili:
Wahusika Bapa sugu-
Hawa huwa sugu katika hali zote, kiasi kwamba hata tuwaonapo mahali pengine hali zao ni zile zile, wao ndio huhukumu hushauri na kuongoza tu na si vinginevyo wanakuwa kama madikteta. Mfano” Bwana Msa” katika riwaya ya “Mzimu wa watu wa kale” ya M.s. Abdulla.
Wahusika bapa – vielelezo
Hawa pamoja na kutobadilika kwao, hupewa majina aghalabu ya kiishara ambayo – humfanya msomaji aelewe tabia na matendo yao. Mfano: “Waziri Majivuno”, “Adili”, Utubora” na “Karama” katika kazi za “Shaaban Robert” ni mfano wa wahusika bapa wala, kiasi ambacho anaondoa sehemu zote za sifa za wahusika huyo.
           
(ii)        Wahusika duara / mviringo
Hawa ni wahusika ambao hubadilika kitabia, kimawazo ama kisaikolojia. Maisha yao hutawaliwa na hali halisi yamaisha. Hivyo wanavutia zaidi kisanii, kwani husogeza hadithi ielekee kwenye hali ya kutendeka au kukubalika na jamii.Mfano, (Rose mistika) , Josina (pepo ya mabwege)
(iii)       Wahusika shida / foili
Hawa ni wahusika ambao huandamwa na shida, misukosuko na taabu na wahusika hawa hutokea kati ya wahusika bapa na duara. Wahusika shida huwategemea wahusika duara au bapa ili waweze kujengeka. Mfano: “Najum” katika riwaya y’’ Mzimu wa Watu wa Kale’’ na m.s Abdulla.
4.         Matumizi ya lugha
Lugha ndiyo njia (nyenzo) aitumiayo msanii wa fasihi kuyaelezea mambo mbali mbali yahusuyo jamii kwa njia ya ubunifu na usanii. Hivyo lugha ndiyo             mzizi wa kazi ya fasihi na bila yenyewe kuwapo haiwezekani kuwa na fasihi.
            Vipengele vya lugha
                        (i)         Methali
            Methali ni tungo fupi zenye hekima na busara ndani yake ambazo hutumika kama kiungo cha lugha kwa lengo la kufunzia na kupenyeza  hekima kwa jamii kupitia fashi.
Methali pia hutumika kujenga mandhari ya kiutamaduni ya kuaminika kuhusu jamii itumiayo methali hizo. Hivyo huweza kusemakuwa pale ambapo methali zimetumika katika kazi mbali mbali za fasihi, nyingi zimejenga fani na maudhui ya kazi hizo.
(ii)        Misemo na nahau
Matumizi ya misemo na nahau katika kazi za fasihi hushabihiana     sana na yale ya methali. Misemo na nahau hutumika kwa madhumuni anuai kama vile kutambulisha mazingira, na wakati husika wa kazi hiyo, lakini pia kupamba kazi ya fasihi pamoja na kuitajirisha lugha ya msanii katika Kazi yake.
(iii)       Tamathali za semi
Tamathali za usemi ni maneno ambayo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia msisitizo, nguvu na maana katika kazi zao, hali kadhalika kuboresha mtindo wa kazi zao. Wakati mwingine huwa na lengo la kupamba kazi ya fasihi na kuongeza utamu wa lugha. Kuna aina nyingi zatamathali za usemi kama ifuatavyo;
(a)Tamathali za mafumbo
Dhihaka (sarcasm)
Hii ni tamathali ya dharura na ina lengo la kumweka mtu katika hali duni kupita kiasi, lakini kwa mbinu ya mafumbo
Mfano:
“Adella alikuwa msichana msafi sana. Ndiyo maana kila, mara alipata kupaka mafuta yaliyonukia na kukaribisha  nzi  walioleta matatizo makubwa”.
Tafsida (Euphemism)
Hii hupunguza ukali wa maneno au utusi katika usemi 
Mfano:
-Kujisaidia au kwenda haja badala ya kunya au kukojoa.
-Kuaga dunia badala ya kufa n.k
Kejeli / shitizai (Irony)
Hii imekusudiwa kuleta maana iliyo kinyume na ile iliyokusudiwa ama kinyume na ukweli ulivyo. Lengo lake ni kutaka kuzuia matatizo na migongano pindi itumikapo kwa lengo maalumu la kufundisha na kuasa.
Mfano:
-Mtu ni mchafu, lakini anaambiwa –sijamwona mtu msafi kama                   wewe.
-Mtu ni adui, lakini anambiwa – wewe ni rafiki mpenzi
-Mtu ni mweusi kama mkaa – anaitwa cheupe.
Kijembe / kiringo (Innuendo)
Huu ni usemi wa mzunguko, ni usemi wa kimafumbo wa kumsema mtu kwa ubaya.
(b)Tamathali za mliganisho
Sitiari (Metaphor)
Ni tamathali inayolinganisha matendo, vitu au tabia ya vitu vyenye maumbile tofauti bila kutumia viunganishi linganishi
Mfano:
-Maisha ni moshi
-Pesa ni maua
-Penzi upepo
-Misitu ni uhai
Tashibiha (simile)
Tamathali inayolinganisha vitu kwa kutumia maneno kama vile mfano wa, kama, mithili ya , sawa na , n.K
Mfano;
-Ana sauti tamu sawa na ya chiriku
-Ana maringo kama twiga
-Ananyata mithili ya kinyonga
-Ana ng’ang’ania kama kupe.
     
Tashihisi (personification)
Tamathali hii huvipa vitu sifa walizonazo binadamu (hupewa uwezo walionao binadamu)
Mfano:
-Mvua iliponyesha misitu ilipiga makofi
-Mawimbi yalitabasamu  kwa upepo wa kusi.
Lakabu
Katika tamathali hii uhusiano wa maneno mawili kisarufi hugeuzwa na pengine huwekwa kinyume na taratibu za kisarufi zilivyo
Mfano:
-Baridi kali ilimkaribisha (lakini mtu ndiye mwenye uwezo wa kukaribisha)
-Giza liliwapokea walipokuwa wakiingia pangoni
(c)Tamathali za msisitizo na nyinginezo
Mubaalagha (Hyperbole)
Hii hutia chumvi kuhusu uwezo wa viumbe, tabia zao na hata sifa zao kwa madhumuni ya kuchekesha au kusisitiza
Mfano:
-Loo! Hebu muangalie mrembo yule! Ana mlima wa kiuno
-Tulimlilia Nyerere hadi kukawa na bahari ya machozi
-Mrembo yule hubeba kila aina ya silaha na huwatia wazimu wanaume wote anaokutana nao.
Taashira / metonumia (metonymy)
Katika tamathali hii jina la sehemu ya kitu kimoja au la kitu kidogo kinachohusiana na kingine kikubwa hutumiwa kuwakilisha kitu kamili.
Mfano:
-Jembe huwakilisha mkulima
-Kutabasamu huwakilisha furaha
-Mvi huwakilisha uzee
-Kalamu huwakilisha mwanafunzi / msomi.
Majazi
Hii ni aina ya sitiari ambayo itajapo sehemu tu ya kitu hapo hapo sehemu hiyo huashiria na kuwakilisha kitu hicho.
Mfano:
Roho – mtu
-Masikini, ajali ile ilipoteza roho tano hapo hapo]
     
Taniaba (Antonomasia)
Hii ni tamathali ambayo kwayo jina la mtu binafsi hutumiwa kwa watu wengine wenye tabia, mwenendo, hali au kazi sawa na ya mtu huyo.
Mfano:
-Yesu – mkombozi
-Yesu wa kwanza wa Afrika alikuwa Kwame Nkrumah
-Nyerere alikuwa Yesu wa kwanza Tanzania
Tabaini (antithesis)
Hii ni usemi unaosisitiza jambo kwa kutumia maneno ya ukinzani (unyume)
Mfano:
-Mwanadamu hupanga Mungu hupanga
-Amekuwa mrefu si mrefu, mfupi si mfupi ni wa kadiri
-Usimwamini mtu, yu acheka machoni, rohoni ana mabaya.
(d)Mbinu nyingine za kisanaa
Takriri (Tautology)
Hapa yanakuwepo marudio kwenye sentensi au kwenye usemi na lengo ni kusisitiza
Mfano:
-Dunia ni ngumu jamani, ni ngumu
-Haba na hapa hujaza kibaba
Mdokezo (Aposiopesis)
Hapa msemaji au mwandishi hukatiza maneno au huacha maneno bila kutaja kitu au maneno ambayo kwa  kawaida ni wazi na huweza kujazwa kwa ubunifu.
     
Mfano:
-Ally alipokuwa analia alisema………………
-Watu wengi huambukizwa ukimwi kwa kushiriki ………………
Tashtiti (Rhetorical Questions)
Ni mbinu ya kuuliza maswali kwa jambo ambalo majibu yake yanafahamika.
     
Mfano:
-Asha na uzuri wake amekufa?
-Loo! Asha ametutoka?
-Hatakuwa nasi tena?
Nidaa (!)
Huu ni msemo unaoonesha kushangazwa na jambo Fulani. Msemo huu huambatana na alama ya kushangaa
Mfano:
-Baba ndiye amefariki!
-Ah! Havijawa nimekutoroka!
-Hakika nitakupenda!
Mjalizo (Asyndeton)
Hapa huwa ni mfuatano tu wa maneno yasiyo na viunganishi vyovyote bali hutengwa kwa alama ya mkato(,)
Mfano:
     
-Nilikaa, nikasubiri, nikachoka
-Nilipanda, nikapalilia, nikavuna, nikauza, nikajenga nyumba.
Tanakali sauti (onomatopeia)
Ni mbinu ya kuiga sauti za milio mbali mbali. Milio hii ni ya wanyama, magari, vitu n.k
Mfano:
-Alitumbukia majini chubwi!
-Alidondoka chini pu!
(e)        Taswira
            Ni picha zinazojitokeza ndani ya mawazo ya msomaji au msikilizaji wa kazi ya fasihi. Matumizi mazuri ya taswira na ishara hutegemea ufundi wa yanayomzunguka yeye na jamii yake pamoja na historia za maisha                        azijuazo.
Aina za Taswira
(i)Taswira za hisi
     Taswira hupenyeza hisia na kuzigandisha akilini mwa msomaji au msikilizaji na kunasisha ujumbe wa mwandishi. Taswira hizi hushughulikia hisi za ndani, na kuweza kumfanya msomaji au msikilizaji awe na wasi wasi aone woga, apandwe na hasira, ahisi kinyaa, n.k
mfano:
             
Akadharau! Siwezi kula chakula kama hicho! Rojorojo nyororo kama limbwata, mfano wa kohozi lenye pumu,liingie katika koo langu lililozoea kuku wa mrija
-Maelezo hayo humfanya mtu akinahi na kutaka kutapika mara akisoma rojorojo, kunyororoka mfano wa kohozi lenye pumu.
(ii)taswira za mawazo / kufikirika
Hizi zinatokana na mawazo yahusuyo mambo yasiyoweza    kuthibitika. Mambo kama kifo, pendo, uchungu, fahamu, sahau, raha n.k
Mfano:
Kifo umefanya nini? Umeninyang’anya penzi langu bila huruma?    kumbuka, nilimpenda nikapoteza fahamu, kifo ukazidi kunidunga sindano ya makiwa?
(iii)       Taswira zionekanazo
Hizi ni picha ambazo hujengwa kwa kutumia vielelezo tunavyovijua vile vinavyofahamika katika maisha ya kila siku.
Mfano:
Dakika haikupita mijusi wawili wliokuwa wamebebana walipita haraka. Midomo yao ilikuwa myekundu. Ghafla walikutana nanyoka aliyeonekana mnene tumboni. Hapana shaka alikuwa amemeza mnyama.
5.Mandhari / mazingira       
Ni sehemu ambamo kazi ya fasihi inafanyika. Mandhari yaweza kuwa ya kubuni kama” Kusadikika” na “Kufikirika” au halisi (ya kweli) mfano mandhari ya Dar es salaam, Arusha n.k. kwa Tanzania.
  6   Jina lakitabu / Jalada la kitabu
Hapo  tunaoanisha jina la kitabu na yaliyoelezwa ndani ya kitabu hicho.      Mfano”Kiu ya Haki”, jina hili linasadifu vipi yaliyomo ndani ya riwaya hiyo. Je, kweli yaliyoelezewa yanadhihirisha kiu ya haki? Pia tunaangalia picha mbali             mbali zilizochorwa juu ya jalada la kitabu na kutafsiri kifasihi jinsi picha hizo zilivyotumika.
7.Kufaulu na kutofaulu kwa mwandishi kifani na kimaudhui
Hapa tunaangalia ubora na udhaifu wa mwandishi kifani na kimaudhui katika kazi husika. Hapa vipengele vya fani na maudhui huzingatiwa kwa kina ili kuweza kupima umadhubuti wa kazi hiyo na hatimaye kuamua kwa haki kama mwandishi amefaulu au la
NB: Rejea vipengele vya fani na maudhui
Soma hadithi ifuatayo kisha ikifuatiwa na uhakiki wake
Sadiki Ukipenda
Kuna mengi – mengi yaliyonivutia kwa Mzee Siwa hata niikaungana naye. Kwanza, ukweli wake. Kwake, neno ni deni kubwa kuliko deni la fedha. Pili, ushujaa wake. Penye haki husimama kidete bila ya kututetereka wala kuwa na hofu ya mtu yeyote; mkubwa au mdogo. Tatu, imani yake, hasa kwangu – daima alikuwa tayari kugawa  mafungu chochote alichokuwa nacho, ijapokuwa ndicho hichohicho . Nne, uhodari na ukakamavu wake wa kazi. Shamba lake ndilo lililokuwa kubwa kuliko shamba la kijan ayeyote pale kijijini petu. Sikwambii wazee ambao daima walistahabu kukaa kwenye mabao mikahawani kupiga domo.
            “Katu,” alikataa Mzee Siwa sirisiri, “sitokokonea uchochole wa sina sina ‘ni, nikiulizwa siungami!”
            Miongoni mwa yote yale, nilihusudu kumsikia akisema. Ulimi wake daima ni nasaha. Kichwa chake ni maarifa. Shauri lake ni busara na mwongozo wake ni mwangaza katika maisha. Hasa kwa kijana kama mimi, ninayezikabili telezi za ulimwengu; ninayepapasa kama kipofu kwenye njia mbaya ya hatari katika kutafuta yale yanayoitwa maisha; njia ambayo vijana wengi huipita wakipambana na vikwazo vya choyo, wivu, jitimai na msiba kwa jumla. Hakika ubongo wa Mzee Siwa ukifanya kazi kwa njia ya ajabu. Hata wakati mwingine nilishindwa kuelewa aliwezaje kutambua siri nyingi na jinsi gani aliweza kupambanua vitendawili vigumu ilhali hata shule haijui
            Kwa kuwa binadamu asingalikosa ila, ila Mzee Siwa, kama ni ila, alijitenga makusudi na wazee wengine wa kijijini na hakuficha kuwaambia kwa nini. Kama alivyo, mtu wa  nipe n’kupe, alikuwa akisema kinywa kipana
            “Mimi na nyinyi tofauti. Mimi naishi leo na kesho, nyinyi mnaishi miaka mia moja nyuma. Vipi tutangamana?” Tabia yake hiyo ya kutoweza kuzizuia akichokozwa kweli chungu wenzake basi wamefarakana naye na kumpagaza jina la Mjuaji! Na wengine Mchawi!
            Lakini si mimi. Mimi namjua kuwa ni mzee anayethamini ut kwa hivyo, asingaliweza kuwa  mchawa. Na baada ya kutokea kadhia hiininayoieleza, ndiyo kabisa nimesadiki kuwa yeye si mchawi, na kwa kweli siku zote hizi yeye amekuwa dhidi ya uchawi Adhuhuri. Jua linaatilisha kila kitu kilichothubutu kupita kwenye uwazi wa dunia. Mbinu zimetakatika samawati, baada ya mawingu kukimbia ukali wa jua. Ila, muda hata muda, kipepo mwanana kilijitahidi kuzimua vuke la joto lililoning’inia angani. Ng’ombe walikuwa wamejilalia malishoni kw auzito na machofu, wakichakua mabaki ya matafuno vinywani mwao. Muda hata muda zilisikika ‘baa’ zao zikikata hewa. Kunguru tu ndio walikuwa wameshughulika kwenye wakati hu wa dhiki. Kunguru hachoki mpaka jua litue.
            Na mimi nilikuwa wa miongoni mwa kunguru. Mmbioni nilikuwa ingawa mbio zangu hazikuambulia kitu cha maana, ila kumeza hewa. Ninapokuwa katika udhia na kusaili mlolongo wa mambo na matukio yaliyotufumaniza sisi vijana na wazee bila ya kup[ata fasili yoyote, huishia kwenda kwa mzee Siwa. Nilihisi kila siku alikuwa na majibu ya masuala yangu ingawa wakati mwingine hayakuniridhisha kumpa siri zangu. Hata kuliko baba’angu!
            Leo kwake alikuwa hayupo. Nilijua alikuwa wapi lakini, niliteremka bondeni, kondeni kwake. Nikamkuta ameshamaliza kupalilia. Sasa akawaanakwangura jembe lililokuwa limegandia tope. Baadaye akalisuuza kwa maji yaliyopita kwenye kijito kilichotiririka mbele ya kibanda chake.
            Baada ya kwisha kumwamkia alinilaumu – “He, huonekani babu? Umeadimika kama wali wa daku? Nilikuwa nikikuwaza moyoni sasa hivi, nikawa n’nasema, mbona Mussa simwoni siku hizi?  Nikajiambia, kama leo hukuja nyumbani, basi nitajilazimisha kukufuata mimi. Nina jambo muhimu sana nataka kukukwambia.” Sauti lake lilelile la kawaida kavu, zito!
            “Salama lakini?” nilimwuliza kwa wasiwasi.
            “Salama kama si salama,” alinijibu kwa mkato.
            “He! Kuna nini tena?” moyo ulianza kunipapa. Nilitabaruki.
            Kilikuwa kizungumkuti. Mara salama kama si salama, na kasha salama tu usiogope …. Lakini ni kawaida yake mzee huyu. Mambo yake kinyumenyume! Yale yangu nilikwenda kwake yalivia kwanza.
            “N’ache nisali kwanza …..je, wewe umeshasali adhuhuri? Au tutasali pamoja?”
            ilinibidi kutoa dharura ya uongo, maana Mzee Siwa kila siku alinihimiza kutekeleza faradhi ya sala.”Nguo zangu hazina udhu. Nitasali nikifika nyumbani.”
            Nikamwacha akitawadha. Na mi’ nikavuta kumbi nikakaa kwa kuegemea nguzo ya kibanda. Nikamwangalia alivyoliwa akijitayarisha kumkabili Mungu wake huku moyo wangu ukinisimanga. Sijui kwa nini, lakini kutazama mzee huyu akijitia udhu kujitayarisha kusali, kulinijaza amani moyoni. Katika hali ya kawaida sijapata kuwa na amani yoyote moyoni mwangu! Kwa kweli wakati pekeemimi ninapopata nafuu na pumziko namna hii ni wakati kama huu wa kutawadha na kumkabili muumba wa vyote.
            Mzee Siwa alitia maji birikani, akanuilia kuvikosha viungo vya mwili wake vilivyofuradhiwa na vilivyosumiwa. Kasha akapachua msala. Nao ulikuwa wa kuti kumba lililosukwa mahsusi kwa kazi hiyo. Aaaa, alikuwa vyako mwenyewe, kunyanyua kuti la kumba , kasha kurukuu na kusujudu. Ah, ukifikiri haya, utaona vipi ilivyo vigumu kukutana na binadamu mwenzako. Ati uvae tai, suti, viatu vya njuti, au kama mwanamke ujipure na kujipondoa, na kujirashia mafuta mazuri …….. na papo mwanadamu atakupokea kwa jeuri!
            Alipokwisha kupiga rakaa zake nne na mbili za suna, alibaki palepale penye msala wake wa kuti la kumba, akawa amenigeukia mimi badala ya kutazama kibla. Kwa muda alinipuuza, akawa anamung’unya midomo akimaliza dua na myuradi.
            Hapo nikapata fursa ya kumwangalia kw akaribu. Ni mzee mwenye umri wa miaka sitini na tano hivi; lakini amewapiku walioko kwenye arobaini na tano: kakacha, kakamaa, mzima kama chuma! Damu ya siha bado inamwenda vizuri chini ya ngozi yake nyeusi kama jongoo. Macho yake makubwa na makali; na mpaka sasa anajivunia nayo kwmba anaweza kutunga uzi sindano anapotia viua kofia yake. Hakuhitajia miwani au msaada wa mwana wa yeyote! Au pale alipotaka kujitoa kepu (ambao siku hizi wamerejea tena katika janibu hii baada ya kupotea miaka thelathini iliyopita). Alipotoa chepu kamwe hakumvalia miwani, alichukua mwiba tu na kama mchezo, punje ya mtama ya chepu ilikuwa chini. Wazee wengi kama yeye ilibidi watolewe chepu na cijana hata kama walivaa miwani.
            Kichwani mvi zilihesabika. Pua yake, midomo yake, masikio na kidevu, vyote bado havijaporomoka; na mashavu hayajashobwekea ndani. Mikono yake bado ilimruhusu kukamata jembe mchana kutwa, na wala mgongo wake haukukataa kuinama na alipoinuka alikuwa kama hakuinama. Mwenyewe alipenda kujiboda,”Nyinyi vijana wa siku hizi mmeubwa kwa mchanga. Sisi kwa udongo wa wa kinamu – ‘fa mchezo dongo la kinamu!” Ukweli ni kwamba, kazi ya ubaharia aliyoifanya kwa muda mrefu wa maisha yake iliufanya mwili wake ushibe upepo wa pwani ulioilinda siha yake. Na zaidi, Mzee Siwa alipenda kujitunza tokea alipokuwa kijana. Ni hakika kwamba mpaka leo hajan’goa hata jino moja!
            Alinuka, akachukua kijaluba chake cha uraibu – kipande cha jani la uambuu, chengachenga za popoo, dole la chokaa akalirambisha juu yake, tumbaku kidogo, mvuato ukawa tayari. Aliukunja vyema uraibu wake, kasha akautumbukiza kinywani.
            Muda! Halafu: “N’ambie…” maneno yake yalitoka ndani ya sshata la uraibu. Macho yake yamenitunga sawasawa; “n’ambie,” aliemdelea, “kuwa m’talokwambia hapa leo, litakuwa baina ya mimi,” alijielekeza kidogo cha sahada, “na wewe….” Akanielekeza na mimi hichohicho kidole cha shahada.
            “Ha…hakuna si…si…siku n’liyotoa siri yako nje,” nilibabaika na kujibu. Mzee Siwa hajapata kutoniamini hata siku moja, leo kimezidi nini?
            Alitazama huku na huku mule mwenye machaka ya Mungu, kasha akaweka panda ya kidole chake cha shahada na kati kutema mate mekundu ya tambuu. Kasha alisogeza mwili wake karibu yangu na kunong’ona, “Mussa, Mussa babu ……unatakiwa!” Kauli hiyo sikuifahamu.
            “Natakiwa? ……Natakiwa na nani?” nilimwuliza.
            Mzee Siwa hakujibu kitu kwa muda. Akawa anaimung’unya midomo wile alivyokuwa akivuata uraibu. Kisaha akabatuka maneno bila ya kunitazama.
            “Baba’ako”, alionyesha wasiwasi kidogo; wasiwasi uliochanganyika na haya.
            “Baba’angu!” Nilishangaa “Ananitaka wapi? …..Na kama ananitaka mbona hajaniita kunieleza alilonalo?”
            Kwa hakikaneno unatakiwa lilikuwa na utata Fulani. Sikujua ni maana ipi mzee huyu aliyokuwa kakusudia. Mimio nilijibu nilivyolichukulia mwenyewe.
            “Ati!” alitema tena mate ya uraibu. “Sivyo kutakiwa hivyo unavyodhani wewe.”
            “Vipi basi?” niliuliza kwa mkato. Nimezidi kuemewa na moyo ukanijaa wahaka. Nilihisisiifahamu lugha ya kiswahili kamwe, ama labda ulimwengu umejaa miujiza.
            “Anataka akutoe kikoa!” Mzee Siwa alisema hivyo huku akijaribu kutazama tena kule machakani, haloafu kwa sauti ya chini aliendelea, “Baba ‘ako ni mchawi. Na sasa anadaiwa mwana. Na ye’ kawaambia wachawi wenzie yu tayari yeyote kati ya ndugu zako, ila si wewe. Lakini wenzake wamekataa. Wanataka sharti wewe, maana wewe ni msomi; na wasomi wana hatari! Kila siku wanatafuna na kuuma!”
            moyo ulinibakuka Mussa. Baba’andu! Baba’angu mchawi! Kumbe kweli wasemayo watu; ‘kikulacho kinguonimo.’ Lakini a-a bado siamini. Baba’angu si mchawi kwa mara ya mwanzo, sitaamini analosema Mzee Siwa.
            “Mengi umenambi Mzee Siwa na nimeyaamini, ila hili!”
            “Haaa,” alicheka kwa kicheko cha ghafla, “uchawi  upo, sadiki ukipenda,” aliendelea, “na tena usidharau hata jambo moja katika yale niliyokwambia au utapoteza maisha yako. Na kama unataka….”alinihakikishia,”mimi nitakuthibitishia ukweli wa maneno yangu …….” alisita hapo, akawa anaramba dari na sakafu ya kinywa chake kugandua masalio ya uraibu yaliyoganda. Muda ukapita. Kisha….
            “Kesho kutwwa,” aliendelea , “usiku wa manane, utakuja kutolewa. Mimi nitakupa kago la kujikinga usipatikane. Kago pia litakupa macho ya kuwafedhehi wachawi. Na hata kama utakuwa tayari kumdhuru baba’ako pia utaweza. Sema tu, unataka vipi? Naona hawa wachawi watatumalizia watoto na vijana. Tutakuja kuuguzwa na kuzikwa na nani?”
            sikuwa na la kusema ilikuwa uzito kuamini yote na kutenda pia. Lakini kudharau sikuweza, kwa vile ninavyomjua Mzee Siwa, si mtu wa kusema uongo. Bila ya shaka nilikuwa na masuala mengi ya kumwuliza, lakini nilihisi huo haukuwa wakati wake.
            “Ni tayari,” nilijibu bila ya kufikiri huku nimetokwa na hisia yoyote kwa baba’angu. Nilikuwa kama jiwe! Jambo moja lakini lilinitia moyo mpango wangu wa kutoka nje ulielekkea kufanikiwa. Nilikuja kwa mzeeSiwa kumwambia hayo kwa kweli, lakini yeye alinifumaniza na yake. Hata hivyo sasa nilimweleza na yeye akakubakiana na mimi kwamba hilo lilikuwa jambo la busara, maana wachawi hawatasita kujaribu tena na tena kuniondoa duniani.
            “Baba twen’zetu, niachie mimi nitayatengeneza yote,” alinihakikishia Mzeealitwaa shepeo lake, akalivaa. Akaweka jembe lake begani, akatia chupa ya maji ya kunywa kapuni mwake na kunikabidhi mimi. Tukatoka
Mzee Siwa alifanya wajibu  wake. Dawa ya mizizi Fulani alinipa kuchemsha na kunywa. Nyingine alinitaka niifukie kwenye kizingiti changu cha chumba. Pia akanipa hirizi kubwa kuifunga mkono wa kulia. Akaniongezea kago nyingine kadha ambazo nilizitekeleza. Sikupuuza agizo lake hata moja. Basi siku ilipofika, nililala kitandani kungojea matokeo. Nusu nina imani, nusu naona haiwezi kuwa. Kwa kweli nilijaa woga na sikuwa na roho. Saa ya msikitini ikagonga. Nikaihesabu milio minane. Moyo wangu ukagutuka. Ukapiga mishindo zaidi kuliko ile ya saa. Nikaanzaa kugwaya na kutetemeka. Damu ikaniruka. Baridi kali ikanijia sijui kutoka wapi, ikanigandama ingawa chumbani mlikuwa na joto! Nilijua leo ni leo, asemaye kesho mwongo. Kanibidi kupiga moyo konde na kusema, kufa au kupona.
Mara nikaona ukuta wangu wa chumba mkono wa kulia ukipasuka! Mbio, mbio, mbio nilitoka nje, nikakimbia chini ya mbuyu. Kazi ya kwanza niliyoagizwa na mzee Siwa imekwisha. Na’mi nikajihisi kama maiti niliyefufuka! Sikujiweza kwa jitimai na hofu. Naam, alikuwa baba’angu! Niliyakumbuka maneno ya mzee Siwa; “Usipite ukuta wa kulia utakaopasuliwa na baba’ko. Pasua ukuta wa kushoto kwa mundu. Na ‘mi nikafuata hivyo hicyo.
Muda si mrefu nilimwona baba’angu akitoka ndani ya chumba changu akimwongoza mtu aliyedhani alikuwa ni mimi. Kumbe lilikuwa chege la mgomba ambalo kwa mazingaombwe ya Mzee Siwa, limegeuzika mtu mwenye wasifu wangu. Wachawi wamekutana na mganguzi wa uchawi! Basi nikamwandama baba’angu na lile zuzu lake. Mimi niliweza kuwaona, lakini wao hawakuweza kuniona. Madawa yalikuwa yamenifunganimefungika. Hakukuwa na uchawi ulioweza kuniingia. Walikwenda kitambo kirefu. Hatimaye wakafika pahala penye uwanda ambapo watu wengi walikuwa wamekusanyika. Ilikuwa jumuia ya wachawi. Wotewalikuwa uchi kama walivyozaliwa. Hawana haya. Nilimeza funda moto na chungu la mate. Wale wachawi wenzake walipomwona baba’angu anaingilizana na ng’ombe au zuzu lake walipayukwa kwa furaha na shangwe, na hapohapo ugoma ukadudwa:
Chakatu chakatu, mahepe
Mtoto wa Kware, mlete!
Kware we Kware, mlete!
Kware alikuwa baba’angu ambaye alionyesha kuchanua upeo wa furaha katika shamrashamra hizo. Na ‘mi nikajongea karibu. Nikasadikisha umadhuburi wa kago la mzee Siwa. Hakuna aliyeniona, ila mimi niliwaona wote waliokuwepo. Wengine niliowajua hawakunishangaza , niliwahi kuwasikia watu wakiwataja kuwa wamo uchawini. Lakini wengine walinishangaza. Walikuwa watu wa desturi niliodhani walikuwa wapole, wacha Mungu na wasiopenda kumdhulumu mtu yeyote. Baba’angu akaingia ngomani akimchezesha mwari wake kwa nguvu. Ngoma ilikuwa ya kukobeana na kupeana uchawi – kike kwa kiume, mpata maptae. Nao ugoma uliendelea kwa muda mrefu. Harafu ukasita ghafla! Sauti ya sheha wetu wa kijiji, mzee Mfaki kombo, kinying’inya cha marehemu Bikirembwe, malkia wa wachawi, ilisikika ikpasua ukimya wa usiku wa manane. Ilikuwa sauti ya hotuba fupi kimafumbofumbo, iliyoeleza ya makusanyiko ule
            “Bwana Kware ameleta changi yake. Kupeana ni kikoa, toa na we’ upewe. Mla kuku w wenziwe, miguu humwelekea. Ametoa mwanawe msomi anayemwonea uchungu zaidi. Na wasomi wanatuletea nini ila balaa! Kware amethamini kilinge cha uchawini. Taireni wazee, musimwandame tena. Na tokea sasa, Mussa mwanawe ni ng’ombe wetu; tumchezeni, tumpigeni, tumchinjeni…”
            ugoma ukadudwa tena. Nyimbo ya safari hii ilikuwa:
                        Nasikia parakacha miembeni;
                        Kma mshambiginya mleteni!
            Huku wakicheza ugoma, walilipiga lile Mussa zuzu. Lo! Hatari kumbe kupigwa uchawini! Sijui ningekuwaje kama yule aliyekuwa akipigwa alikuwa mimi kweli. Nadhani dhoruba mbili tu zingetosha kunitupa chini, maiti mkavu! Magongo, marungu, mawe, mapanga, walilitwanga nalo zuzu. Furaha vicheko vifijo huku wakicheza kwa hesabu. Walioona Wasahili. Hatimaye sheba, sheba wa kijiji chetu na uchawi, alisitisha ugoma na hujuma
            “Basi tena, kesho ‘uyo. Kware, mrejeshe mwana. Kesho kutwa tutakuja mchukua kwa shangwe kubwa zaidi, kesho kutwa tukapokuja kukuekea chege uzike na sisi utupe mtoto tumle…”
            Ole wao! Wameondokea patupu leo kwa mara ya mwanzo. Hawana habari kuwa mara hii, udhalimu wao haukufua dafu. Mbinu walizotaka kutumia wao, tumeshazitumia sisi. Mzee Siwa kawacheza!
            Basi ikabaki kazi ya mwisho na ‘mi sikusita, niliitekeleza. Ilinijia sauti ya Mzee Siwa tena …..Atakapokuwa akilirejesha hilo change la zuzu walilolipiga mfuate baba’ko mundu wako. Ukifika mlangoni pako tu mpige dafran moja, moja tu usizidi…..ukizidisha! umekwisha ! nikamwandama. Usiku ulikuwa na kimya cha ajabu- isipokuwa mara mojamoja, budi alibutia kama vile akiwazomea wachawi kwa uhasidi wao. Shaari ilizuia hata miti kunong’ona na mazingira yote yalijaa kitisho. Ulikuwa usiku wa kuogofya! Na sasa nikahisi ubaridi wa alfajiri ukinyotoa maungoni na ndani ya nafsi yangu mkachimbuka hasira na chuki.sikuwaza kingine ila kisasi .hata kama yule niliye kuwa nikimfuata  kumdhuru  alikuwa baba’angu.baba aliyetaka kuitoa roho ya mwanawe.
            Alipofika mlangoni tu nilimrushia mundu wa kichwa. Mmoja tu!
Alipiga usiyahi mkali, lakini hakutoka damu! Kasha alinijia kwa kilio  cha huzuni na kuniambia,’unaona sijatoka damu,nipige tena nife,mimi sistahiki kuishi kwa  nilivyokutendea….’
            Niliyakumbuka maneno ya mzee siwa..,ukizidisha umekwisha!;sikumsikiliza;la kwa haraka za ajabu nilifunga mlango wa chumba changu na kupanda kitandani pangu.sikupata usingizi kamwe jimbi la saa kumi za alfajiri  liliwika.niliinuka nikatawadha na kusali.nikaomba mungu anihifadhi na kunizidishia maisha marefu. Kasha nilirudi kitandani na kujaribu kufumba macho. Ng’o; usingizi haukuja. Nafsi yangu nzima ilizongwa na mawazo matupu! Huendaje kufikia hivi dunia, mtu na mwanawe kuhujumiana? Ama kweli imani imekwisha. Hii ni aheri dunia!
            Asubuhi nilipoangalia chumba changu, nilikuta kuta zote nzima. Nje, lile chege la mgomba wachawi walilodhania ni Mussa, lilikuwa limelala mbele ya mlango – chege la mgomba si mtu tena! Nilikuwa nina hakika sasa kwamba baba’angu atalala hivyohivyo si muda mrefu. Na kweli, saa sita za mchana baba’angu aliiaga dunia, akaniachia maisha yangu aliyotaka ni mwachie yeye. Kila mtu alishangazwa na kifo chake, na kama kawaida kila mtu alisema vyake. Baaadhi walisema kapigwa na wachawi wenzake kwa kushindwa kunitoa mimi. Wengine walisema karogwa na ndugu zake waliomwekea kisasi kwa kuwaulia watoto wao. Hapana aliyejua sababu ya kifo chake ila mimi na Mzee Siwa na labda wachawi wenzake waliotushuku sisi.
            Na jkwa hayo msinilaumu. Nakwambieni roho tamu; na penye ukatili wa kulana roho, msiione ajabu mtu kutetea roho yake. Kisa mkasa! Zaidi ninafuraha kubwa. Hapo nilipo nimo melini nikisafiri kuona ulimwengu mwingine. Wangu umenishinda kwa muda. Ningependa kurudi pale nitakapokuwa mtu kamili nitakayekuwa huru mimi na roho yangu. Nitakapoweza kusema hii ni nchi aliyoniachia baba’angu aliyejaribu kuniua. Na si kuwa peke yangu niliyekuwa na mori huo – nilipoingia melini niligundua vijana wengi kama mimi wamo humo. Wengine hata hawajui wanaelekea wapi, lakini wanajua wanakotoka. Na wala hawajuti kwa nini wameondoka kwao, ingawa hawana uhakika na wanakokwenda. Sijui kutatokezea nini katika dunia hii? Na wengine walinihadithia kwamba wenzetu wengi wako nje wameshatangulia. Wengine wameshaukata wengine wanahangaika naq kubuga na njia. Heri ya hayo wanasema. Huzuni yangu kubwa ilikuwa tu kumwacha mtu kama Mzee Siwa – mtu adimu, au unasemaje? Lakini Mzee  Siwa anaweza kuyamudu maisha ya pahala popote; hata motoni! Aliniambia hivyo, na akataka n’ende na dunia yangu! Ati siku zake zimekwisha na zangu ndio kwanza zinaanza!
            Katika kazi ya fasihi inafananishwa na chombo cha chakula na maudhui kama chakula ndani ya chombo na msanii ndiye mpishi, chombo kikiwa kibovu au kichafu chakula nacho chaweza kuwa kibovu hivyo kushindwa kuliwa. Hivyo basi msanii analazimika kulia kikisha chombo na chakula vinakuwa safi. Hata hivyo tunaweza kufananisha fani na maudhui kama pande mbili za shilingi ambazo haziwezi kutenanishwa.
Katika hadithi hii ya “Sadiki Ukipenda” iliyoandikwa na Said A. Mohamed tutaenda kuangalia maudhui, fani na dhana zake pia tutaona nafsi ya hadithi hii katika fasihi ya kiswahili ya majaribio.
            Maudhui, haya ni jumla ya mawazo yote au ujumbe uliomo ndani ya haduthi hii au ndani ya kazi yoyote ya kifasihi.
“Ni jumla ya mambo yote yanayozungumziwa katika KAZI YA KIFASIHI”
Dhana hii inaundwa na dhamira, ujumbe falsafa, migogoro na itikadi.
`           Dhamira kuu katika hadithi hii ni ujenzi wa jamii mpya, jamii ambayo itakuwa safi bila kuwa na dhuluma, uvivu, na watenda maovu, bali iwe na viongozi waleta maendeleo, wazalendo, wenye mapenzi ya dhati kwa jamii yao na wachapa kazi.
Dhamira hii inaundwa na dhamira ndogondogo kama ifuatavyo
            Umuhimu na kufanya kazi, Msanii “Said A. Mohamed” ameweza kuonesha wanajamii hasa wazee na vijana wanavyoshindwa kufanya kazi bali kukaa mikahawani kucheza bao tu katika hadithi hii tunamuona mzee Siwa anavyowakilisha kundi la wachapakazi kama sifa yake ya nne inavyosema “…. Kutoa sifa zake…..na ukakamavu wake wa kazi. Shamba lake ndilo lililokuwa kubw akuliko shamba la kijana yeyote pale kijijjini petu”
            Pia tunamuona Musa kama kijana anayejishughulisha na suala la utafutajji na kundi lake na hata yeye mwenyewe alikuwa kijana msomi.
            Dhumuni na uonevu Mwandishi ameweza kuonesha kundi ambalo kazi yake ilikuwa ni kutenda maovu yaani kudhulumu na kuonea na hili lilikuwa tabaka la juu. Msanii anasema “………..lakini wengine walinishangza.Walikuwa watu wa desturi niliyodhani walikuwa wapole,wacha Mungu na wasiopenda kudhulumu mtu yeyote….’[uk.7]hivyo basi tunaona hata viongozi wa dini na wanaotegemewa katika jamii wanadhulumu ndugu zae wa karibu. Mfano., mzee Kware.
            Matabaka katika jamii. Msanii ameonesha matabaka mbalimbali kama vile wasomi na ambao hawakusoma, tabala tawala na walimu, wavuvi na wachapakazi, wema na watenda maovu,
Tabaka la wasomi linawakilishwa na Mussa na tabaka la ambao hawakusoma linawakilishwa na wachawi. Tabaka tawala linawakilishwa na wachawi. Mfano, mzee Kware na kundi lake. Tabaka la wachapakazi linawakilishwa na mzee Sira na wavivu wanawakilishwa na watendamaovu ambapo mzee Siwa anawakilisha tabaka la wema na hasa wacha Mungu.
            Ujasiri na kujitoa mhanga, msanii ameweza kwa kiasi kikubwa kulifichua kundi la wajasiri na umuhimu wakewake. Hii inadhihirishwa pale alipomuonesha mzee Sira kama jasiri wa kusema lukweli na kujitoa mhanga ili kufichua maovu katika jamii mfano, msanii anasema
            “…mimi ni mtu wa nipe nikupe…”(uk 1) akiwa na maana ya kwamba ukisema naye anasema/ atasema
            Pia mzee Siwa anaonekana jasiri pale ambapo alifichua siri ya watenda maovu kwa Musa kw kumuambia wazi kuwa babaye ni mchawi. Kwa upande mwingine Musa anaonesha ujasiri na kujitoa mhanga kwa kupambana na watenda maovu hadi kuwashinda.
            Usaliti, Msanii anaonesha usaliti katika jamii usaliti huu uko katika makundi mawili, usaliti mzuri na susaliti mbaya. Usaliti wa mzee Siwa kufichua siri ya wachawi kwa Musa huu ni usaliti mzuri. Usaliti wa mzee Kware na wachawi wenzake kutaka kuwazulu ndugu zao wa karibu ni usaliti mbaya katika jamii yoyote. Mfano , mzee Mfaki Kombo kusaliti wananchi aliowaongoza pia ni usaliti mbaya.
            Suala la uzalendo, Mwandishi pia amefichua suala la uzalendo pale alipomuonesha mzee Siwa akilitumika Taifa lake hata baada ya kuwa amestafu pia kitendo cha kufichua siri ya uchawi bila uoga ni uzalendo wa pekee. Kwa upande mwingine msanii amemuonesha Musa akipambana na Wachawi (watenda maovu)kitendo hiki ni cha uzalendo wa pekee katika jamii.
            Suala la mapenzi, Msanii ameweza kuyonesha mapenzi ya aina mbili, mapenzi ya dhati na mapenzi ya uongo. Mzee Siwa amechorwa kuwa na mapenzi ya dhati kwa Musa pamoja na jamii yake kwa ujumla, mfano kitendo cha kumpatia Musa kago ili aipukane na maovu ni kitendo cha mapenzi ya kweli.
Pia Musa anaonesha mapenzi ya kweli kwa mzeeSiwa kw akumtembelea mara kwa mara. Msanii anasema  “….Na sasa hivi nilikuwa njiani kuelekea kwake mtu pekee niliyeweza kumpa siri zangu…” (uk 2) mapenzi ya uongo yameonekana yamejitokeza kwa mzee Kware na wachawi wenzake kutaka kuua Musa ndugu yao wa karibu
            Umuhimu wa elimu, Mhusika Musa aliweza kuleta mapinduzi kwa kupkea ushauri toka kwa mzee Siwa hii hi kwa sababu alikuwa na Msomi katika jamii. Lakini wale wazee kijijini hawakueza maendeleo kwa sababu ya kukosa elimu.
            UJUMBE; “Hii ni DHANA inayotumiwa kuelezea taarifa ambazo MSANII au MTUNZI hutoa kwa wasomaji ametoa ujumbe, kwamba, kikulacho kinguonmo, Mle kuku wa wenzio miguu humuelekea.
            MIGOGORO; “Hii ni istilahi inayotumiwa kurejerea mvutano unaokuwako kati ya mhusika mmoja na mwingine katika kazi ya kifasihi”, katika hadithi kundi na kundi katika jamii.
Kwanza tunaona mgogoro kati …ya mzee Kware na wenzake Msomi na si mwingine yeyote. Pili msanii ameonesha mgogoro kati ya kundi la wasomi na wasio wasomi hii  ni pale hawa wanaoneshwa na Musa kama msomi na kundi la wachawi ambao sio wasomi akiwemo babayake. Tatu mzee Siwa na mzee  wenzake kijijini pale ambapo mzee Siwa alipoweza kukataa mambo yao.
            FALSAFA; “Istilahi hii hutumiwa kuelezea wazo au mawazo anayoamini mtu au mwandishi kuwa mwandishi9 anaamini kuwa, mapinduzi ndio njia pekee ya kujikombo toka kwenye mikono ya wadhilumaji.vilevile msanii anaamini kuwa elimu ni siraha ya kuleta mabadiliko maendeleo katika jamii
 
1.  Wamitila K.W(2003)KAMUSI YA FASIHI / ISTILAHI
 NA NADHARIA, Nairobi Kenya uk 282
2.  T.H.J ………………ukk 121  
 3. T.H.J ………………uk 41
Fani; Huu ni ufundi katika kazi ya fasihi masnii hutumia katika kuomba kazi yake.
“Ni ule ufundi wa kisanaa anautumia msanii katika kazi yake”1 Msanii ameweza kutumia sana fani katika vipengele vifuatavyo.
MUUNDO; “Ni mpango na mtiririko wa kazi kwa mpango wa visa na matukio”2 katika hadithi hii ya “Sadiki Ukipenda” msanii ametumia muundo wa moja kwa moja au msago kwani tunaona mtiririko wa matukio unafuatana kuanzia mwanzo hadi mwisho. Hii ni pale Musa anapoanza kwa kusimulia sifa za mzee Siwa, kifo cha baba yake na mwisho tunaona anahama nchi. 
Mtindo; “Ni ile mnamna ambayo msanii hutunga kazi hiyo na kuipa sura ambayo kifani na kimaudhui huainisha kanuni kawaida zilizofuatwa kama zilizopo (za kimapokeo) au ni za kipekee”3
Mwandishi katika hadithi hii ametumia mtindo wa monolojia (masimulizi ya mtu mmoja) pia ametumia nafsi zote tatu mfano. Mimi nafsi ya kwanza umoja uk 4, wewe nafsi ya kwanza wingi uk 5
LUGHA; “Lugha ndiyo nyenzo kuu katika kazi ya fasihi. Dhamira na maudhui hayawezi kuwafikia au kuwasilishwa bila ya kuweko kwa lugha “4 katika hadithi hii ya “Sadiki ukipenda” msanii ameweza kutu lugha ya kisanii iliyosheheni methali misemo, nahau tamathali za usemi na hata mbinu nyingine yote haya katika kufikisha ujumbe uliokusudiwa kwa hadhira iliyokusudiwa.
1. SENKORO F.E.M.K(1980), fasihi,FASIHI, PRESS AND PUBLICITY                                       CENTRE, DAR ES SALAAM uk 8
2.   T.H.J ……uk 26
            3.   T.H.J ……uk 26
            4  Wamitila K.W(2002),KICHOCHEO CHA FASIHI SIMULIZI NA ANDISHI
                             chuo cha Elimu na masomo ya mbali, Nairobi uk 193.
Matumizi ya methali; methali zifuatazo ndani ya hadithi hii
(i)  mla kuku wa wengi ,mguu humwelekea uk7
(ii)  Wakulacho wnguonimo
            Misemo
(i) Leo ni leo asemaye kesho ni mwongo ……uk6
(ii)Mtu wa nipe nikupe ……………………….uk 1
(iii)Kupiga  kupiga moyo konde ……. uk 6
            Tamathali za usemi; “Ni maneno, sentensi ambazo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo hata sauti katika maandishi au kusema kuleta maana au kubadili kulingana na kusudi la mtunzi”1
katika hadithi hii tamathaliza semi zilizotumika ni kama ifuatavyo;
            Takriri neno
(i)  Babangu babangu …………..uk 5
(ii)  Kuna mengi mengi ………..uk 1
(iii)  Natakiwa nitakiwa na nani…..4
Takriri nusu mstari
(i)  Mtoto wa kware mlete! Kware we mlete   …..6
            Sitiari
(i)  Kwake neno ni deni …………1
(ii)  Kichwa chake ni maarifa ……...uk 1
(iii)  Mwanawe ni ng’ombe wetu …..uk 7
(iv)  Ulimi wake ni nasaha ……..1
 
1: Kahigi K.K na Mulokozi M.M. (1979) KUNGA ZA
USHAIRI NA DIWANI YETU, T.P.H. dar es salaamu uk 132.
            Matumizi ya Tabaini
            (i)  Mtu wa nipe nikupe ……….uk 1
            (ii)  Salama kama si salama …….uk 2
            (iii)niliwaza na kuazua ……..uk 5     
Matumizi ya Tashibiha
            (i) Umeadimika  kama wali wa daku ..uk2
(ii)  Mzima kama chuma …….uk3.
            (iii)  Mweusi kama jongoo…
Matumizi ya Tashihisi
            (i)  Miti ilinong’ona………uk 9
            (ii) Mbingu zilitakatika baada ya mawingu kukimbia ukali wa jua …..uk2
           
Mjalizo
            Ati avae tai, suti, viatu vya njugu au kama mwanamke ajipare na kujipodoa na kujishia mafuta mazuri. Uk
Mdokezo.
            (i)  Ha…. hakuna si ….si …siku niliyotoa siri nje uk 4
            (ii)  Shahada na wewe ……….? Uk 4
Sitiari
            (i) Kwake naona ni deni ……….uk4 
(ii)  Kichwa chake ni maarifa
            (iii)  Ulimi wake ni nasaha
            (iv)  Kupeana ni kuokoa
            Nidaa
             He! Kuna nini tena?
            Matumizi ya Tafaida
(i)     Baba angu aliaga  dunia …uk 9
Lugha ya picha. Msanii ametumia lugha ya picha (taswira) “Hii ni dhana ambayo hutumiwa kuelezea neon, kirai au maelezo ambayo yaaunda picha Fulani katika akili msomaji”1 . Msanii ametumia tawsira zifuatazo.
Uchawi – akimaanisha matatizo katika jamii
            Ngoma – Taratibu au sheria
            Meli – mzunguko wa maisha
            Ng’ombe – wanyonyaji / Tabuka taswila
Kunguru – watu wasio na maisha mazuri
Hirizi – mawazo ya kimapinduzi
Kago – mbinu / wazo zuri elimu
Mandhari, “Hutumika kuelezea sehemu Fulani ambako lendo linatendeka au mazingira ya kisaikolojia ya tendo Fulani”2 Hadithi hii ya “Sadiki Ukipenda” msanii ametumia mazingira ambayo yametenda kuanzia kijijini wanakotumia jembe la mkono hadi mjini katika nchi za ulimwengu wa tatu hata dunia kote.
            Jina la hadithi; “Sadiki Ukipenda” linasadifu kwa kiasi kikubwa yale yaliyomo ndani ya hadithi hii kwani tunaona mzee Siwa anamtaarifu Mussa kuwa baba yake ni mtendamaovu (mchawi) na Mussa anashindwa kuandiki na hivyo Mzee Siwa anamwambia sadiki ukipenda.
            Kufaulu na kutofaulu kwa mwandishi amefaulu kwa kiasi kikubwa sana, na ndio maana ameweza kuibua dhamira mbalimbali mfano dhuluma iliyotanda katika jamii na suala la kutofanya kazi pamoja matabaka kwa ujumla. Na ametoa suluhisho ya kwamba ili kuleta maendeleo katika jamii lazima matatizo yaondolewe
            Kufaulu kifani. Kifani msanii ameweza kufaulu sana kwani ametunia lugha nzuri iliyosheheni usanii matumizi ya methali, misemo, nahau na tamathali za uemi na nsuko mzima wa matukio.
            Wahusika katika hadithi hii msanii ametumia wahusika wa kutosha. Msanii amemtumia Mussa kama mhusika mkuu na wengine.
           
Mussa mhusika mkuu
·         Kijana
·         Msomi
·         Anasikiliza ushauri
·         Alisimulia hadithi
·         Jasiri na mwanamapinduzi
Mzee Siwa, mzee wa miaka 65
·         Mchapakazi na mkakamavu
·         Mkweli
·         Shujaa
·         Mzalendo
·         Anaipenda nchi yake
·         Aliwahi kufanya kazi ya ubaharia
·         Mweusi kama jogoo
Mzee Kware, Baba yake Mussa.
·         Mchawi (mtendamaovu)
·         Alisaliti mwanae
·         Hana upendo kwa nchi yake
Mfaki Kombo, sheha, kiongozi
·         Tabaka la juu
·         Kiongozi wa watenda maovu
·         Kinying’inya cha Bi-kirembwe
Wachawi wengine (watenda maovu/ wadhulumaji)
·         Hawana upendo kwa nchi yao
·         Tabaka tawala
·         Hawana elimu
Nafasi ya hadithi hii ya “Sadiki Ukipenda” katika fasihi ya majaribio. Fasihi ya majaribio ni fasihi ambayo imeandikwa kwa mara ya kwanza na kukiuka faida au mazoea yaliyozoeleka katika jamii. Mfano, matumizi ya taswira ndani ya taswira, vipengele vya fasihi simulizi katika fasihi andishi, matumizi ya tashititi.
            Hakika hadithi ya “Sadiki Ukipenda ni fasihi ya kiswahili ya majaribio kwa sifa zake yenyewe. Kwanza hadithi hii imejaa udhanishi kwa kiasi kikubwa kuelezea mambo ambayo hayawezi kuonekana katika ulimwengu wa macho mfano ukuta kubomoka ili Mussa aweze kupita yaani uhalisia mazingaombwe.
            Pili matumizi ya majina ya wahusika ambao wameisha tumika katika hadithi au kazi zingine za fasihi zilizopita mfano Bibi Kirembwe ni sifa tosha ya kuifanya hadithi hii kuwa fasihi ya majaribio.
            Tatu matumizi ya picha na nyimbo ndaini ya hadithi ni kuifanya hadithi hii kuwa fasihi ya majaribio. Mwisho jicho la uhakiki linaihakiki kazi hii kama fasihi ya majaribio ya kiswahili.
UHAKIKI WA SADIKI UKIPENDA
Sadiki ukipenda ni hadithi fupi iliyoandikwa na said .A. Mohamed , kwa kutumia hadithi hii tutaangalia vipengele vya Fani, maudhui
Pia tutaangalia kufaulu na  kutofaulu kwa mwandishi hii itatupa nafasi ya kutoa maoni kuhusu vipengele hivyo vya fani na maudhui.
Kwanza tutaanza kuangalia maana ya Hadithi fupi, maana ya Fani na maudhui.
Hadithi fupi ni nini? Kwa mujibu wa Mbatiali swali hili huishia kujibiwa kwa kueleza ni nini ambacho si hadithi fupi kwa ujumla hadithi fupi ni moja tanzu za Riwaya.
Fani kwa mujibu wa kamusi ya Fasihi, istalahi na Nadharia ya k.w. wamitila anasema:
                        “Dhana hii hutumiwa kuelezea
muuundo au mpangilio wa kazi
ya kifasihi au hata sehemu zake”
senkoro f.e.m.k anasema
“Fani katika fasihi ni ule
ufundi wa kisanii anaotumia
msanii katika kazi yake”
kwa ujumla Fani ni ujuzi atumiao msanii katika kufikisha ujumbe kwa hadhira yake fani kuna vipengele vifuatavyo; muundo, mtindo, matumizi ya lugha mandhari na wahusika.
Maudhui katika kamusi ya fasihi , istilahi na Nadharia iliyoandikwa na wamitila anatoa maana ya maudhui ya kama ifuatayo:
“Ni jumla ya mambo  yote yanayozungumzia
katika kazi ya kifasihi”
maudhui hutumiwa kwa upana kujumlisha dhamira ujumbe, falsafa, msimamo na migogoro.
Kwa kutumia hadithi fupi ya sadiki ukipenda tunaanza kuangalia vipengele vya fani na maudhui
Tukianza na fani, tunaangalia muundo , mwandishi ametumia muundo wa moja kwa moja, ambapo mwandishi anakisimulia kisa kwa kumuelezea mzee Siwa, kasha uhusiano wake na Mussa. Pia anaelezea alivyomsaidia Mussa katika kuepukana na kifo chake mwishoo anaonesha mafanikio waliyo yapata kwa kuua mzee Kware. Kisa kimetungwa kwa mtiririko wa matukio kufuatana.
Mtindo; hapa tunaangalia upangaji wa fani na maudhui wa msanii ambapo unapelekea kutofautiana na wasanii wengine mwandishi wa sadiki ukipenda ametumia nafsi zote tatu katika kazi yake.             
Mfano:- ameonesha “mimi” nafsi ya kwanza umoja …nafsi ya kwanza wingi “sisi” nafsi ya pili umoja “wewe” nafsi ya pili wingi “nyinyi”
Mtindo ambao ametumia katika lugha umemfanya mwandishi kuonesha upekee katika kazi yake ametumia lahaja ambayo hajazoeleka kwa watumiaji wengi wa lugha ya kiswahili hivyo kufanya lugha ionekane ngumu. Pia majibizano na masimuzi yametumika katika hadithi hii vile vile mwandishi ametumia nyimbo katika … mwandishi ametumia uchawi katika kazi yake hicyo kuonesha utofauti na kazi nyingine kwani sikazi zote hutumia mbinu hii.
Matumizi ya lugha .mwandishi wa hadithi hii ametumia lugha ya kisanii iliyosheni Taamathali za semi , methali, nahau, mafumbo, lugha ya picha yote haya na katika kufikisha ujumbe kwa hadhira.
Tamathali za semi
Sitiari?
-kwake neon ni deni
-kichwa chake ni maarifa
-ulimi wake daima ni nasaha
-mwongozo wake ni mwangaza wa maisha
-mwanawe ni ngo’mbe wetu
takriri
Takriri konsonanti
Hii imetokea katika …………wimbo
“…..mtoto wa kware, mlete!
Kware we kware, mlete!
Tashibiha
-ninayo papasa kama kipofu
-umeadimika kama wali wa daku?
-…mzima kama chuma
-….ngozi yake nyeusi kama jongoo
-…bundu alihutia kama vile anawazomea wachawi
tabaini
-mtu wa nipe n’kupe
-salama kama si salama
-niliwaza na kuwazua
Tashihisi
-baada ya mawingu kukimbia
-maisha yake yaliufanya mwili wake ushibe upepo
-shuari ilizuia hata miti kunong’ona
Tanakali sauti
-Muda baada ya muda zilisikika “baa”zao
-“haa” alicheka
- parakacha miembeni
Tafsida
- kuaga dunia
-unatakiwa
Mbinu nyingine za kisanii
Mdokezo
- Niambie……….
- na wewe………
- Ha.. hakuna ... si … si
- Na  kama unataka ….
Mjalizo
Magogo, marungu,mawe,mapanga waliitwanga naku zuzu,furaha, vicheko, vifijo huku wakicheza kwa wimbo mtamu.
 Methali
- kikulacho kinguonimo
Nahau
- kupiga moyoa konde
Misemo
- sitakokonea uchochole wa sina sina hi nikiulizwa siungami,
- nipe n’kupe
- mla kuku wa mwenziwe miguu humwelekea
Lugha ya picha (Taswira)
- Mwandishi ameonesha taswira kwa kuonesha jinsi zuzu likopigwa
- pia ameonesha taweira katika              , Jinsi ukuta wa chumba cha Mussa ulivyo kuwa ukipasuka.
Sitiari
 Mwandishi ametumia sitiari ya uchawi na wachawi katika kufikisha ujumbe wake. Mwandishi ametumiwa wachawi katika kuonesha tabaka tawala. Mfano wa wachawi ambao ndio tabaka  tawala Mzee faki kombo na Mzee kware ambao wanawakilisha tabaka tawala.
         Ishara mbalimbali zimetumika katika kufisha ujumbe.
Kunguru
mwandishi ametumia kuguru ili kuonesha watu wenye maisha ya kubahatisha  na wsiokuwa na mwelekeo.
Ng’ombe,
Pia mwandishi ametumia ng’ombe ili ionesha tawala la watu wanyonyaji (winye nacho) wamiridhika na maisha tofauti na kunguru.
Ngoma ya wachawi,
Mwandishi ametumia mdundo wa ngoma ili kuonesha wachawi (tabaka tawala) kuwa lina taratibu na sheria ambazo zinatakiwa zifuatwe na wao.
Zuzu/Ngoma,
Mwandishi ameonesha jinsi ambavyo wachawi (tabaka tawala) linavyopewa mzugo  kupumbazwa na mbinu za wanamapinduzi.(Mzee siwa na Mussa).
Dawa na Hirizi.
         Ambazo alipewa Mussa ni mawazo aliyopewa na Mzee siwa. Ili aweze kuwashinda wachawi (tabaka tawala).
Meli.
Mwandishi ametumia meli ili kuonesha kwamba maisha ni mzunguko na wote tupo safarini wengi hatujui tuendako.
Mandhari.
Mwandishli ametumia mandhari ya nchi za dunia ya tatu ambazo maendeleo yake ni duni na zinakabiliwa na umaskini na watu kukosa elimu. Mwandishi ametumia madhari ya kijiji ambapo wakulima hutumia jambe la mkono.
Wahusika.
Mwandishi amegawa wahusika wake katika sehemu tatu mhusika mkuu, wahusika waasaudizi na wahusika wajenzi.
Mussa
- msomi aliyechukiwa na wachawi
- mwanamapinduzi , alifanikewa kupambana na wachawi
- jasiri , aliweza kumuua baba yake (mchawi) mpiga maendeleo
- mdadisi, aliweza kungundua mbinu za wachawi kw kusaidiwa na mzee siwa (alifuata nyendo zao).
1.  Wahusika wasaidizi.
   Mzee siwa sirisiri 
      - mzee mwenye miaka 65
      - mwanamapinduzi
      - mchapa kazi
      - anathamini utu kuliko pesa anapinga mchawi na anapenda maendeleo
2.   Mzee kware.
       - baba yake mussa
       - mchawi ( tabaka tawala)
       - mtu asiyependa kaendeleo ya jamii.
3.   Mhusika mjenzi (FAKI KOMBO)
        - mchawi ( mtawala)
        - kinyinginya  cha marehemu Bi kirembwe
        - anawapinga wasomi.
Maudhui.
Dhamira.
Dhamira kuu – UJENZI WA JAMII MPYA.
Ujenzi wa jamii mpya ni dhamira ambayo mwandishi ameitumia kama dhamira kuu ili kuonesha jinsi mabadiliko yanavyotokea katika jamii kwa kuyashinda maovu.
Dhamira ndogo ndogo
1.       Ushirikina na uchawi,
        Mwandishi ameonesha imani za ushirikina na uchawi kama ni moja ya vikwazo vya maendeleo katika jamii. Amewatumia wahusika wawili Mzee siwa na Mzee faki kombo pia Mzee kware ambaye alikuwa Tatari kumuua motto wake, ambayealikuwa ni msomi, kwani waliamini si kweli . lakini mwandishi ameonesha jinsi wachawi walivyoshindwa na kufanya haraka za ujenzi wa jamii zizidi kupata mafanikio.
2. Umuhimu wa Elimu
           Mwandishi ameonesha kuna ukosefu wa elimu wa aina mbili katika kadithi yake. Kwanza ukosefu wa elimu ya darasani ambayo hata mzee siwa ameikosa na wapo watu wengi ambao wameikosa . Pili mwandishiameonesha ukosefu wa elimu ya kujitambua, kama  vile unyonyaji unaoendelea katika jamii wapo watu wengi walikuwa hawaelewi hata Mussa mwenyewe alikuwa haelewi paka alivyopewa Elimu ( Hilizi na Madawa) ndo akagundua. Hivyo elimu ni kitu muhimu katika jamii ili kuleta maendeleo na kuondoa viongozi wasiofaa.
3. Umuhimu wa kufanya kazi
            Mwndishi ameonesha tatizo lililopo katika jamii yetu kwamba wapo watu wavivu ambao muda mwingi wanautumia katika kufanya mambo yasiyo ya muhimu kama kucheza bao.
             Vile vile mwandishi ameonesha jinsi mzee siwa anayo jishughulisha na ukilima .  yote ni katika kuleta mabadiliko katika jamii.
Umuhimu wa kuthamini utu
             Mwandishi ameonesha katika hadithi yake kuwa katika jamii kuna umuhimu wa kuthamini utu wa mtu , kwani utu ni  bora kuliko pesa     -mwandishi amemtumia mhusika Mzee siwa , jinsi anavyothamini utu, kitu ambacho kilinjengea maadui hasa kwa wale wasiopenda maendeleo ya jamii . Tabia   hii yam zee siwa ndio iliyo fanya  mussa amukani hiyo kuwaza kushirikiana katika kufanya mabadiliko katka jamii(kumuua moja ya wachawi)
Ujumbe
1. Uvivu ;ni adui wa maendeleo
2. Kikulacho ki nguoni mwako
3. Pesa si msingi wa utu
4. Uchawi ni kikwazo cha maendeleo
5. kuleta maendeleo (mabadiliko ) katika jamii ni jambo (kitu) ambacho ni          muhiumu ambapo mtu lazima ujitoe mhanga .
Falsafa.
  Msandishi anaamini uchawi ni kiwazo  cha maendeleo katika jamii , Hivyo wachawi lazima wauwawe.
Msimamo
   Mwandishi anamsimamo wa kimapinduzi , kwani anataka mabadiliko katika jamii kwa kuwaondoa viongozi ( Tabaka tawala) wenye kujali maslahi binafsi.
Migogoro
Mgogoro kati ya wasomi na wasiosoma (Tabaka tawala)
Mwandishi ameonesha kuwa katika jamii hiyo kuna watu ambao wamesoma na wapo wasiosoma . Ambapo wasomi wanachukiwa na wale wasiosoma .
        Mgogoro huu pia unahusisha wachawi (tabaka tawala) na wasomi (walio tabaka tawala) wachawi wnahofia kwamba wasomi wataibusha hisia kwa jamii na kuonesha maovu yafanywayo na tabaka tawala  Mzee faki kombo anasema:
“ Na wasomi wanatuletea  nini ila balaa!
Mussa na nafsi yake
        Mgogoro huu unaoneshwa  na mwandishi anavyo muonesha Mussa asivyoamini yale aliyoambiwa na Mzee Siwa kwamba baba yake ni mchawi .
Suluhisho  la kisa hiki, mwandishi ameonesha suluhisho kwa kuonesha ushindi uiopatikana kwa wanmapinduzi wakiongozwa na mzee siwa pamoja Mussa .
Kwani kifo cha Mzee kware badala kya Mussa kinaonesha ushindi mkubwa .Kwani mwisho mwandishi  Mussa akiingia melini, hiyo inonesha Mussa anaendelea na maisha kwani maisha ni mzunguko .
            Kwa kuhitimisha mwandishi amefaulu kufika ujumbe kwa kutumia kipengele cha maudhui pia amefaulu kutumia njia ( Fani) yenye ubunifu na utofauti katika kufikisha ujumbe. Mafanikio makubwa yameonekana zaidi kwa kutumia fasihi ya majaribio ya Kiswahili.
            Pia mwandishi amefulu  kw kufuata vigezo vya uandishi wa hadithi fupi. Mambo ambayo mwandishi ameyafuata ni pamoja na uasili umoja , ubunifu na mbano, ubora wa mtindo, tendo dhahiri pia umbo au kiini wazi.
  
CHATI (Chemsha Bongo)
Jaza Jedwali lifuatalo
2
3
4
1
7
8
9
10
6
13
5
11
12
Kwenda Chini
1.  Kufanikiwa kwa sherehe
2. Wazo au mawazo yanayojadiliwa
    Katika kazi ya fasihi
3. Mpangilio wa kazi ya kifasihi
4. Eneo au mazingira ambamo kazi ya
    Fasihi inafanyika.
5. Kifaa cha kuonesha muda
6. Kubali kuwa jambo Fulani ni hakika.
Kwenda Kulia
 1.  Ufundi au ujuzi wa kuwasilisha
      Mawazo kisanaa.
 7.  Hiki, kile
 8.  Mzaha
 9.  Kinyume cha nje
10. Tamko kuwa utaeleza jambo Fulani
 6 .  Kuketi
 5.   Jambo lisilo la uwazi
11. Hamu ya kufanya kitu , jambo
12. Vazi livaliwalo shingoni
13. Kinyume cha ndio 
Powered by Blogger.