TAFSIRI NA UKALIMANI

TAFSIRI NA UKALIMANI

DHANA, DHIMA NA HISTORIA YA TAFSIRI
Tafsiri ni uhawilishaji wa mawazo kutoka lugha moja ya maandishi kwenda lugha ingine ya maandishi. Mawazo yanayoshughulikiwa katika tafsiri sharti yawe katika maandishi na si vinginevyo, pia mawazo kati ya lugha chanzi na lugha lengwa sharti yalingane. (Mwansoko, 1996:1).
HISTORIA FUPI YA TAFSIRI
Maendeleo ya kiuchumi, kisayansi na kiutamaduni yanayofurahiwa leo duniani yalitokana na juhudi za ugunduzi wa watu wa kale na yalizifikia nchi mbalimbali kwa njia ya tafsiri.
Inasadikika kuwa sayansi na taaluma za kisasa zilianzia Afrika huko Misri miaka 3000 na zaidi kabla ya Kristo.
Ugunduzi na ustaarabu wa Ulaya kwa karne za baadaye hususani karne ya 19 ulitokana na ugunduzi wa Afrika. Mbinu kuu katika kueneza elimu hii ya Wamisri huko Ulaya ilikuwa ni tafsiri. Wasomi wengi wa Ulaya walijifunza lugha ya Misri na kuishi huko kwa miaka mingi na hatimaye walitafsiri elimu hii ya Wamisri na mambo yote waliyojifunza huko na kuyasambaza Ulaya.
Wakati wa himaya ya Warumi hasa baada ya Ukristo kuenea Ulaya nzima, elimu hiyo ya zamani ilianza kupigwa vita kwa kudaiwa kuwa ni ya kipagani. Hali hiyo ilisababisha kuibuka kwa kipindi kilichojulikana kama, The dark ages yaani, zama za giza.
Baada ya Uislamu kuingia na kuimarika, wasomi wengi wa ki-Islam waliipekua elimu ya kale ya Wamisri wakaifasiri kwa Kiarabu na kuipanua na kuijaliza kulingana na maendeleo ya wakati huo. Hii ilichochea mlipuko wa ustawi na maendeleo ya tafsiri.
Karne ya 19 tafsiri kwa kiasi kikubwa ilikuwa ya mkondo au mwelekeo mmoja ambapo vitabu vya waandishi na wanasayansi mashuhuri kutoka nchi zilizoendelea vilitafasiriwa kwa ajili ya wasomaji wa nchi zinazoendelea.
Karne ya sasa inajulikana kama karne ya tafsiri kwa sababu mikataba mingi ya kimataifa kama ya mashirika ya umma na binafsi sasa inafasiriwa kwa yeyote anayehitaji taarifa hizo. Maendeleo ya haraka ya teknolojia na haja ya kueneza mahitaji ya tafsiri vinachochea kukua kwa taaluma hii.
Nchini Tanzania taaluma ya tafsiri haina historia ndefu. Tafsiri ya kwanza katika Kiswahili inayofahamika ni Utenzi wa Hamziyyauliotungwa huko Misri karne ya 13 na kufasiriwa kwa Kiswahili na Bwana Idarus bin Athuman aliyeishi kaskazini mwa Kenya miaka ya 1700 – 1750.
Kipindi cha ukoloni kazi mbalimbali zilitafsiriwa na wamisionari kwa mfano Biblia (Injili ya Luka na Yohana), Hekaya za Abunuwasi na hadithi nyingine, Alfu – Lela Ulela (siku elfu na moja), Safari za Allan Quartermain, Robinson Cruso, n.k
Baada ya uhuru wazawa walifanya juhudi za kufasiri vitabu bora vya ulimwengu kwa Kiswahili mf. Mwl J.K Nyerere alifasiri vitabu viwili vya mwandishi mashuhuri wa Uingereza William Shakespeare vilivyojulikana kama  Juliasi Kaizari  na  Mabepari Wa Venis. Mwingine ni Paul Sozigwaaliyefasiri kitabu cha Song of Lawino.  Kwa ujumla wananchi wengi waliokuwa na ujuzi wa lugha za kigeni walifasiri maandishi mbalimbali muhimu kwa lugha ya Kiswahili ili kueneza maarifa na taaluma kwa wazawa wenzao.
Kutokana na taaluma ya tafsiri hivi sasa Kiswahili kina hazina ya falsafa, fasihi, sayansi na ufundi toka lugha za mataifa mbalimbali kama Uingereza, Ufaransa, Uarabuni, Ureno, n.k
Pamoja na mafanikio ya shughuli za kifasiri nchini Tanzania baadhi ya tafsiri zilizopo zinaonesha kasoro katika uchaguzi wa kazi za kufasiri, kazi zilizofasiriwa toka lugha za asili ni ile ya Anicet Kitereza  inayoitwa Bwana Muyombekere na Bibi Bugonoka, Ntulanalwo na Bulihwali (1980) kutoka lugha ya Kikerewe.
Hivi sasa huduma ya tafsiri nchini Tanzania inatolewa na Idara mahususi za tafsiri chini ya Taasisi ya iliyokuwa Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) ambayo sasa inaitwa Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (TATAKI), Shirika la Habari Tanzania (SHIHATA) na International Language Orientation Services.
Maslahi na haki za wafasiri zinalindwa na kusimamiwa na chama cha wafasiri wa Tanzania kilichoanzishwa mwaka 1981.
DHIMA/KAZI YA TAFSIRI
Dhima ya tafsiri katika maendeleo ya binadamu ni kubwa kutokana na ukweli kwamba tafsiri ndio daraja kati ya jamii mbalimbali za watu wanaotumia lugha zinazotofautiana.
           Tafsiri ina dhima zifuatazo:
    1.   Tafsiri kama njia ya mawasiliano
Tafsiri hutumika kutolea maelezo ya kibiashara kama vile jinsi ya kutumia bidhaa zinazouzwa nchi za nje, matangazo ya biashara kupitia broshua zenye fasiri katika vyombo vya habari na katika nyaraka rasmi kama mikataba na ripoti za kimataifa, makala za kitaaluma, vitabu vya kiada na ziada. Tafsiri katika mawasiliano imeongezeka sana kutokana na utegemezi wa mataifa yanayoendelea kwa nchi zilizoendelea kiuchumi, kiutaalamu na teknolojia. Hata hivyo, ni muhimu kufanya tafsiri ya kimawasiliano kwa umakini mkubwa ili kuepuka upotoshaji wa taarifa kwa mfano katika matumizi ya dawa iwapo mfasiri atafasiri kinyume huweza kusababisha madhara kwa mtumiaji.
    2.   Tafsiri kama nyenzo ya kueneza utamaduni
Tafsiri hutumiwa pia kama nyenzo ya kueneza tamaduni za jamii za ulimwenguni kupitia tafsiri na mwingiliano wa mataifa mbalimbali mathalan, jamii za kiafrika utamaduni wake umeathiriwa sana na tamaduni za jamii za Ulaya kwa mfano chakula na ulaji. Kwa upande mwingine, maandishi ya kitafsiri yanayoendelea kufasiriwa kutoka lugha moja hadi nyingine yanazidi kueneza utamaduni mpya kutoka taifa moja hadi lingine.
   3.   Tafsiri kama mbinu ya kujifunza lugha
Mazoezi ya kutafsiri humfanya mfasiri apekuwe kwa undani na umakini zaidi vipengele anuwai vya kiisimu vya lugha. Kadiri mfasiri anavyofanya kazi ya kufasiri ndivyo anavyokomaza umahiri wake katika lugha na hatimaye hujikuta mwenye umakini mkubwa katika lugha husika.
   4.   Tafsiri kama kiliwazo cha mfasiri
Nafsi ya mfasiri huliwazika na kufurahi kadiri anavyotatua matatizo ya kutafsiri na hasa anapopata visawe muafaka katika lugha lengwa. Ugumu wa kazi hii unapotatuliwa huwa ndio furaha ya mfasiri na chachu ya kuendelea kufasiri kazi nyingine nyingi zaidi.
UAINISHAJI WA MATINI ZA TAFSIRI
Matini za tafsiri zinaweza kuainishwa katika makundi kadhaa:
1. Matini kufuatana na dhanna ya lugha:
Hapa tunapata aina tatu za matini ambazo ni:
(a) Matini elezi:
Hizi ni matini ambazo mwandishi wake hutumia lugha kuelezea hisia zake bila kujali maelezo hayo yatapokelewaje na hadhira.
Mifano ya matini elezi ni kama vile:
v Fasihi iliyobuniwa kwa makini
v Hotuba na nyaraka za viongozi na watu wenye mamlaka
v Wasifu binafsi, insha, mawasiliano binafsi baina ya watu na hasa yanayohusu hisia za mwandishi binafsi bila kujali wasomaji lengwa.
(b) Matini arifu:
Hizi ni matini zinazohusu mada yoyote ile yenye maarifa kwa mfano sayansi, teknolojia, biashara na uchumi. Matini hizi huwa katika maumbo sanifu kama vitabu, ripoti, makala katika magazeti au majarida ya kitaaluma.
Matini arifu zina sifa kuu mbili. Sifa ya kwanza ni kwamba ndizo matini zinazofasiriwa na idadi kubwa ya wafasiri walioajiriwa katika mashirika ya kimataifa, kampuni kubwa za binafsi na asasi nyingine za tafsiri, pili asilimia kubwa ya matini hizi huwa zimekosewa sana hivyo, ni jukumu la mfasiri kufanya masahihisho yanayohitajika ili kufanya kazi iwe na ubora zaidi.

(c) Matini amili:
Matini hizi hulenga kuibua hisia za msomaji na kumfanya afikiri au atende kwa namna ambayo imekusudiwa na mwandishi wa matini. Mifano ya matini amili ni kama vile:
v Matangazo
v Propaganda
v Maombi
v Mialiko
v Fasihi pendwa, n.k
Mambo muhimu kuhusu matini amili ni pamoja na:
     ·      Kuonesha uhusiano baina ya mwandishi na hadhira
  Mfano:
-       Mheshimiwa waziri,
-       Kwa heshima na taadhima,
-       Wako mtiifu, n.k
      ·      Matini amili lazima ziandikwe kwa lugha inayoeleweka kwa hadhira mara moja ili ujumbe uliomo ueleweke kwa urahisi na hadhira itekeleze kwa urahisi na kama inavyotarajiwa na mwandishi.

Hata hivyo, kuna matini chache sana ambazo zimejipambanua kuwa ni elezi, arifu au amili. Matini nyingi huwa na mchanganyiko wa sifa zote huku sifa moja ikijitokeza zaidi ya nyingine.
2. Uainishaji wa matini kufuatana na istilahi
Uainishaji huu huwezesha kubaini kama matini ni ya kiufundi, nusu kiufundi au isiyo ya kiufundi.


3. Uainishaji wa matini kufuatana na mada
Hii husaidia kubaini kama matini ni ya kitaaluma, kidini, kisiasa, n.k
MBINU/NJIA  ZA  TAFSIRI
Katika kufasiri matini kuna mbinu kadhaa zinazotumiwa ili kufanikisha zoezi hili. Wataalamu wamejaribu kuainisha mbinu mbalimbali za kufasiri. Mwansoko na wenzake (1996:24-29) ametoa mbinu nne zinazoonekana kuwa kuu.
(a)Tafsiri ya neno kwa neno (word to word Translation)
Mbinu hii humaanisha kutafsiri maneno yakiwa peke yake (pwekepweke) kwa kufuata maana ya msingi ya lugha chanzi na kutokujali muktadha wa lugha lengwa. Kila neno na kila mofimu hufasiriwa. Msingi wa tafsiri hii ni matini chanzi au tuseme mpangilio wake ni sawa na ule wa matini chanzi. Mbinu hii inatumika zaidi katika uchambuzi wa miundo na maumbo ya maneno katika lugha.
Mfano:
Kiswahili:              A       -     na      -  lima
Kiingereza:          He/she – present –  dig

Kiswahili:            Tu  -      na     -  soma -  kitabu
Kiingereza:          We -  present -  read -   book

Kiswahili:       Wa      -   ta       -  enda  -  mlima     -  ni
Kiingereza:     They   -  future  -  go  -  hill/mount  -  at  
UBORA NA UDHAIFU
Mbinu hii inasaidia kutoa taarifa fulani za lugha lengwa. Kwa upande mwingine mbinu hii inaweza kupotosha maana. Haitoi maana kwa uangavu sana. Mfano, kwa mbinu hii tamathali za semi zinatafsiriwa kisisisi. Kwa ujumla mbinu hii si madhubuti.
(b)  Tafsiri sisisi (Direct Translation)
Hii ni tafsiri ambayo maneno hufasiriwa kwa maana zake za msingi katika matini ya lugha asilia lakini kwa kufuata sarufi ya lugha lengwa.
Mfano:
Kiswahili: Dora, huyu ni mama yangu na huyu ni mjomba wangu
Kiingereza: Dora, this is my mother and this is my uncle.

Kiswahili: Huniwezi
Kiingereza: You can’t me (maana haikubaliki)

Kiswahili: Nimekupata
Kiingereza: I have got you

Kiswahili: Tunapanda mbegu
Kiingereza: We are climbing seeds

Kiswahili: Mimi ni moto wa kuotea mbali
Kiingereza: I am the fire of dreaming  far (maana haikubaliki)

UBORA NA UDHAIFU
Mbinu hii inabainisha mahusiano ya wazungumzaji. Kwa kuangalia tafsiri zinazotokana na mbinu hii tunaweza kujua kuwa wazungumzaji wanahusiana kwa namna fulani. Kwa upande mwingine mbinu hii inapotosha maana. Haikubaliki kwa sababu haifuati muktadha sanifu. Zaidi ya hayo, njia hii haifanyi kazi katika kutafsiri matini za kifasihi. Kwa mfano.
Kiswahili: Mashoto ana mkono mrefu (yaani mwizi)
Kiingereza: Mashoto has a long hand (badala ya Mashoto is a thief)

(c) Tafsiri ya kisemantiki (Semantic Translation)
Hii ni tafsiri ambayo huzingatia maana iliyotolewa na mwandishi wa lugha chanzi na hairuhusiwi kufanya marekebisho katika lugha chanzi ili kukidhi matakwa ya lugha lengwa. Mfasiri anatakiwa kufasiri kila kipengele katika matini ya lugha chanzi ili kupata maana iliyokusudiwa katika lugha lengwa. Hapa mfasiri hufasiri kila neno katika sentensi kama lilivyo katika lugha chanzi lakini kwa kufuata sarufi ya lugha lengwa.
Mfano:

  Kiswahili:
*   Mwalimu Maeda alizaliwa mwaka 1980
*   Alianza shule ya msingi mwaka 1987
*   Alimaliza shule ya msingi mwaka 1993 na kujiunga na shule ya sekondari Manyara 1994
*   Hivi sasa yeye ni mwalimu wa shule ya sekondari Mbezi Beach
  Kiingereza
*   Maeda the teacher was born in 1980
*   He started his primary school in 1987
*   He completed his primary school education in 1993 and joined Manyara secondary School in 1994
*   Currently, he is a teacher at Mbezi Beach High School.
UBORA WA MBINU HII
Ubora wa mbinu hii ya tafsiri ya kisemantiki ni ile hali ya kuwa na uwezo mkubwa wa kuendeleza lugha lengwa kwa kuingiza miundo na misemo toka lugha chanzi.
Mfano:
Kiingereza                                 Kiswahili
Goodmorning                              Asubuhi njema
Yours truly                                  Wako mkweli
How are things at home?             Habari za nyumbani?
It leads to                                    Inapelekea

Mbali na kuendeleza lugha, mbinu hii ya kisemantiki husaidia kunukuu maneno ya mtu mwingine kwani kila neno linatakiwa litafsiriwe jinsi lilivyo bila kupoteza hata kipengele kimoja. Tena tafsiri hii haipotoshi maana au umbo la matini ya lugha chanzi katika matini ya lugha lengwa.

UDHAIFU WA MBINU HII
Tafsiri hii ya kisemantiki haitilii maanani nahau na misemo maalumu inayohusiana na utamaduni wa lugha lengwa.
Mfano:
Kiingereza                         Kiswahili
Veronica married John       Veronica alimuoa John
Like father, like son            Kama baba, kama mwana

(d) Tafsiri ya Kimawasiliano (Communicative Translation)
Hii ni tafsiri ambayo huzingatia hadhira ya lugha lengwa kwa kumjali sana msomaji wa matini hiyo. Hii ni tafsiri huru kwa sababu mfasiri anaweza kuongeza au kupunguza maneno ya matini ya lugha chanzi wakati wa kufasiri ilimradi tu ujumbe uwafikie walengwa kwa namna inayotakiwa bila kupoteza wazo la matini ya lugha chanzi. Mfasiri anao uhuru wa kutafuta maneno au vifungu vya maneno yanayolingana na nahau, methali, mila na desturi na mazingira ya lugha lengwa kwa kuzingatia mwelekeo wake wa kiutamaduni, kihistoria na kimazingira kwa hadhira lengwa.
Mfano:
Kiingereza                          Kiswahili
Veronica married Chris       Chris alimuoa Veronica
                                           Veronica aliolewa na Chris
Pia, katika tafsiri ya kimawasiliano hadhira lengwa huelewa kwa urahisi tafsiri ya kimawasiliano kwa sababu ni rahisi kuhusisha kila kisemwacho na hali halisi katika mazingira yao.

Vilevile, tafsiri hii huweza kuboresha au kusahihisha kifikiriwacho kuwa kilipotoshwa na matini ya lugha chanzi ili kiweze kueleweka vizuri katika matini ya lugha lengwa. Wakati mwingine tafsiri ya kimawasiliano huweza kubadilika kulingana na mabadiliko ya kihistoria, kiitikadi na kimazingira.
Hata hivyo, tafsiri ya kimawasiliano ina udhaifu wa kutokuwa na uwezo wa kuendeleza na kuingiza miundo au misemo kutoka lugha asilia kwenda lugha lengwa. Hali hii inatokana na ukweli kuwa tafsiri hii haizingatii miundo, misemo, na umahiri wa lugha asilia wakati wa kufasiri bali huzingatia wazo la jumla la kiutamaduni kwa lugha lengwa.

Vilevile, udhaifu mwingine katika tafsiri ya kimawasiliano hujitokeza pale mfasiri anapoegemea sana kwenye mawazo, historia, utamaduni, mazingira na itikadi ya lugha lengwa. Kwa mfano katika mwaka 2002 vyombo vya habari vilisikika vikitangaza.
*   His excellency president Sadam Hussein (vyombo vya Iraq)
*   Gaidi Sadam Hussein (vymbo vya habari vya Marekani)

MCHAKATO WA TAFSIRI
Mfasiri anapaswa kwanza kuainisha matini kabla ya kuanza hatua ya maandalizi. Kuainisha matini ni kitendo cha kuzigawa matini katika aina mbalimbali kutokana na mahitaji yanayotofautiana ya kifasiri kwa kila aina ya matini. Uainishaji wa matini hujikita katika mikabala mitatu ambayo ni Uainishaji wa matini kufuatana na istilahi, mada na kufuatana na dhima ya lugha.

Baada ya kuainisha matini, mfasiri hufanya shughuli ya uchambuzi wa matini kwa mtazamo wa tafsiri lengwa kwa kuzingatia usomaji wa matini nzima, kubaini lengo na mtindo wa matini chanzi. Uchambuzi wa matini ukikamilika, kazi inayofuata ni kuifasiri matini chanzi. Mchakato wa kufasiri ni kipengele muhimu katika tafsiri ambao hufuata hatua saba zifuatazo.


1.   Maandalizi
Katika hatua hii, mfasiri huhitaji kufahamu vizuri maudhui ya matini ya lugha chanzi. Mfasiri huisoma matini nzima ya lugha chanzi ili kubaini ujumbe wake, mtindo wake na kuziwekea alama maalumu sehemu zenye utata au ugumu. Pia mfasiri hubaini usuli wa matini ili kupata taarifa za mwandishi, malengo yake, utamaduni wa mwandishi na wasomaji (hadhira) wa matini chanzi. Vilevile mfasiri huzingatia sifa za kiisimu za matini chanzi na kuandika katika kijitabu maalumu msamiati na istilahi muhimu na maneno ya kiutamaduni.
2.    Uchambuzi
Katika hatua hii, mfasiri huchunguza kwa makini maneno pamoja na maelezo muhimu ya matini chanzi yaliyoandikwa katika hatua ya maandalizi. Zoezi hili hufanywa kwa kutumia marejeleo mbalimbali kama vile kamusi, orodha za msamiati na istilahi mpya.
3.   Uhawilishaji
Katika hatua hii, mfasiri huhawilisha mawazo, maana na ujumbe kutoka kwenye matini chanzi kwenda kwenye matini lengwa. Mfasiri anaweza kufanya uamuzi juu ya dhanna za kisarufi zinazoweza kutumiwa kwenye matini lengwa kuelezea maana za matini chanzi kwa wepesi na ubora unaotakiwa.
4.   Rasimu ya kwanza
Shughuli ya uhawilishaji huzaa rasimu ya kwanza ambayo ni matini mpya katika lugha lengwa. Mfasiri hupata nafasi ya kwanza ya kufanya marekebisho kwa kuzingatia umbo la matini lengwa kila inapowezekana. Vilevile, mfasiri anashauriwa muda wote afikirie juu ya hadhira anayoilenga pamoja na lengo la matini chanzi.
5.   Udurusu wa rasimu ya kwanza
Hatua hii hutoa nafasi ya kwanza ya kusahihisha matini iliyokwisha tafsiriwa. Mfasiri anashauriwa asome rasimu nzima ya tafsiri kwa sauti ili aweze kufanya yafuatayo:
-       Kusahihisha makosa ya kisarufi na kimuundo ya tungo mbalimbali
-       Kunyoosha sehemu zenye tafsiri ya mzunguko na matumizi ya sinonimia zisizo za lazima
-       Kuona kuwa maana zilizohawilishwa kwenye matini lengwa ni sahihi ukilinganisha na zile za matini chanzi
-       Kubaini iwapo mada au ujumbe mkuu wa matini unajitokeza waziwazi katika tafsiri

6.   Kusomwa kwa rasimu ya kwanza na mtu mwingine
Katika hatua hii, mfasiri humpatia mtu mwingine ambaye huisoma na kuona kama inaeleweka na ina mtiririko mzuri wa mawazo ili isomeke kama tafsiri pale inapowezekana. Dhima kuu ya msomaji wa pili ni kuona kama tafsiri iko sahihi, inaeleweka na ina mtiririko mzuri unaokubalika. Pia msomaji wa pili huweza kutoa mapendekezo juu ya marekebisho yanayohitajika kufanywa baada ya kubaini udhaifu wa tafsiri aliyoisoma.
7.   Usawidi wa rasimu ya mwisho
Hatua hii ndiyo hatua ya mwisho katika mchakato wa tafsiri ambao hufanyika baada ya mfasiri kupata maoni ya msomaji wa pili. Hapa mfasiri huyatumia mapendekezo na maelekezo ya msomaji wa pili ili kuisahihisha tena tafsiri yake na hatimaye kutoa rasimu ya mwisho ya tafsiri.

         UMUHIMU WA MCHAKATO WA TAFSIRI
*   Husaidia mfasiri kufanya maandalizi yote muhimu ya tafsiri yanayohitajika na hivyo kupata maana sahihi ya istilahi mbalimbali.
*   Husaidia mfasiri kutoa tafsiri sahihi ya matini chanzi kwenda katika matini lengwa.
*   Huwafanya walengwa kuelewa ujumbe uliomo katika matini chanzi kwani mfasiri hufasiri kwa kuzingatia mazingira na utamaduni wa hadhira lengwa.
*   Hufanya kazi ya tafsiri kuepuka makosa madogomadogo ya kimaana na kimuundo katika matini lengwa.
*   Hurahisisha kazi ya kutafsiri na kuifanya kuwa nyepesi zaidi na isiyochosha.
TOFAUTI KATIKA TAFSIRI
Swali: “Inadaiwa kuwa mfasiri ni msaliti kwani hawezi kukwepa kusaliti matini asilia au matini lengwa.” Jadili.

Kwa mujibu wa kamusi ya Kiswahili sanifu ya TUKI toleo la pili la 2004, Msaliti ni mtu anayeshirikiana na maadui wa nchi yake, mtu anayefanya vitendo viovu dhidi ya nchi yake, haini, mtu anayechonganisha ndugu au majirani ili wakosane.
Kutokana na fasili ya kamusi juu ya msaliti tunaweza kusema kuwa, msaliti wa kazi ya tafsiri ni mtu anayekiuka kanuni, sheria na taratibu za matini chanzi au matini lengwa kwa ajili ya kunufaisha au kukomoa hadhira lengwa.
Usaliti wa mfasiri unasababishwa na kuegemea upande mmoja kutokana na upungufu katika tafsiri. Kwa hakika hakuna matini lengwa iliyo sawa kabisa na matini chanzi.
Tofauti za kiisimu, kiutamaduni, kihistoria na kimazingira baina ya lugha katika matini asilia na matini lengwa hufanya iwe vigumu kutafsiri mawazo ya lugha moja katika lugha ingine kwa kiwango sawa.
Baadhi ya mambo ambayo husababisha usaliti katika tafsiri ni pamoja na tofauti za kiisimu, kifasihi, kiitikadi, kimtindo, misemo, vitendawili, nahau, mazingira na mila.
    1.   Tofauti za kiisimu
Tofauti za maumbo, miundo na maana kati ya lugha ya Kiswahili na lugha za Ulaya husababisha tafsiri kuwa na upungufu. Maumbo ya Kiingereza kwa mfano huruhusu kauli nyingine elekezi kutoonesha umoja na wingi wa wahusika. Mfano huu wa maumbo huwezesha kutoa tafsiri pana zaidi. Kauli hizi zinapotafsiriwa katika matini lengwa, mathalan Kiswahili hulazimu kubainisha vipengele vyote.
Mfano:
Kiingereza                                 Kiswahili
No entrance                                Usiingie ndani
Quiet please                                Usipige kelele
No smoking                                 Usivute sigara
Kutokana na mifano hiyo ni kwamba tafsiri ya Kiswahili hujibana zaidi. Ukisema Usipige kelele inamaana wewe na sio mimi au yeye. Kwa upande wa miundo kuna baadhi ya wafasiri huhawilisha ruwaza za sintaksia ya Kiingereza katika Kiswahili na hivyo kufanya tafsiri zao kuwa na mushikeri.
Kwa mfano:
Kiingereza                         Kiswahili
Nine thousand                    Tisa elfu
Five million                        Tano milioni
Kwa upande wa maana, maneno mengine katika Kiingereza hayaakisi ipasavyo katika tafsiri za Kiswahili.
Kwa mfano:
Kiingereza                                 Kiswahili
Intensive care unit (ICU)             Chumba cha wagonjwa mahututi     

Katika maana hiyo hakuna sehemu katika Kiingereza inayotaja mahututi.
   2.   Tofauti za kifasihi
Taarifa zilizomo katika fasihi huangaliwa kisanii na hivyo huhitaji wasomaji wafanye bidii katika uchambuzi ili wapate maudhui ya fasihi ihusikayo. Kwa mfano; Ndulute (1994) anasema kuwa kutafsiri mashairi ya Shaaban Robert ni kitu kinachovutia lakini pia ni cha hatari kutokana na mawazo yake mazito na ya kina, pia falsafa yake na usanii wake kwa ujumla; mfano katika shairi la Ua mfasiri anaweza kujiuliza je, Ua linalozungumziwa hapa ni lipi? Ua la mmea, penzi au mauaji. Je, mfasiri atatoa fasiri ipi kwa lugha lengwa pasipo kupoteza maana wala kusaliti lugha chanzi.
    3.   Tofauti za Kiitikadi na Kihisia
Katika tafsiri nyingi za vitabu na magazeti itikadi na hisia za wafasiri zinaweza kuathiri matokeo ya tafsiri zao.
Kwa mfano:
         Kiingereza                         Kiswahili
         Merchants of Venice          Mabepari wa Venisi

Katika jina la kitabu hicho, Nyerere alitafsiri Merchantskama mabepari badala ya wafanyabiashara ambayo ndiyo tafsiri sahihi zaidi ya Merchants. Hii inamfanya Nyerere aseme hivyo kwa sababu ya itikadi na hisia alizonazo kuwa wafanyabiashara ni mabepari hivyo ni wanyonyaji.
     4.   Tofauti za Mtindo
Mara nyingi inakuwa vigumu kueleza dhanna na taarifa kwa kufuata mtindo unaotakiwa katika uwanja huo. Hii ni kwa sababu, Kiswahili kama zilivyo lugha nyingine za kiafrika hazijawa na tofauti dhahiri za mtindo.
Kwa mfano:
         Kiingereza                                 Kiswahili
         Lend me your ears                       Naomba mnisikilize
         May I have your attention           Naomba mnisikilize   
Tafsiri ya Kiingereza inaonekana kuwa pana zaidi kuliko ya Kiswahili, yaani kuna namna zaidi ya moja ya kuulizia jambo moja.
    5.   Tofauti za Mazingira na Mila
Kwa kawaida mazingira, mila na desturi kati ya watumiaji wa lugha asilia na wale wa lugha lengwa mara nyingi hufanya tafsiri kuwa ngumu. Kwa mfano maneno karibu tena yanapotumiwa na mswahili  anapomuaga mgeni wake hayana maana ya moja kwa moja na yale ya Kiingereza welcome again bali humaanisha goodbye.
     6.   Tofauti za Misemo, Vitendawili, Methali na Nahau
Maneno haya huendana na utamaduni wa watu fulani unaotofautiana kutoka jamii moja na nyingine.
      Mfano:
-       funga virago, enda joshi (nahau),
-       mwenda pole hajikwai (methali),
-       popo mbili zavuka mto (kitendawili),
-       kata shingo, kula kichwa (misemo).
Kwa kuwa vitendawili, nahau, methali na misemo huendana na utamaduni wa watu fulani, hivyo tafsiri ya maneno kama hayo huweza kukumbwa na matatizo kama vile; kutopatikana kwa visawe vya kimuundo vya mafungu kama hayo katika lugha lengwa.
Tatizolingine ni upatikanaji wa visawe mwafaka vya dhanna na maana zake katika lugha lengwa.
Wafasiri wamekuwa wakijiuliza kama kweli misemo na tungo za namna hiyo zinaweza kufasirika inavyopaswa. Misemo ya Kiingereza kwenda Kiswahili inaleta utata sana katika kufasiri iwapo mfasiri hajui mazingira ya lugha asilia.
   Kwa mfano:
         Kiingereza                         Kiswahili
         A hot debate                       Mjadala wa moto
                                                   Mjadala mzito
                                                   Mjadala mkali
         UMUHIMU WA TAFSIRI KATIKA JAMII
Maendeleo ya jamii yoyote ile kiutamaduni, kisiasa na kiuchumi hutegemea sana maendeleo ya sayansi na teknolojia ndani ya jamii husika. Sayansi na teknolojia ni uwanja wowote ule unaohusu mada za kimaarifa na kiufundi. Sayansi na teknolojia inahusu suala la elimu katika uhandisi, tiba, elektroniki, sayansi ya nyukilia na kadhalika.
Kazi ya tafsiri ndio msingi mkuu katika jamii kupata maendeleo katika suala la mawasiliano juu ya masuala yanayohusu siasa, uchumi na utamaduni. Katika karne hii ya sayansi na teknolojia ambapo dunia inaungana na kuonekana sawa na kijiji kwa sababu ya utandawazi. Kwa hiyo tafsiri ya istilahi mbalimbali hasa zile za kisayansi ni muhimu sana kwa maendeleo ya jamii ya sasa kwa sababu hurahisisha suala la mawasiliano katika pande zote.
Mfasiri wa istilahi hasa za kisayansi hana budi kuwa makini sana anapotafsiri istilahi zinazohusika. Kwa kawaida tafsiri ya istilahi za sayansi na teknolojia zina lengo moja kuu ambalo ni kutoa ujumbe toka lugha asilia na kuupeleka katika lugha lengwa kwa kutumia lugha ya kiulimwengu ambayo haifungamani na utamaduni wa jamii fulani. Kwa hiyo mambo yafuatayo yanafaa kuzingatiwa katika tafsiri mbalimbali hasa zile za kisayansi.
Kwanza, istilahi sharti ziwe toshelevu yaani ziakisi vilivyo sifa za dhanna zinazowakilishwa. Pili, istilahi sharti zifuate mfumo wa kisarufi wa lugha lengwa. Tatu, istilahi sharti ziwe fupi na zenye kueleweka na Nne, istilahi hasa za kisayansi yafaa ziwakilishe maana moja tu na pale inapowezekana zisiwe na sinonimia.
Mambo yote manne yaliyotajwa hapo juu yakitekelezeka, tafsiri hutoa au huzaa matunda mema kwa jamii husika katika nyanja za kisiasa, kiutamaduni na kiuchumi katika ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia. Zifuatazo ni baadhi ya faida za tafsiri kwa jamii lengwa.
   1.   Kwanza, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii husika kwa sababu husaidia kimatumizi katika istilahi za lugha ya kufundishia kwa mfano lugha ya Kiingereza ambayo hutumika katika suala la kufundishia sehemu mbalimbali duniani imetafsiri lugha mbalimbali kama vile Kigiriki na Kilatini.
Mfano:
                 Kigiriki            Kiingereza
                 Physics              Physics
                 Khemia              Chemistry
                
                 Kilatini             Kiingereza
                 Moles                Molecule
Katika mfano huo, lugha asilia ya maneno ya Kiingereza Physics na Chemistry ni Kigiriki ambapo neno molecule lugha asilia ni Kilatini. Pia katika lugha ya Kiswahili istilahi Fizikia, Kemia na molekiulini maneno (istilahi) yaliyotafsiriwa kutoka lugha ya Kiingereza. Wanafunzi, walimu, wahadhiri na jamii kwa ujumla wamefaidika na wanaendelea kufaidika na matumizi ya istilahi hizo za kisayansi kwa sababu ya kazi nzuri ya tafsiri.
    2.   Pili, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii lengwa kwa sababu husaidia kutafsiri istilahi mbalimbali za kimaarifa au kiufundi kutoka lugha  asilia yaani lugha ambayo haieleweki sana kwa jamii nyingine inayotumia lugha lengwa na kuweza kueleweka na kutumiwa na wengi kama siyo wote katika lugha lengwa kwa sababu ya kazi nzuri ya tafsiri.
Kwa mfano:
                 Kiingereza                Kiswahili
                 Asprin                        Aspirini
                 Tyre                           Tairi
                 Globalization             Utandawazi
                 E-mail                        Barua pepe
                 Fax                             Namba nukushi
    3.   Tatu, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii husika kwa sababu husaidia katika kubuni au kuunda majina ya biashara katika lugha ya Kiswahili ambapo maneno ya kigeni hupatiwa maumbo ya Kiswahili.
Kwa mfano:
-       Sabuni chapa FOMA (kutokana na “foam”)
-       Sabuni chapa KODROI (kutokana na “Corduroy”)
-       Kileo chapa KONYAGI (kutokana na “Cognac”)
   4.   Nne, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii lengwa kwa sababu husaidia lugha lengwa ambayo hutumiwa na wengi ili kujitosheleza katika istilahi mbalimbali. Kiswahili ni mfano mzuri wa lugha lengwa ya namna hiyo kwa sababu Kiswahili ni lugha iliyosheheni istilahi ambazo chimbuko lake ni lugha mbalimbali.
  Kwa mfano:
Neno la Kiswahili                      Chimbuko lake/Lugha
Shati                                           Kiingereza
Shamba                                       Kifaransa
Nanasi                                         Kireno
Shehe                                          Kiarabu    
  5. Tano, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii husika kwa kurahisisha na kuchapusha mawasiliano ya kitaaluma kwa waandishi wa vitabu vya kitaaluma, walimu, wahadhiri na wanafunzi. Pia hurahisisha mawasiliano katika makongamano ya kawaida na makongamano ya kimataifa kuhusu maendeleo ya jamii kisiasa, kiutamaduni na kiuchumi; vilevile kazi ya tafsiri ni muhimu sana katika mihadhara ya kidini inayoendeshwa kimataifa katika nchi mbalimbali. Hapa suala la ukalimani hutiliwa maanani zaidi ili kurahisisha mawasiliano.
   6. Sita, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii lengwa kwa sababu vitabu mbalimbali vinavyosomwa na watu wa matabaka yote katika jamii watu wazima, watoto, n.k. huweza kueleweka kwa wote kwa sababu ya kazi nzuri ya tafsiri. Kwa mfano Bibliatakatifu ni kitabu ambacho kimetafsiriwa katika lugha mbalimbali kwa sababu kinasomwa na watu wa tabaka zote katika jamii karibu duniani kote.
    7. Saba, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii husika hasa karne hii ya sayansi na teknolojia kwa sababu huwa katika mfumo wa kidhanna na huwakilisha dhanna moja tu pale inapowezekana.
Kwa mfano:
         Kiingereza                         Kiswahili
         Machine                             Mashine
         Prove                                  Thibitisha
         Protestant                           Mprotestanti (Muasi)
   8. Nane, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii lengwa kwa sababu husaidia istilahi za kisayansi na kiteknolojia kutoka lugha asilia kuwa sahihi, kwa kuandikwa na kutamkwa kwa urahisi katika lugha lengwa.
Kwa mfano:
         Kiingereza                Kiswahili
         Radio                         Redio
         Television                  Televisheni
         Computer                   Kompyuta
    9.  Tisa, kazi ya tafsiri ni muhimu kwa jamii husika kwa sababu husaidia uhai wa lugha, yaani kubadilika kimsamiati/istilahi kulingana na wakati na hasa katika kuakisi matukio mbalimbali. Mara nyingi mabadiliko au istilahi mpya hujitokeza kutokana na mambo mapya yanayoibuka katika jamii na hivyo kuleta uhai katika lugha lengwa.
Kwa mfano:
Kiingereza                Kiswahili
Stakeholders              Mwanzo – washika dau
                                           Sasa        - wadau
Globalization             Mwanzo – Udandarizi
Sasa        - utandawazi
HIV/AIDS                  Mwanzo – Juliana
                                           Sasa        - UKIMWI

Uhai wa matumizi ya maneno hayo umepata mashiko katika siku za hivi karibuni; awali ilikuwa vigumu sana kwa istilahi hizo kutumiwa katika lugha ya Kiswahili katika miaka ya mwanzoni mwa 1980 na kurudi nyuma. Istilahi ambayo ilisikika sana ilikuwa ni ukoloni mamboleo badala ya neno la sasa la utandawazi.
     10.    Kumi, kazi ya tafsiri ni muhimu sana kwa jamii husika hasa katika karne hii ya sayansi na teknolojia kwa sababu husaidia sana katika vyombo vya habari kama vile redio, televisheni na magazeti katika kufikisha ujumbe kwa walengwa wote. Redio, televisheni na magazeti ni vyombo vya habari vitumikavyo kutolea taarifa hasa zilizo mpya kwa sababu huhusiana na uvumbuzi mpya wa kisayansi na kiteknolojia. Mara nyingi vyombo hivi hupata taarifa zake nyingi kutoka Mashirika ya habari ya kigeni kama vile REUTERS, CNN, SKYNET, n.k ambapo taarifa zake huwa katika lugha za kigeni kama vile Kiingereza, kwa hiyo vyombo vya habari hulazimika kuzitafsiri taarifa husika kabla ya kuzitangaza au kuzichapisha.

Kwa ujumla kazi ya tafsiri ni kazi muhimu sana kwa jamii yoyote ile hasa katika karne hii ya sayansi na teknolojia. Kwa hiyo, mfasiri anapaswa kujua taaluma ya somo ambamo istilahi zinatoka kwa sababu ni mtu anayeshirikisha watumiaji wote wa lugha katika uvumbuzi wa matumizi ya lugha lengwa. Vilevile, tafsiri ni fani kamili yenye kuhitaji ujuzi, ustadi na uwezo maalumu wa lugha mbili au zaidi ambazo mfasiri atazitumia katika kazi yake ya kufasiri.

Mwisho, kwa kuwa lugha ya Kiswahili matumizi yake yanapanuka kwa haraka sana tafsiri ya istilahi inapaswa kuwa kazi ya kudumu inayohitaji mpango maalumu wa utekelezaji ikiwa ni pamoja na kufanya kazi hiyo.

Hasara za Tafsiri katika Utamaduni.
Baada ya kuelezea faida mbali mbali za tafsiri katika utamaduni wa Tanzania na Afrika kwa jumla. Zifuatazo ni hasara za tafsiri kwa jamii.
Ø Tafsiri imesababisha jamii za waafrika kuiga utamaduni wa mataifa ya nje.
Kwa mujibu wa Kamati ya Taarifa za Tovuti Kuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania zilizofanyiwa marekebisho mwaka (2015) zinaeleza kuwa: “Utamaduni wa Tanzania ni matokeo ya athari za kiafrika, kiarabu, kizungu na kihindi. Maadili, mila na desturi za kiafrika zinabadilishwa polepole na maisha ya kisasa, ingawa kwa kasi ndogo sana miongoni mwa jamii ya wamasai”. Kutokana na maelezo hayo ni wazi kuwa, jamii nyingi za waafrika zikiwemo za watanzania, zimeanza kuathirika kwa kuiga mila na tamaduni za kimagharibi kupitia tafsiri za kazi mbali mbali za kijamii na mpaka sasa hali hiyo inaendelea kupitia njia nyengine mbali mbali kama vile utalii na maingiliano baina ya waafrika, wazungu, waarabu na wahindi.
Ø Tafsiri imesababisha mivutano na makundi ya kidini kati ya jamii za waafrika.
Ukirudia historia ya tafsiri katika nchi za ulaya, utaona, mnamo karne ya 16 kulikuwa na    muamko mkubwa wa kidini ambao ulianzia Ujerumani na kusambaa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni. Mwamko huu ulipinga muundo, mwelekeo, falsafa na mafunzo mengi ya kanisa katoliki ya wakati huo na matumizi ya lugha moja ya kilatini katika misa na mafunzo ya kidini. Hali hii ilisababisha mgawanyiko katika dini ya kikiristo. Watu mbali mbali walitafsiri maandiko matakatifu katika lugha mbali mbali. Kwa mfano Martin Luther King alitafsiri Biblia takatifu kutoka kilatini kwenda lugha ya Kiingereza (1611) ikaitwa “The King James Bible”, pia alitafsiri Biblia kutoka Kilatini kwenda lugh ya Kijerumani. Baada ya kuona tafsiri ya Kilatini imeacha baadhi ya vipengele katika maandiko hayo matakatifu, Jarome alitafsiri Biblia ya Kigiriki na Kiebrania kutoka lugha ya Kilatini.
Kutokana na maelezo hayo ni wazi kuwa, mgawanyiko wa kidini haukuishia katika nchi za ulaya na katika dini ya kikristo peke yake bali ulienea ulimwengu mzima zikiwemo nchi za afrika kwa sababu ya kutafsiriwa maandiko matukufu mbalimbali kama vile biblia, kur-an na vitabu vyingine vya mafunzo ya dini . Sasa hivi ukichunguza katika dini zote hasa za uislamu na ukristo utakuta mivutano kati ya waumini juu ya makundi yao. Kwa mfano katika ukristo utakuta makundi kama vile wakatoliki, wasabato na kadhalika. Ama kwa upande wa dini ya kiislamu kuna makundi kama vile suni, ibadhi, shia na kadhalika. Yote hayo yametokana na kufasiriwa kwa maandiko ya dini na ufahamu wa waumini katika maandiko hayo.
Ø Baadhi ya njia za tafsiri husababisha kwenda kinyume na sarufi ya lugha lengwa au utamaduni wa lugha lengwa.
Hoja hii anajiegemeza zaidi katika aina za tafsiri ambazo ni tafsiri ya neno kwa neno, tafsiri sisisi, tafsiri ya kisemantiki na tafsiri ya mawasiliano. Lakini hapa tuangalie zaidi tafsiri ya neno kwa neno. Mara nyingi tunapotafsiri sentensi au matini kwa kutumia njia hii, lazima tufuate sarufi ya lugha chanzi hivyo husababisha  makosa ya kimuundo na kimaana ya lugha lengwa. Mifano ifuatayo inafafanua zaidi.
        Kiingereza          kwenda             Kiswahili:
I / like / banana / s / more / than / orange / s /
Mimi / penda/kama / ndizi / wingi / zaidi / kuliko / chungwa / wingi /
Kiswahili   kwenda   Kiingereza
Wa / toto / wa / dogo / wa / na / imba / kwa / furaha /
Plural / child / plural / small / they / present continues tense (singular) / by/for / happiness
Unapochunguza mifano ya hapo juu, utakuta kuwa ufuataji wa sarufi ya lugha chanzi husababisha kuharibu sarufi ya lugha lengwa na kupoteza maana inayokusudiwa kutoka lugha chanzi.Vile vile tunapotafsiri methali, misemo, nahau na matini nyingine za kifasihi, kwa kutumia njia yoyote ya tafsiri, mfasiri anaweza kwenda kinyume na utamaduni wa lugha lengwa endapo atakuwa si mzoefu wa utamaduni wa jamii hiyo.
Ø Tafsiri husababisha matumizi mabaya ya lugha ya Kiswahili katika maandishi.
Moja ya njia ya uchanganyaji wa lugha katika maandishi ni tafsiri. Watu wengi wanaojishughulisha na kutafsiri matini mbalimbali kwenda lugha ya Kiswahili huathiriwa na kazi hiyo na kuwasababishia kuchanganya lugha pale wanapoandika kazi nyingine za Kiswahili jambo ambalo ni kinyume na utamaduni wa mtanzania. Jambo hili huweza kujitokeza kwa waandishi wa makala mbalimbali za Kiswahili lakini pia wahariri wa magazeti.   
     Hapa nataka nifahamike kuwa, sipingi utumiaji wa neno au maneno ya lugha nyingine kama Kiingereza ambayo yana lengo la kutoa ufafanuzi zaidi juu ya jambo fulani ambapo mara nyingi maneno hayo huwekwa katika mabano. Bali nakusudia uchanganyaji wa lugha kwa ujumla. Mfano katika upekuaji wa makala mbalimbali nimegundua matumizi hayo kama ifuatavyo:-        
“Mimi ninadhani values za jamii ni kioo ambacho maendeleo yoyote that we want  and to find out kwa udi na uvumba lazima ya reflect, kama we have not values za       maana ni vipi tutaendelea”
Kwa hiyo mtu anayetumia lugha kama inavyoonekana katika maelezo yaliyopo hapo juu, mimi kwa maoni yangu naona mtu huyo ameathiriwa na lugha ya Kiingereza au kutokana na kufanya kazi nyingi za tafsiri.

Kukalimani

Kutokana na fasili ya TUKI, tunaweza kusema kuwa kukalimani ni kuhawilisha mawazo moja kwa moja kutoka lugha moja ya mazungumzo kwenda lugha ingine ya mazungumzo bila kupoteza, kupotosha au kubadili maana. Mtu anaweza kukalimani mazungumzo ya Kiingereza au Kifaransa kwenda Kiswahili. Shughuli ya kukalimani inasaidia kuunganisha na kujenga uhusiano mwema kati ya tamaduni mbili au zaidi kwa njia ya mazungumzo toka lugha moja hadi lugha nyingine.
Hata hivyo, wataalamu wa kukalimani sio kwamba wanafasili mazungumzo au maongezi tu kwa lugha lengwa (ya hadhira), pia hubainisha na kupambanua dhanna husika kwa mujibu wa muktadha uliopo bila kupoteza lengo la mzungumzaji wa lugha asilia (fanani). Mkalimani hupaswa kuelewa lengo mahususi la mazungumzo ili kukalimani kinachozungumzwa kwa usahihi. Inamlazimu mkalimani kuwa makini sana na tamaduni zinazohusiana sana na lugha husika.
Wataalamu wa kukalimani wanapaswa kuwa makini sana katika kuelewa kwa usahihi kile kinachozungumzwa kwenye lugha asilia na lugha lengwa ili kufafanua au kueleza wazo au dhanna kwa usahihi. Kwa kawaida, mkalimani hubadili maneno ya lugha chanzi na kuyaweka katika maana ya lugha lengwa na kisha kubadili njia ya mazungumzo. Kwa hiyo, shughuli ya kukalimani inahitaji uwezo mkubwa wa kusikia, kuelewa na kutunza kumbukumbu za kile kinachozungumzwa.
Mfano wa kukalimani:
Muuza Duka:   Karibu shangazi
Mkalimani:      welcome aunt
Mnunuzi:          Thank you. How are you?
Mkalimani:      Asante. Habari gani?
Muuza Duka:   Nzuri, nikusaidie nini?
Mkalimani:      Fine. What should I sell to you today?
Mnunuzi:          I want to buy three kilos of sugar, two packets of tea
                           Leaves, one tin of powdered milk and two litres of
                           Cooking oil. How much?
Mkalimani:      Ninataka kununua sukari kilo tatu, majani ya chai pakiti
                            mbili, maziwa ya unga kopo moja na mafuta ya
                           kupikia lita mbili. Bei gani?
Muuza Duka:   Sukari kilo tatu ni shilingi 4,500/- majani ya chai
                            mazuri ya Tanzania pakiti mbili ni shilingi 1,600/-
                            maziwa ya unga kopo la NIDO ni shilingi 4,000/= na
                            lita mbili za mafuta ya kupikia ya alizeti ni shilingi
                            7,000/- jumla ni shilingi 17,100/-
Mkalimani:      Three kilos of sugar is Tsh 4500/-, a good Tanzania
                            packets of tea leaves is Tsh 1600/-, one tin of NIDO
                            powdered milk is Tsh 4000/- and two litres of
                            sunflower cooking oil is Tsh 7000/-. The total is
                            17,100/- only.
Mnunuzi:                  Excuse me!Is there washing soap?
Mkalimani:      Samahani! Kuna sabuni ya kufulia?
Muuza Duka:   Ndiyo! Nina sabuni za miche tu. Sina sabuni za unga
Mkalimani:      Yes, I have bar soap only. I don’t have powdered soap
Mnunuzi:          How much is it?
Mkalimani:      Bei gani?
Muuza Duka:   Shilingi mia sita
Mkalimani:      Six hundred shillings
Mnunuzi:          Okay, please give me two bars. Do you have match
                           boxes?
Mkalimani:      Sawa, nipatie miche miwili. Una vibiriti?
Muuza Duka:   Ndiyo kiberiti kimoja ni sh 50/-
Mkalimani:      Yes I do. One is 50/-
Mnunuzi:          Okay, here is the money
Mkalimani:      Sawa. Hizi hapa pesa zako
Muuza Duka:   Asante sana na karibu tena
Mkalimani:      Thank you and welcome again.

MBINU ZA KUKALIMANI

Kuna mbinu mbalimbali za kukalimani. Hata hivyo wataalamu wengi wa ukalimani wameainisha mbinu kuu mbili ambazo ni Kukalimani papo kwa papo na Kukalimani kwa kufuata dhanna/wazo.
    1.   Kukalimani papo kwa papo
Kukalimani papo kwa papo ni mbinu ya kukalimani ambayo hutumika sana katika taaluma. Mbinu hii humtaka mkalimani kusikiliza na kuongea huku akionesha ishara mbalimbali kwa mujibu wa mazungumzo yanayoendelea. Mkalimani anatakiwa kuwa mwelewa na makini katika kutarajia mwisho wa sentensi ya mzungumzaji wa mada husika katika mazungumzo yanayoendelea.

Kukalimani papo kwa papo mara nyingi hutumika katika mikutano ya kimataifa, kwenye mahakama za kimataifa na katika mikutano mikubwa na midogo ya mahubiri ya kidini. Kwa mfano, wakalimani katika mikutano ya kimataifa hukaa au husimama wakiwa wamevalia vipokea sauti ambavyo hubanwa kichwani na kuongea kwa kutumia vipaza sauti vinavyoelekeza sauti zao moja kwa moja kwa walengwa.

Mkalimani hawezi kuanza tu kazi ya kukalimani kabla ya kuelewa maana ya sentensi kwa ujumla. Kwa hiyo hali hii hudhihirisha ugumu wa shughuli ya kukalimani kwa sababu mkalimani anatakiwa akalimani sentensi aliyoisikia na kuiweka katika lugha ya hadhira lengwa huku akisikiliza na kuelewa sentensi inayofuata. Haitakiwi mkalimani atumie muda mrefu kusikiliza  kisha kuongea kwa sababu akifanya hivyo atapoteza baadhi ya maneno yanayoongelewa na kupoteza maana ya mazungumzo yanayoendelea kwa wakati huo.
    2.   Kukalimani kwa kufuata dhanna au wazo
Kukalimani kwa kufuata dhanna au wazo pia ni mbinu ingine inayotumika katika shughuli ya kukalimani. Mbinu hii humtaka mkalimani kusikiliza kwa muda kisha kukalimani kwa lugha ya hadhira lengwa baada ya kupata dhanna kutokana na maelezo yaliyotolewa na mzungumzaji wa lugha asilia. Mkalimani anaweza kutulia kwa muda kati ya dakika moja hadi tano kabla ya kukalimani kilichosemwa na mzungumzaji.
Wakati mwingine mkalimani huweza kunukuu maneno machache kwenye kijidaftari ili asipoteze dhanna nzima ya mzungumzaji wa lugha asilia wakati wa kukalimani kilichosemwa na mzungumzaji. Mbinu hii haitumiwi sana na wakalimani kwa sababu mara nyingi hushindwa kutoa dhanna nzima kutokana na ukweli kwamba si rahisi kukumbuka kila neno lililotamkwa na fanani kwa hadhira lengwa.
UMUHIMU WA KAZI YA KUKALIMANI
   1.   Kazi ya kukalimani hurahisisha mawasiliano miongoni mwa jamii mbili au zaidi zenye tamaduni tofauti. Kazi hii hurahisisha na kuchepusha mawasiliano ya kawaida au ya kitaaluma. Kwa mfano kazi ya kukalimani hurahisisha mawasiliano katika makongamano ya kimataifa kuhusu maendeleo ya jamii katika nyanja za siasa, uchumi na utamaduni.
    2. Pili, kazi ya kukalimani husaidia kudumisha amani ya kisiasa na kiuchumi duniani. Watu waliofarakana huweza kukaa pamoja na kuzungumza chini ya wasuluhishi wa kimataifa. Kwa mfano nchi nyingi za kiafrika kama vile Liberia, Ethiopia, Rwanda, Burundi, Kongo-DRC, Angola, Msumbiji, Siera Leon, Chadi na Nigeria zimepata utulivu baada ya kusuluhishwa na mataifa ya nje ambayo yanatumia lugha tofauti na za nchi hizo. Ni kazi ya kukalimani ndiyo iliyosaidia kujenga maelewano ndani ya tamaduni tofauti za jamii hizo.
    3. Tatu, kazi ya kukalimani husaidia kudumisha amani ya kijamii duniani. Kwa mfano wahubiri wengi wa kimataifa huweza kupeleka ujumbe wa Mungu sehemu mbalimbali za dunia zenye lugha tofauti kupitia ukalimani. Wakalimani huweza kueleza au kufafanua juu ya maana ya mzungumzaji wa lugha asilia kwa kutumia lugha ya hadhira lengwa.
    4.  Nne, kazi ya kukalimani ni nyenzo muhimu sana ya kujifunzia lugha ya pili. Kwa mfano mtu anayetumia Kiswahili huweza kujifunza lugha ya Kiingereza kupitia kwa mkalimani. Mtu wa namna hiyo huweza kujifunza na kuelewa maana ya maneno mbalimbali, matamshi yake na matumizi yake katika lugha ya mazungumzo. Mtu anayejifunza lugha ya pili kupitia kwa mkalimani hufaidika na matumizi mbalimbali ya istilahi tofauti za lugha ya fanani kwa sababu ya kazi ya kukalimani. Hadhira lengwa huwa makini sana na kujijengea uwezo mkubwa wa kusikiliza, kusikia, kuelewa na kutunza kumbukumbu za kile kinachozungumzwa.
  5.Tano, kazi ya kukalimani husaidia hadhira lengwa kujifunza pia mawasiliano ya ishara kama fanani anatumia njia hiyo ya mawasiliano. Mkalimani huweza kufasili mawasiliano ya ishara au alama anazozitumia mzungumzaji kwa kuzungumza kwa lunga lengwa.
Sita, kazi ya kukalimani husaidia uhai wa lugha kulingana na wakati katika kuakisi mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni yaliyojitokeza katika jamii husika. Kwa mfano neno Stakeholder katika lugha ya Kiingereza, mwanzo wakalimani walilitamka kuwa ni washika dau katika lugha ya Kiswahili lakini kwa sasa neno hilo linatamkwa kama wadau katika Kiswahili. Pia neno Low class peoplekatika Kiingereza lilitamkwa kama Makabwelalakini hivi sasa ni walalahoi.


SIFA ZA MKALIMANI
Kuna sifa mbalimbali ambazo mkalimani anapaswa kuwa nazo. Hii ni kutokana na ugumu wa kazi ya kukalimani. Hata hivyo, wataalamu mbalimbali wa kazi ya kukalimani wanabainisha sifa kuu tatu kwa ajili ya mkalimani. Sifa izo ni elimu ya kutosha juu ya lugha zinazotumika. Elimu ya kutosha juu ya hadhira na uelewa wa matumizi sahihi ya mbinu za kimawasiliano.
    1.   Uelewa wa kina juu ya lugha zinazotumika
Mkalimani mzuri ni yule ambaye ana utaalamu wa kutosha katika lugha zinazotumika. Kwa mfano kama anakalimani Kiingereza kwenda Kiswahili, mkalimani anapaswa kuwa mtaalamu au mahiri wa lugha mbili yaani Kiingereza na Kiswahili. Mbali na kuwa mahiri katika lugha mbili au zaidi, pia ni vizuri mkalimani akawa na uelewa juu ya dhanna anayoikalimani. Mkalimani anatakiwa kuwa na uelewa juu ya istilahi zinazotumika katika dhanna husika. Kama ni mahakamani, mkalimani anapaswa kuwa na uelewa wa hali ya juu wa istilahi za kisheria au kama ni mahubiri ya kidini mkalimani anapswa pia kuwa na uelewa juu ya istilahi za ki-Biblia au Kuran. Vilevile, mkalimani anapaswa kwenda na wakati kulingana na lugha inavyobadilika katika jamii kutokana na mifumo ya kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni iliyopo kwa wakati huo. Mkalimani anapaswa kuelewa angalau kwa ufupi juu ya jambo linalotarajiwa kuongelewa mbele ya hadhira kutoka kwa fanani au mtoa mada kabla ya kuanza shughuli ya kukalimani.
    2.   Uelewa wa kina juu ya hadhira husika
Mkalimani anapaswa kuielewa hadhira yake kiumri, kielimu, mazingira ya kijiografia, mtazamo na matarajio yake. Mkalimani anapokuwa na uelewa wa kina juu ya elimu ya hadhira yake inamsaidia kutumia lugha inayoeleweka kwa hadhira. Mkalimani anapokuwa na uelewa wa mazingira ya kijiografia ya hadhira yake inamsaidia kutumia lugha ambayo haikiuki mila na desturi za jamii husika. Vilevile, mkalimani anapaswa kuelewa umri wa hadhira yake kwa ujumla ili aweze kutumia lugha inayojenga uhusiano mwema kati yake na hadhira lengwa.
    3.   Uelewa wa kina juu ya matumizi sahihi ya mbinu za kimawasiliano
Mkalimani anapaswa kutumia mbinu mbalimbali za kimawasiliano anapofanya kazi yake ya kukalimani. Mkalimani hulazimika kutumia mifano na ishara mbalimbali zinazoeleweka kwa hadhira yake na zenye kuleta maana isiyo na dhanna ya kimatusi. Mifano hiyo iwe inahusu hadhira kwa lengo la kuelezea kwa kina kile kilichotamkwa na fanani. Mawasiliano mazuri huambatana na matumizi mazuri na sahihi ya maneno, sauti na ishara mbalimbali wakati mkalimani anapofanya kazi ya kukalimani.
Matumizi mazuri ya maneno huweza kutoa hamasa kwa hadhira juu ya kupenda na kuendelea kusikiliza kile kinachoelezwa. Mkalimani anapaswa kuepuka matumizi ya lugha ya mkato na maneno makali. Mkalimani ahakikishe istilahi anazotumia zinaeleweka vizuri kwa hadhira yake. Kwa kuwa kazi ya kukalimani huhusu mazungumzo, mkalimani hana budi kutumia sauti nzuri na yenye mvuto kwa hadhira yake. Matumizi sahihi ya kupanda na kushuka kwa sauti ya mkalimani huakisi kwa usahihi dhanna inayoongelewa pamoja na muktadha wa hadhira yake. Sauti inapaswa kusikika kikamilifu kwa hadhira lengwa kulingana na mada husika. Mkalimani anapaswa kuepuka kuongea polepole sana au kwa haraka sana.

Vilevile, mkalimani anapaswa kutumia ishara ili kusaidia hadhira yake kuelewa zaidi juu ya neno au maneno yaliyotamkwa. Kwa ufupi ni kwamba, mawasiliano ya ishara ni aina ya mawasiliano ambapo binadamu hutumia viungo vyake vya mwili kama vile macho, kichwa, mabega, mikono na vidole, kwa hiyo mkalimani wakati mwingine humlazimu kutumia viungo vyake vya mwili ili kujenga uelewa wa kina kwa hadhira yake kutokana na kile kinachosemwa na fanani.
Powered by Blogger.