NADHARIYA YA TAMTHIYA NA DRAMA

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
1.0 Utangulizi 
Tamthiliya ni utanzu mmoja kati ya tanzu tatu kuu za fasihi yaani Riwaya, Tamthiliya na Ushairi. Tamthiliya hutegemea mazungumzo na uigizaji ili kuwasilisha ujumbe wake. Katika moduli hii, dhana za Sanaa za Maonyesho, Drama na Tamthiliya zitafasiriwa, tutaainisha tamthiliya katika makundi mbalimbali na hatimaye kueleza nafasi ya tamthiliya katika jamii.

 1.1 Dhana za Sanaa za Maonyesho,

 Drama na Tamthiya Sanaa za Maonyesho Sanaa za maonyesho, kwa mujibu wa Mlama (1983), ni sanaa ambayo huwasilisha, ana kwa ana, tukio fulani kwa hadhira kwa kutumia usanii wa kiutendaji. Sanaa za maonyesho huliweka wazo katika hali ambapo tukio hilo linaweza kutendeka kwa kutumia usanii wa utendaji kama vile vitendo, uchezaji ngoma, n.k.

 Drama 

Drama ni taaluma inayohusu uigizaji wa hali fulani iwe ni vitendo, tabia au hisia za binadamu kwa kufuata taratibu maalumu. Drama ni aina mojawapo ya sanaa za maonyesho ambayo usanii wa kiutendaji wake hutegemea zaidi vitendo na uongeaji, tofauti na aina nyingine kama vile ngoma ambazo hutegemea zaidi uchezaji ngoma na upigaji muziki. Drama ni sanaa ya maonyesho yenye asili ya nchi za Ulaya. 

Tamthiliya 

Neno ‘tamthiliya’ linatokana na kitenzi ‘mithilisha’kwa maana ya kufananisha au kulinganisha. Katika Kiswahili, tamthiliya linatumika kwa maana ya ‘michezo ya kuigiza’. Katika tamthiliya huwa kuna ufananishaji ambapo mwigizaji hujifananisha na mhusika wa mchezo wakati wa kuigiza. Tamthiliya huwasilisha mambo kimaigizo kwa kutoa picha ya mambo ambayo yametokea hivyo au yanaaminika yangeweza kutokea hivyo. Tamthiliya husawiri hali mbalimbali katika maisha ya jamii na ndiposa ikaitwa tamthiliya kwa kule kujaribu kufananisha mazungumzo na maigizo hayo kifasihi na hali halisi katika jamii husika. Mazrui na Syambo (1992) wanaieleza tamthiliya kuwa ni utungo wa fasihi ambao umebuniwa, kwa kiasi kikubwa, kwa lugha ya  Asili ya kitenzi hiki ni Kiarabu.
mazungumzo yenye kuzua na kuendeleza matukio ya hadithi ya utungo huo. 
Lugha ya mazungumzo baina ya wahusika ni alama kubwa ya tamthiliya. Chanzo cha matukio ya hadithi ya tamthiliya fulani mara nyingi hupatikana mumo humo katika mazungumzo ya wahusika wake. TUKI (2004) nao wanafasili tamthiliya kuwa ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo. Kutokana na maelezo haya, tunaweza kusema kwamba tamthiliya ni aina mojawapo ya sanaa za maonyesho ambayo usanii wa utendaji wake hutegemea zaidi vitendo na uongeji, tofauti na aina nyingine kama vile ngoma ambazo hutegemea zaidi uchezaji ngoma na upigaji mziki. Tamthiliya ni ule utungo ambao unaweza kuwa umeandikwa au haukuandikwa unaoliweka wazo linalowasilishwa katika umbo la tukio la kuliwezesha kutendeka mbele ya hadhira (Mulama, P. 1983: 206). 
Kigezo kikuu cha tamthiliya ni kuweza kuwasilishwa jukwaani na kutazamwa na hadhira. Tamthiliya huwa na sifa za kawaida za maonyesho (Muhando na Balisidya, 1976; Muhando, 1983 na Mulokozi, 1996). Kila tamthiliya ina sifa za kipekee kulingana na maudhui yake na jinsi maudhui hayo yalivyowasilishwa (fani). 
Hata hivyo, tamthiliya nyingi zina sifa zifuatazo: 
i) Utoshelevu Kimuundo. Tamthiliya nzuri huwa na sehemu tatu muhimu: Mwanzo, Katikati na               Mwisho. Sehemu zake zinatazamiwa kuingiliana, kujengana na kukamilishana. 
ii) Tamthiliya huwa na lengo. Katika zama za Aristotle, kwa mfano, tanzia ziliwajibika kuzindua hofu       na huruma. 
iii) Vitendo vyote vinavyofanyika katika tamthiliya vinapaswa kuchangia katika ufanisi wa dhamira         za mtunzi. 
iv) Fani. Watunzi wa tamthiliya wanawajibika kutumia mbinu za kisanii zinazowashajiisha wasomaji       au watazamaji kuendelea kusoma au kutazamia maatokeo ya matendo yanayoigwa. Mbinu hizo ni       pamoja na jazanda, kejeli, ritifaa, tashbihi, tashihisi na uzungumzi nafsia. 
v) Wasanii bora ni wale wanaotunga tamthiliya zinazozungumzia kadhia zinazoweza kutimia katika        maisha ya binadamu. 
1.2 Drama za Kijadi Drama za kijadi ni zile sanaa za maonyesho ambazo zimechimbuka katika jamii za kiafrika, ikiwemo Tanzania. Sanaa hizo ni pamoja na Maelezo ya kina yanapatikana katika Dorsch,S.T.(1965)Aristotle/Horace/Longinus: Classical Literary Criticism. Penguin: Harmondsworth.  ngoma, majigambo, miviga ya ndoa, harusi, mazishi, jando na unyago, matambiko, utambaji hadithi, n.k. Katika shughuli hizi watu hufanya vitendo vya kisanaa kama vile uchezaji ngoma, uimbaji, upigaji muziki na utongoaji mashairi vikiambatana na matendo ya mwili na matumizi ya lugha. 
Vitendo hivi vya kisanaa ni mojawapo ya njia bora ya kuwasiliana kati ya watu na watu wengine, au watu na miungu na mizimu, katika jitihada za kuyakabili mazingira na kuendeleza jamii. Kwa kucheza ngoma watoto hufundishwa tabia inayotegemewa na jamii utu uzimani. 
Kwa kuimba, kucheza na kutenda, miungu huelezwa matatizo ya ukame, magonjwa, mafuriko, n.k. kwa kutamba hadithi watu hufunzwa historia ya jamii, tabia nzuri, jinsi ya kuishi na watu wengine n.k. 
1.3 Aina za Tamthiya 
Tamthiliya ni za aina kadha. Kila aina ina sifa zake maalum. Kimsingi, tunaweza kuvitumia vigezo vya muda (duration) na utanzu (genre) kuzigawa tamthiliya katika aina mbalimbali. Kwa mujibu wa kigezo cha kwanza, muda, kuna tamthiliya ambazo huwa na tendo moja na huchukua muda mfupi. 
Kwa mfano, tamthliya ya Samuel Beckett iitwayo ‘Breath’ inachukua muda wa dakika moja hivi kuigizwa ilhali ‘Maisha Subira’ iliyoandikwa na Omari, S. itachukua muda mrefu kuigiza. 
Kigezo cha muda hutegemea wakati ilhali cha utanzu hutegemea yaliyomo (maudhui) au mada ya tamthiliya. Kutokana na kigezo hiki cha pili tunaweza kuainisha vitanzu vifuatavyo: 
a) Tanzia (Tragedy) 
b) Futuhi/Komedia (Comedy) 
c) Melodrama (Melodrama) 
d) Kichekesho (Farce) 
e) Tanzia–ramsa/Tanzia-futuhi (Tragicomedy) 
f) Tamthiliya ya Kihistoria (Historical Play) 
g) Tamthiliya Tatizo (Problem Play) 
h) Tamthiliya ya Kibwege (Absurd Drama)
1.3.1 Tanzia (Tragedy) 
Kijelezi cha Dhana ‘Tanzia’ Tanzia ni aina ya tamthiliya yenye uzito unaodhihirika kihisia au kifikra. Tanzia huwa na suala, matendo na malengo dhati. Aristotle alikuwa mtu wa kwanza ambaye baada ya kuyatazama maandishi ya tamthiliya za Kigiriki aliandika maana ya tanzia katika kitabu chake cha Poetics . Kutokana na uchunguzi wake aliona tanzia kuwa ni tamthiliya yenye huzuni ambayo inagusa hisia za watazamaji kiasi cha kuogopesha na kumwonea huruma mhusika mkuu ambaye hupata janga. Na mara zote huyu mhusika mkuu huwa na mwenendo bora unaokubalika na jamii. Pia mwenye msimamo. Janga analolipata lisiwe kubwa kiasi cha kusababisha mtazamaji kuogopa sana hata kushindwa kumwonea huruma mhusika.
Aristotle aliuona utanzu huu kama ‘mwigo’ au ‘uigaji’ wa tendo ambalo lina udhati, ukamilifu, ubora na ukuu fulani. Kwa mujibu wa mtaalamu huyu, tendo hilo lazima liwe na uwezo wa kuwaathiri watazamaji na kuwafanya waingiwe na huzuni au kihoro pamoja na kuwa na uwezo wa kuzitakasa hisia za woga au huzuni katika kile alichokiita mtakasohisia. Mtazamaji mwishoni mwa tamthiliya alijiona katika hali ile ya yule aliyeanguka. Hali hii inamfanya atambue nafasi na hatima yake katika ulimwengu huu na kujiweka mahala pake anapostahili. Lugha iliyotumika ni ushairi. Tanzia aliyokusudia Aristotle iliwahusu wahusika wa hali ya mkwezo kama wafalme, malkia, miungu na wengineo. Watunzi maarufu wa tanzia ya kiyunani ni pamoja na Aeschylus, Sophocles na Euripedes. 
Hata hivyo, dhana ya tanzia sasa imepanuliwa kama ilivyo hata dhana ya shujaa wa kitanzia. Augusto Boal ambaye amekuja miaka mingi sana baada ya Aristotle amefanya uchambuzi wa kazi za tanzia. Anaiona tanzia ya Aristotle kama aina ya sanaa ambayo inatumiwa na wanasiasa kuwatawala watu. Muunda wa sanaa ya Kigiriki inagawa watu katika makundi mawili ya kitawala na kutawaliwa ambayo moja hutoa mawazo na lingine hupokea. Kule kuogopa na kumwonea huruma mhusika mkuu ambaye ni mtawala/mkuu ni kuendeleza utabaka uliopo kuwa mambo hayabadiliki. Boal anaiona tanzia ya Kigiriki kuwa ni ya ukandamizaji na haifai kuleta mabadiliko ya jamii . 
Steiner, G. naye anasema wakati huu tulio nao hakuna kitu kama tanzia. Anasema mambo yaliyofanya tanzia kuwepo hayapo tena hivyo tanzia imekufa6 . Mambo ambayo yalikuwa yakimshinda mhusika mkuu – nguvu za kiungu, hayapo tena kutokana na maendeleo ya binadamu. Hapo awali katika tanzia mhusika mkuu hakuwa na matumaini ya mambo kuwa mazuri punde anapoanguka. Huo ulikuwa mwisho wa  Aristotle (386 – 322 KM) kitabu hiki kinahusu ‘Sanaa ya Utunzi’. 
Mackeon, R. (1974) Aristotle. New York: Random House. Ukrasa wa 21 5 Boal, A. (1979) Theatre of the Oppressed. London: Pluto Press. Ukrasa wa 46,  Steiner, G. (1961) The Death of Tragedy. London: Faber & Faber. 5 kila kitu. Steiner anasema tanzia ilikuwepo wakati wa Sophocles, Shakespeare na Racine lakini baada ya hapo masuala yote yana ufumbuzi katika tamthiliya. Hata ushairi ambao ulizifanya kazi za tanzia zieleweke kwa wachache tu ukapotea na badala yake kuzuka lugha nathari (prose). 
Hivyo tamthiliya zote zenye masahibu makuu lakini zenye fikra au uelekeo wa ukombozi sio tanzia bali tamthiliya nzito. Kwa upande wake, Wole Soyinka anaamini kuwa licha ya kuwepo mabadiliko katika maisha na fikra za binadamu, bado tanzia, kama ilivyoletwa na Wagiriki ipo na inahitajika. Soyinka huona kuwa janga limpatapo mhusika katika tanzia halimhusu yeye binafsi tu, bali linavuruga hali nzima ya utulivu ya jamii yake. Jamii ya mhusika wa tanzia ya Kiafrika, kwa mfano, hujumlisha wale waishio na waliokufa – mizimu na miungu . 
Kiwango cha uzito wa tanzia kutokana na Soyinka ni kikubwa zaidi ukiangalia idadi ya wale wote wanaohusishwa na janga hilo. Kimsingi, wasomi wote hawa isipokuwa Steiner wanakubaliana katika uwepo wa tanzia. Hata kwa Steiner maendeleo ya binadamu anayoyasifia kuwa yameua tanzia bado yameshindwa kuondoa uovu katika binadamu, ambacho ni kipengele muhimu kinachosababisha janga kwa binadamu. Maendeleo ya mahusiano kati ya binadamu yapo bado kama hapo awali. Mikondo Minne ya Tanzia Kuna mikondo minne ya tanzia, nayo ni: Tanzia ya Urasimi (Classical Tragedy), Tanzia ya Urasimi Mpya (Neo-classical Tragedy), Tanzia ya Kisasa (Modern Tragedy) na Tanzia ya Kikomunisti (Socialist Realism Tragedy). i) Tanzia ya Urasimi (Classical Tragedy) Hii iliweza kuwepo kutokana na tabaka la mabwanyenye kufadhili sanaa huko Ugiriki. Hivyo liliitumia tanzia kwa manufaa yake yenyewe. Mengi yanayojitokeza kwenye tanzia hizi ni kwa ajili ya kukudhi matakwa ya tabaka hili. Mambo yanayoonyesha hali hii ni ‘status quo’ ambapo mhusika mkuu sharti awe mtu bora ambaye kutokana na kutokamilika kwake kimatendo kwa ajili ya ubinadamu wake anapata janga ambalo linamtoa katika hali ya juu aliyokuwa nayo na kuwa duni. Aidha, wakati wa urasimi fikra za watu ziliiweka miungu kama yenye kauli ya wema au uovu katika yote yaliyofanyika duniani; hivyo  Soyinka, W. (1976) Myth, Literature and the African World. Cambridge: Cambridge University Press. Kurasa 37 - 60  Yaani ‘hali kama ilivyo’  mawazo haya yamesababisha mhusika mkuu kuangushwa na nguvu hizi za kiungu ambazo hawezi kushindana nazo. 
Nguvu hizi za kiungu hutawala matendo na matukio ya wahusika. Mawazo ya wakati huu yaliheshimu hadhi ya binadamu na kuyaona maisha yake yenye maana na kuthaminika. Ingawa binadamu si rahisi kueleweka (ni changamano), anahusika kwa njia moja au nyingine na masahibu yanayomkuta. Katika tanzia hizi binadamu yu huru kufuata ushauri wake mwenyewe na ni katika kufanya hivi ndiyo tabia yake hujitokeza. Ukaragosi hauna nafasi katika tanzia. Karagosi siku zote haaminiki na hudharaulika, hivyo hafai kuwa mhusika mkuu. Anatakiwa mtu ambaye ingawa anakabiliwa na magumu yamshindayo, haonyeshi ukaragosi bali huwa na msimamo maalum. 
Lugha ilitumika pia kukidhi matakwa ya tabaka tawala. Lugha ya tanzia ilikuwa ya kishairi ambayo ilisababisha mgawanyiko kati ya watazamaji wa hali ya chini na ya juu. Waigizaji kutenganishwa na watazamaji kulisaidia upande mmoja kubugia yale ambayo upande mwingine uliyatoa. kuwepo kwa kiitikio/kibwagizo ilikuwa ishara ya demokrasia au sauti ya wengi. Mfano wa tanzia ya urasimi ni Mfalme Edipode . Tanzia hii inaanza na hali mbaya ya magonjwa ya kufisha katika mji wa Thebe. Watu wa Thebe wanakusanyika kuzungumza juu ya janga hili. Inabainika kuwa hali mbaya ya Thebe inatokana na kuuliwa kwa mfalme wa zamani Laio. Ili janga litoweke, sharti muuaji ambaye yu miongoni mwa watu wa Thebe apatikane. Mfalme Edipode anaamua kufuatilia jambo hili mpaka huyo muuaji aliyelaaniwa apatikane. 
Chanzo cha maovu katika tanzia hii ni utabiri wa hapo kale wa miungu kuwa mfalme Laio atauawa kwa mkono wa mwanawe mwenyewe ambaye pia atamwoa mama yake. Katika uchunguzi wake anagundua kuwa yeye ndiye aliyemuua Laio na pia kumwoa mama yake. Haya ni matukio maovu ya utabiri ambayo waliohusika walijaribu kuyakwepa na kushindwa. Anapogundua tanzia yake, Edipode anajipofusha na kuhamia ughaibuni. Kabla janga halijamtokea mhusika mkuu, sharti apitie awamu tatu – ‘harmatia, perepeteia na anagnoris’. Tanzia ya urasimi ianzapo, mhusika mkuu anaonyesha dosari katika tabia yake – harmatia. Mara nyingi mhusika mkuu huwa amefikia hali aliyonayo sasa kutokana na dosari. Mhusika mkuu hubadilika pale  mambo yaanzapo kumwendea kombo, anapitia awamu ya perepeteia. Licha ya mambo kumgeukia, anagundua kuwa ana dosari; kitu alichotenda kimesababisha mabadiliko kutoka ya ufanisi na kuwa ya kudidimia – anagnoris. Mhusika mkuu anapaswa kukubali kosa lake na kamwe hafanyi ajizi kwa kulikimbia janga linalomngojea (catastrophe). Janga linalotokea husababisha mhusika kufa au wapenzi wake kufa. Mara kwa mara hata ikiwa mhusika hafi, yanayompata ni mabaya zaidi ya kufa. 
Awamu zote ni kumfanya mtazamaji kuondokana na hisia (catharsis) ili awe mtu bora zaidi baada ya onyesho la tanzia10 . ii) Tanzia ya Urasimi Mpya (Neo-classical Tragedy) Wakati huu pia tabaka tawala limechangia katika kuifanya tanzia iwe kama ilivyo. Tabaka hili ndilo lililomiliki sanaa hivyo liliingiza mawazo yake katika tanzia. Huu ulikuwa wakati wa utaifa kwa Waingereza hivyo mambo mengi yaliyotokea nje ya taifa hili yaliachwa. Isitoshe, katika kudhamini tamthiliya, Ufalme wa Uingereza ulikataza tamthiliya ya kugusia mambo ya kidini na kitawala. Ufalme ulikuwa tayari kudhamini tamthiliya kama chombo cha kuleta burudani tu. 
Wakati huu kulikuwepo kwa mwamko wa kifikra uliojulikana kama ‘cartesian rationalism’ – ambao uliweka maanani sana tofauti kati ya umbo la ndani na la nje – hususan kuhusu tabia ya binadamu11 . Miungu na mashetani waliendelea kuwepo kwenye tanzia hizi na walikuwa na uzito. Ila kutokana na mwamko wa fikra mpya uliokuwepo watu walifanya uchunguzi wa kina kwanza ili kupambanua kati ya miungu halisi na bandia. Fikra hizi ambazo zilikuwa uzao wa tabaka tawala zilionekana kwenye tanzia wakati huu. Mhusika mkuu aliendelea kuwa wa tabaka la juu. Lugha iliendelea kuwa ya kishairi isipokuwa wakati mwingine watu wa chini waliongea lugha ya kawaida. Huu ni ubaguzi ambao ulibagua kati ya watazamaji wa kawaida na wale wa hali ya juu ambao walifuatilia vizuri zaidi matukio ya jukwaani. 
Mwakilishi mkuu wa wakati huu ni William Shakespeare (1564 – 1616) ambaye licha ya kuona tanzia kuwa ni sababu ya uovu ambao mtu humtendea mwingine, hakwenda mbali kuonyesha undani wa mahusiano haya bali aliishia kwenye kuzingatia dhamira sana. Mara 10 Rejelea Baoal (1979) Ibid. 36 – 37 Kwa maelezo ya kina zaidi 11 Grierson, H.  Cross Currents in English Literature of the Seventeenth Century. London: Peregrine Books. Page 99 – 127. 8 nyingi mhusika wake kwenye tanzia alitatanishwa na dhamira yake mwenyewe. Mfano mzuri ni tanzia yake ya Hamlet12 ambayo mbali na kuonyesha uovu utendekao katika jamii pia kuna mvutano wa dhamira kati ya mhusika huyo huyo mmoja. Kazi zake nyingine ni kama vile Makbeth, Juliasi Kaizari, Tufani na Mabepari wa Venisi. Izingatiwe kuwa Shakespeare aliliandikia tabaka tawala hivyo katu hakuonyesha mgongano wa kitabaka. Alionyesha mambo kuwa ni ya kudumu na hayabadiliki. iii) Tanzia ya Kisasa (Modern Tragedy) Tanzia hii imechipuka kutokana na mabadiliko ya fikra na maisha yaliyotokea Ulaya katika karne ya 18. Huu ni wakati ambao ubepari ulianza kushamiri hasa kutokana na kuvumbuliwa kwa mashine ziendazo kwa mvuke (steam engines). Wakati huu ulijulikana kama Mapinduzi ya Viwanda (Industrial Revolution). Ni wakati ambao watu wengi iliwabidi kwenda mijini kufanya kazi viwandani. Miji ikafurika na hali mbovu za maisha zikajitokeza. Hali hii ikawafanya wafanyakazi hawa wawe na ufahamu wa unyonyaji uliokuwa ukiendelea. Msemo mashuhuri wa wakati huo, ‘watu wote wameumbwa kuwa huru na sawa’ ulichangia kwa kiasi kikubwa katika kujenga mawazo tofauti na yale ya urasimi mpya. Wanafalsafa Auguste Comte na Charles Darwin walichangia kwa kiasi kikubwa kutokana na kazi zao za ‘Positivism’13 na ‘Origin of species’ zilizoandikwa karne ya 18. Wanafalsafa hawa walihamasisha watu kutumia sayansi kutumia sayansi katika maswala ya jamii kutafuta chanzo cha matatizo na kudhibiti matokeo yake. Walihamasisha watu kutafuta njia za kufanya ili maarifa yote yahudumie matakwa ya wakati uliopo. Hivyo kila tawi la maarifa likajihusisha katika mambo ya wakati huo. Tanzia nayo ilienda sambamba na mabadiliko haya. Mungu au miungu haikuwa tena na nafasi yoyote kwenye maisha ya binadamu. Yote yaliyomsibu binadamu yalikuwa na chanzo chake katika maisha haya haya yenye kufahamika na milango mitano ya maarifa/hisi/fahamu. Rousseau anasimamia msimamo huu kwa kusema kuwa kiini cha uovu hutokana na jamii na sio nje ya jamii. Mhusika mkuu aliyekumbwa na janga alitoka katika ngazi yoyote ya jamii. Mhusika huyu alisakamwa na: mtu mwingine, nafsi yake na jamii. 12 Shakespeare, W. (1958) Hamlet. London: Penguin. 13 Pia Falsafa ya Umbile. Hii ni falsafa inayozingatia tu mambo yanayoonekana na kujulikana vyema na wanadamu. 9 Lugha nayo ikabadilika kutoka ya ushairi hadi ya kawaida ili kurahisisha mawasiliano. Iliunganisha kwa ufanisi zaidi mwigizaji na hadhira yake. Licha ya lugha kuunganisha mwigizaji na mtazamaji, bado kiini kikubwa cha tanzia kilibakia kuwa ‘Catharsis’14 kama katika mikondo ya awali. Ingawa mtazamaji alijitambulisha na mhusika mkuu kwa yale magumu yanayompata, Steiner haoni kuangamia kwa mhusika mkuu kuwa ndio mwisho bali kulitoa fundisho kwa jamii kuwa inaweza kubadilika na hatimaye kupata mwisho mzuri. Huu mwisho mzuri ungepatikana aidha kwa kubadilisha hali mbaya ya maisha na kuwa nzuri au kupata mwisho mzuri kutokana na mawazo ya kidini ya maisha baada ya kifo. Henrich Ibsen (1828 – 1906) ndiye aliyeashiria mwanzo wa tanzia ya kisasa kuanzia 1870. Tanzia hizi zilionyesha jinsi misingi potovu ya jamii ilivyoangusha watu. Katika tanzia yake ‘Ghosts’15 (Mizuka) mwanamke anashurutishwa kukaa na mumewe ambaye hampendi. Isitoshe, ni mwanaume ambaye kutokana na tabia yake ametengwa na jamii. Mtoto wa kiume wanayemzaa anarithi kaswende kutoka kwa babake. Mwisho wa tanzia kijana wa kiume anahehuka na mama mtu anapata wenda wazimu. Matukio haya husababishwa kwa kwa sababu jamii hushurutishwa kufuata maadili potovu. Arthur Miller (1915 - ) katika tanzi yake ya ‘Kifo cha Mfanyabiashara’ (Death of a Salesman)16 iliyoandikwa 1949, anazungumzia mhusika mkuu Willy Loman ambaye ni mfanya – biashara. Katika maisha, yeye anataka apendwe, ajulikane na asifiwe. Anafahamu kuwa mambo yote haya anaweza kuyapata ikiwa atapata mafanikio maishani. Kwa Willy mafanikio ni utajiri na anaamini mtu hawezi kupendwa bila kuwa na mafanikio. Willy anadhani watoto wake hawampendi kwa sababu hajafaulu maishani. Watampenda tu kama atafanikiwa. Anaamini kuwa mapenzi ni kitu cha kutafutwa au kununuliwa na hakitolewi bure. Pia anawaeleza wanawake kuwa hawataheshimiwa kama hawatakuwa na mali. Anagundua mtoto wake Biff anampenda kwa dhati ingawa wote hawana mafanikio. Tendo hili linampa fununu kuwa amekuwa akiamini imani potofu. Fununu inatokea mwisho wa tanzia ambapo pia Willy anapata ajali ya gari. Katika ‘A Doll’s House’17, mwandishi Ibsen anaonyesha jinsi mhusika Nora anavyotaka kubadili maisha yake duni na magumu 14 Yaani ‘mtakaso hisia’, kutoa au kupoza hisia zilizochemka 15 Ibsen, H. (1965) Ghosts. London: Bard. 16 Miller, A. (1968) Death of a Salesman. Nairobi: East African Educational Publishers. 17 Ibsen, H. (1906) A Doll’s House: The Collected Works of Henrich Ibsen Volume VII. London: Heinemann. 10 yanayosababishwa na mumewe. Nora anaamua kumwacha mumewe na watoto ili aweze kuamua mambo yake mwenyewe. A Doll’s House ni tanzia iliyoshambulia ndoa na maisha ya familia kuwa chanzo cha hali ngumu kwa wahusika. Hivyo kwa Steiner mhusika wa tanzia hii ya kisasa haangamii kabisa kwa sababu majibu ya matatizo yake yapo na kama ni anguko ni anguko la muda tu. Tanzia za kisasa zina mielekeo tofauti hasa ukizingatia kuwa mawazo ya binadamu hayana mipaka na watu sehemu mbali mbali hawabanwi na mawazo na itikadi za aina moja tu. iv) Tanzia ya Kikomunisti (Socialist Realism Tragedy) Tanzia hizi zimetokana na mawazo ya Marx na Ukomunisti18 ya kutaka kuleta jamii isiyo na matabaka duniani. Tanzia za aina hii ni za matumaini juu ya ushindi wa ujamaa duniani na lazima ziongelee kuhusu hilo tu. Ni mwiko kwa mhusika mkuu wa tamthiliya hizi kushindwa kuutangaza ujamaa duniani. Ni tanzia ionyeshayo jinsi jamii nzima inavyobadilika na kuwa ya kikomunisti. Mwisho wa tanzia hizi hutakiwa kuwa mzuri kwa ushindi wa ujamaa. Mawazo yaliyotawala tanzia hizi yalitokana na chama cha Ukomunisti huko Urusi na ni fikra ambazo zililazimishwa kwa wanaotawaliwa hasa ukichukulia kuwa jamii hiyo pia ililazimishwa kuwa ya mfumo wa chama kimoja. Matabaka ya wakati wa Kigiriki na wa Shakespeare hayatofautiani ya kipindi hiki. Wananchi wa Urusi walilazimishwa kubugia mawazo ambayo hawakuyapenda. Huu toka mwanzo ulikuwa ukandamizaji wa haki za binadamu au uwepo wa uovu kama katika matabaka yote yaliyotangulia. Wahakiki wa tamthiliya hii wanaposema tanzia haina nafasi katika jamii yao ni kuwakoga wananchi kuwa wategemee maisha yasiyowezekana19 . Lugha iliyotumika ni ya kawaida ili kuleta maelewano bora kati ya waigizaji na watazamaji. Kulikuwepo na mtengano maalumu kati ya mwigizaji na mtazamaji. Miungu haina nafasi kubwa kabisa kwenye tanzia hizi. Mhusika mkuu wa tanzia hizi ambaye ni mhusika aliyejengwa kipropaganda kwa manufaa ya siasa ya kikomunisti huitwa mhusika mkuu wa matumaini. Naye ana sifa zifuatazo: 18 Marx, K. & Engels, F. (1969) The Communist Manifesto: Selected Works Volume I. Moscow: Progress Publishers. Pages 98 - 137 19 Lunacharsky, A. (1973) On Literature and Art. Moscow: Progress Publishers. 11 o Yeye ni mfano kati ya mifano. o Amefikia kiwango cha juu zaidi cha ubinadamu, hana ubinafsi. o Hana makosa yoyote (kama anayo ni madogo sana kama kukasirika hivi wakati fulani fulani). Na anaweza kuwa na mambo yasiyofaa ya kujiosha akielekea kwenye kiwango cha juu cha maisha lakini yasiwe kikwazo kwake. o Lazima aielewe siasa barabara. o Awe na akili. o Awe na moyo wa ushupavu. o Awe na uzalendo. o Aheshimu wanawake. o Awe tayari kujitoa mhanga. o Ana msimamo mmmoja tu; nao ni kufikia kilele cha ukomunisti. Hachanganyi weupe na weusi. o Akipatwa na shida anajua ni lazima aikwepe ili afikie lengo lake. Mfano mzuri wa tanzia hizi ni ‘The Measures Taken’20 ya Brecht. Katika tanzia hii, mhusika mkuu – The Young Comrade – anajitoa muhanga ili wenzake waweze kueneza ukomunisti nchini China. Brecht hakuwa muasisi wa tanzia hizi isipokuwa alikubali kubadili jamii. 1.3.2Futuhi/Komedia (Comedy) Futuhi au komedia ni utungo ambao unachekesha na kuchangamsha. Tamthiliya ya aina hii inaweza kutusawiria picha yakini katika maisha yetu kwa undani ikitumia dhihaka na kejeli kwa kuchekesha. Futuhi huficha ukali wa masuto kadri inavyoendelea kutuburudisha. Futuhi hulenga kurekebisha tabia inazozidhihaki au inazozicheka. Kusema futuhi inafurahisha haina maana kuwa dhamira yake haina uzito. Futuhi huzungumzia masuala ya kijamii, kisiasa na kiuchumi kwa njia ya kuchekesha. Futuhi huweza kuwa na sifa zinazotofautiana – jambo ambalo hutumiwa kama kigezo cha kuainisha aina mbalimbali. Lakini vyovyote iwavyo, futuhi hujikwepesha na masuala, kutia hofu au kushtua. Athari ya futuhi (kuchekesha) hutokana na matendo, mienendo ya wahusika na hitilafu au ila za kuingiliana kwa kiusemi. Futuhi huwa na viwango mbalimbali vya kuchekesha. Kwanza, kuna kiwango hafifu (duni) ambacho huhusishwa na Futuhi ya Chini21. Kuna 20 Brecht, B. (1960) The Measures Taken. The Jewish. 21 Ucheshi unaopatikana katika futuhi ya aina hii ni rahisi kutambulikana na aghalabu waigizaji hutenda vitendo vya kuchekesha vilivyo wazi. 12 baadhi ya kazi ambapo kiwango cha kuchekesha huwa kigumu kutambulikana na huhitaji utambuzi mpevu. Hii ni sifa ya aina ya futuhi iitwayo Futuhi ya Juu22. Aina zingine ni pamoja na: Futuhi ya Kikanivali, Futuhi ya Kitashtiti, Futuhi ya Maadili, Futuhi ya Mawazo, Futuhi ya Ucheshi na Futuhi Zimbwe. Mifano mizuri ya futuhi ni ‘Aliyeonja Pepo’ (Topan, F.), ‘Usaliti Mjini’ (Imbuga, F.), Twelfth Night (Shakespeare, W.), Importance of Being Earnest (Wilde Oscar), Mkaguzi Mkuu wa Serikali (Gogol, Nikolai), The Lion and the Jewel (Soyinka, W.) na ‘Masaibu ya Ndugu Jero’ (Soyinka, W.). 1.3.3Melodrama Katika zama za urasimi, aina hii ilitumiwa kuelezea aina ya drama au tamthiliya iliyokuwa na matumizi mengi ya uimbaji au nyimbo (melos). Kwa hiyo, melodrama ni dhana inayotumiwa kuelezea aina ya tamthiliya ambayo imetawaliwa na uimbaji wa nyimbo. Melodrama inafanana sana na tanzia ingawa mara nyingi nguli wa melodrama humalizika na ushindi, matokeo yake yanasisimua sana na mwendo wa msuko wake huwa ni wa haraka haraka zaidi. Wahusika wake huvutia na kufurahisha lakini hawana sifa za kishujaa. Dhamira ya melodrama huzungukia mvutano kati ya wema na uovu au ubaya. Miishio ya tamthiliya hizi haina sifa ya mtakasohisia kama ilivyo na tanzia bali huwa ni aina ya ushindi wa mhusika mwema. Mfano mzuri ni ‘The Begger’s Opera’ iliyotungwa na mwanatamthiliya wa Kiingereza John Gay kunako 1728. 1.3.4Kichekesho (Farce) Kichekesho ni aina ya tamthiliya ambayo huwa na uwezo wa kusababisha kicheko kingi kutokana na mbinu za kifutuhi ya chini kama ucheshi, hali zisizokuwa za kawaida au wahusika wasio wa kawaida kama vile wahusika wa kiume huweza kuvaa mavazi ya wahusika wa kike na wale wa kike kuyavaa mavazi ya kiume, visa vingi vya mapenzi ya kuchekesha, mikimbizano jukwaani, matukio ya kiajabu, kuchezea maneno, nk. Kichekesho huwa na wahusika, matendo, mazingira na vitushi vya kuchekesha kwa jinsi vilivyotiliwa chumvi. Ingawa Kichekesho kinahusiana na Futuhi, kinatofautiana nayo kutokana na sifa yake ya kudhamiria tu kuibusha kicheko na kutumbuiza. Futuhi pia hutumbuiza lakini zaidi ya hivyo inalenga kurekebisha tabia inazozicheka. ‘Charley’s Aunt’ ya Brandon Thomas ni mfano wa kichekesho maarufu. 22 Ucheshi wake huhitaji ung’amuzi au akili kuugundua. Kwa kawaida ucheshi wa futuhi ya juu hufumbatwa katika matumizi ya lugha na ni nadra sana kutegemea matendo au miondoko ya waigizaji. 13 Kichekesho hiki kilitolewa kwa mara ya kwanza1892. Vichekesho vingi vya Kiswahili havichapishwi kama vitabu. 1.3.5Tanzia–ramsa/Tanzia-futuhi (Tragicomedy) Tanzia-ramsa ni aina ya tamthiliya ambayo huonyesha mabadiliko ya aina fulani yanayogeuza mwelekeo wa matukio ya kitanzia na kuufanya kuwa tofauti au wa kufurahisha. Hali hii inaweza kupatikana kwa kuwepo kwa hasidi au mui anayetubu na kuyajutia makosa au msimamo wake au kuwepo kwa mandhari ya kiulimbwende. Kimsingi, tanzia-ramsa ni tanzia inayoishia kwa furaha. Kinyume chake ni Futuhi Zimbwe23. Dhana hii inaakisi kwa kiasi kikubwa baadhi ya mitazamo ya kidhanaishi ya fasihi ambapo ushujaa na tanzia havijitokezi katika hali ya kawaida kama vilivyozoeleka. Hali hii inadhihirika katika tamthiliya kama vile ‘The Cherry Orchard’ (Anton Chekhov, 1904), ‘The Winter’s Tale’ (William Shakespeare, 1611). Utanzu huu wa tamthiliya sio maarufu miongoni mwa wanatamthiliya wa Kiafrika. 1.3.6Tamthiliya ya Kihistoria (Historical Play) Hii ni tamthiliya inayojengwa kutokana na mhusika au matukio ya kihistoria. Mifano ni ‘Kinjeketile’ (Hussein, E.), ‘Mkwava wa Uhehe’ (Mulokozi, M.), ‘Mzalendo Kimathi’ (Ngugi, T) na ‘Mnara Wawaka Moto’ (Rocha Chimerah). 1.3.7Tamthiliya Tatizo (Problem Play) Tamthiliya hizi pia huitwa Tamthiliya Tasnifu au Tamthiliya Tanzo. Utanzu huu wa tamthiliya huzungumzia suala fulani katika jamii. Ni tamthiliya inayojenga dhamira yake juu ya tatizo mahsusi la kijamii. Dhamira hiyo hujengwa kupitia kwa mhusika mkuu ambaye anakabiliana na tatizo ambalo ni kielelezo cha mazingira yake ya kijamii. Katika tamthiliya ya Kithaka wa Mberia, ‘Natala’, kwa mfano, tatizo la kudunishwa kwa mwanamke, ambalo mhusika mkuu (Natala) anakabiliana nalo ni kiwakilishi cha hali ya mwanamke katika jamii nyingi za Kiafrika. Tamthiliya hii inashughulikia suala la mwanamke katika jamii inayoendelea kutawaliwa na itikadi inayopendelea wanaume na inayozingatia desturi za kumrithi mke baada ya kifo cha mumewe. Mifano mingine tamthiliya tatizo ni ‘Nguzo Mama’ na ‘Lina Ubani’ (Muhando, P.), ‘Kifo Kisimani’ (Mberia, K.),‘Mashetani’ (Hussein, E.) na ‘Mama Ee’ (Mwachofi, K.). Sio lazima mtunzi wa tamthiliya tatizo atoe 23 Aina ya Tanzia-ramsa ambayo huisha kwa namna ya kukatisha tamaa au kusikitisha. 14 suluhisho la tatizo analolishughulikia. Hata hivyo, baadhi ya watunzi wa kazi za aina hii hupendekeza soluhisho fulani. 1.3.8Tamthiliya ya Kibwege (Absurd Drama) Hizi ni kazi za sanaa ambazo hupuuza kaida zinazotarajiwa za utunzi wa tamthiliya. Ni tamthiliya ambazo huelekea kudokeza kuwa maisha yana uwazi usiokuwa na maana au hayana maana. Waandishi wanaoakisi mawazo ya aina hii wameathiriwa kwa kiasi kikubwa na udhanaishi. Wahusika wanaopatikana katika tamthiliya za aina hii huweza kujitokeza katika sura mbalimbali, kubadilisha hata jinsia, masuala ya maonyesho hayatiliwi maanani, mfuatano wa kiwakati unapuuzwa na mpaka uliopo kati ya uhalisi na utohalisi huvunjwa. Katika fasihi ya Ulaya waandishi wanaohusishwa na mtazamo huu ni Samuel Beckett (Waiting for Godot, 1956 na Endgame, 1959) na Eugene Ionescu (The Bald Prima Donna, The Lesson, The Chairs na Rhinocerous). Katika fasihi ya Kiswahili sifa za aina hii zinajitokeza katika tamthiliya ya ‘Amezidi’ (Mohamed, 1995) na ‘Upotovu’ (Njiru Kimunyi, 2000). 1.4 Dhima za Tamthiya Husababisha mawasiliano ya kisanii kati ya makundi mawili ya watu – waigizaji na watazamaji (hadhira) yatokee. Huburudisha – tamthiliya inapoonyeshwa jukwaani hutoa burudani. Hufundisha na hata huhamasisha. Katika tamthiliya huwepo adili (funzo) na ujumbe ambao unawaelekeza, kuwaadibu, kuwaonya na kuwaongoza kwenye matarajio ya jamii husika. Taasisi nyingi zimekumbatia tamthiliya kufundishia malengo yao na pia kwa propaganda. Tamthiliya ina nafasi kubwa kukuza lugha ya kiswahili. Lugha ya tamthiliya ni lugha maalum ambayo hueleza migongano kwa muhtasari na hii huifanya tamthiliya kuwa mahala pafaapo kwa kujifunza utaalam huu. Mapato: kitabu kinapouzwa mwandishi hupata kipato. Tamthliya inapoonyeshwa jukwaani, viingilio humpatia msanii kipato. Sehemu nyingi siku hizi wanatamthiliya hupata mshahara. Wasomi na waandishi wa fani ya tamthiliya huajiriwa katika sehemu nyingi kama mashuleni, vyuoni, taasisini, redioni na kwenye studio za televisheni. Tamthiliya ina nafasi ya kipekee katika kuhifadhi zile sanaa za maonyesho za asili ambazo zimepitwa na wakati na zile ambazo bado zinatumika kwa kuzitia katika fani ya tamthiliya. Hii licha ya kuzifanya 15 tamthiliya zetu ziwe na upekee wa kitanzania bali pia zitautangaza utamaduni huu. Lengo la serikali likiwa ni kumfanya kila mwananchi ajue kusoma na kuandika, tamthiliya ina nafasi kubwa huko mbele kwani kipengele cha usomi ambacho sasa ni kikwazo kikubwa kitakuwa kimeondoka. Tamthiliya zinaweza kutumiwa kufundishia baadhi ya masomo ya shule za msingi. 1.5 Maswali ya Marudio 1. Tamthiliya ni nini? Eleza kwa kutoa mifano mwafaka. 2. Fafanua sifa zozote SITA zinazoutambulisha utanzu wa tamthiliya. 3. Eleza dhima ya tamthiliya katika jamii. 4. Eleza kwa tafsili dhana zifuatazo: a) Sanaa za Maonyesho b) Drama za Kijadi c) Drama 5. Toa maelezo mafupi kuhusu tanzu za tamthiliya zifuatazo: a) Futuhi b) Tamthiliya ya Kibwege c) Melodrama d) Kichekesho e) Tanzia-ramsa f) Tamthiliya ya Kihistoria g) Tamthiliya Tatizo
Powered by Blogger.