MAENDELEO YA KISWAHILI CHIMBUKO NA ASILI YA KISWAHILI

SURA YA TATU

MAENDELEO YA KISWAHILI
CHIMBUKO NA ASILI YA KISWAHILI
Neno chimbuko linarejelea mahali kitu kilipoanzia. Hivyo basi tunapozungumzia chimbuko la kiswahili ni dhahiri kuwa tunataka kujua ni wapi hasa kiswahili kilianzia? Kuhusu chimbuko la kiswahili mpaka leo hakuna majibu sahihi na yenye ushahidi wa kutosha kuthibitisha jambo hili na hii ni kusema kuwa chimbuko la kiswahili halijulikani ni wapi hasa(Maelezo zaidi yapo mbele). Neno asili lina maana ya jinsi kitu au jambo lilivyotokea au lilivyoanza. Kwa hiyo tunapoangalia asili ya kiswahili tunaangalia jinsi kiswahili kilivyotokea au kilivyoanza   
      Kila lugha ina asili yake.Lugha huwapo ili kukidhi haja ya mahitaji ya kimawasiliano ya jamii inayohusika . Lugha ya asili ya jamii yoyote ndiyo inayotupa picha halisi ya  shughuli za maisha  ya jamii hiyo kwa mfano shughuli ya kazi ,sanaa,ufundi,mila na desturi.
Historia ya Kiswahili inakabiliwa na matatizo ya ithibati (ushahidi) kuhusu chimbuko lake kutokana na:
     i)  kukosekana kwa ushahidi wa kutosha
    ii)  walioiandika historia hii ni wageni ambao waliandika kadiri walivyodhani baada ya kupata ushahidi mdogo sana
  iii) kutofautiana kwa wataalamu kuhusu nadharia mbalimbali zinazohusu chimbuko la kiswahili.

Nadharia mbalimbali kuhusu asili ya Kiswahili.
1.        Kiswahili asili yake ni Kongo. Baadhi ya wataalamu hudai kuwa asili ya lugha ya kiswahili ni huko Kongo ambayobaadaye iliitwa Zaire na sasa inaitwa Jamuhuri ya watu wa Kongo.  





Dai hili linaimarishwa na wazo jingine linalodai kwamba katika vipindi vilivyopita kuwa,sehemu za pwani ya Afrika mashariki hazikuwa zimekaliwa na  watu. Kutokana na hali ya vita sehemu za Kongo wabantu walisambaa na kuja  pwani ya Afrika mashariki kupitia Kigoma. Baadhi ya wabantu hawa walipitia sehemu za Uganda wakati wa kusambaa kwao,walieneza pia lugha zao ikiwemo hii ya  kiswahili.
       Udhaifu wa nadharia hii ni kwamba madai ya kuwa asili ya kiswahili ni Kongo hayana msingi kwani mpaka sasa wataalamu wanaodai hivi hawajaweza kueleza na kuthibitisha kisayansi ama kihistoria juu ya lini hasa watu walianza kuishi pwani ya Afrika mashariki.

 2.    Kiswahili ni  Pijini  

Pijini ni lugha mseto ya muda inayozuka pindi makundi mawili yenye lugha mbili tofauti yakutanapo. Wenye kushikilia nadharia hii hudai kuwa Kiswahili kimezuka kutokana na kuingiliana kwa wenyeji wa pwani na wageni wa Kiarabu ambao kila mmoja alikuwa na lugha yake. Ili kufanikisha mawasiliano katika shughuli za biashara ndipokulipozuka lugha hii ya kati na kuwa lugha ya Kiswahili haikuwepo kabla ya ujio huu.
Kigezo wanachokitumia ni msamiati mwingi wa Kiarabu katika Kiswahili kama vile wakati , habari, salam.ahera, asante, shikamoo na mengineyo mengi.
Udhaifu wa nadharia hii ni kuwa haiangalii vipengele vingine vya lugha kama vile matamshi ya maneno, maumbo ya maneno na miundo ya tungo.

3.  Kiswahili  ni Krioli / lugha ya vizalia.

Kikrioli ni pijini iliyokomaa na kutumiwa kama lugha ya awali ya wazungumzaji wake . Wenye  kuunga mkono nadharia hii husema kuwa Kiswahili kimetokana na mwingiliano kati ya wanawake wenyeji wa pwani na waarabu ambapo mwingiliano huo ulizaa  uhusiano wa kimapenzi. Watoto waliozaliwa  (vizalia) ambao walikuwa ni chotara (suriyama) walijifunza maneno ya kibantu toka kwa mama zao na ya kiarabu toka kwa baba zao. Katika harakati za kujirekebisha wakajikuta wanaongea upotoshi wa lugha ya Kiarabu. Hivyo Kiswahili ni upotoshi wa matamshi ya lugha ya kiarabu.
Kigezo wanachokitumia ni msamiati na matamshi

Mfano:

 Wakt -  wakati
   Khabar – habari

Udhaifu wa nadharia hii ni kuwa haiangalii lahaja zingine za Kiswahili ambazo zinasikilizana katika msamiati, matamshi, maana za maneno na miuundo ya tungo.
Lahaja maana yake ni tofauti ya usemaji unaojitokeza kati ya wasema lugha moja. Utofauti huu waweza kuwa wa kimatamshi ama maumbo ya maneno lakini msingi wa maana na miundo hubaki kuwa ileile. Baadhi ya lahaja za Kiswahili ni Kiunguja, Kimakunduchi Kimafia, Kilamu, Kimvita, Kinzuwani,Kingazija , Kimtang’ata, nk.

      ZOEZI:

1.  Unadhani ni kwa sababu gani nadharia za pijini na krioli hazijitoshelezi kuthibitisha madai yao?
2.    Eleza uarabu uliomo  katika lugha ya Kiswahili.


4.            Kiswahili ni Kiarabu

Kuna hoja kuu tatu ambazo baadhi ya wananadharia hii huzitumia kutetea nadharia hii kuwa Kiswahili asili yake ni Kiarabu.
(i)Inahusu neno lenyewe Kiswahili ambalo asili yake ni Kiarabu. Neno Kiswahili linatokana na neno “sahel”(umoja) na “sawahil”(wingi) kwa maana ya pwani.
   (ii)        Inadaiwa kuwa maneno mengi yenye asili ya kiarabu yaliyomo katika kiswahili ni ishara kuwa kiswahili kilianza kama pijini ya kiarabu 
(iii)          Inadaiwa kwamba kwa kuwa Kiswahili kilianzia pwani, na kwa kuwa idadi kubwa sana ya wenyeji wa pwani ni waislamu na kwa kuwa uislamu uliletwa na Waarabu, basi Kiswahili nacho kililetwa na Waarabu.



UDHAIFU


    (i)        Lugha ya Kiswahili imetokea kuwa na maneno ya kigeni yenye asili ya Kiarabu, lakini si Kiarabu tu bali hata lugha nyingine kama Kiajemi, Kireno,Kihispania nk. Wasemaji wa lugha mbili tofauti wanapokutana hawaachi kuathiriana kilugha. Lugha kuwa na maneno mengi ya kigeni toka lugha nyingine hakuifanyi iwe imetokana na hiyo lugha nyingine.
                        .  
 (ii)       Kigezo cha dini nacho hakikubaliki, lugha haiwi lugha kwa sababu ya imani. Hata hivyo lugha ya Kiarabu yenyewe ilikuwepo karne nyingi kabla ya majilio ya uislam, kama ambavyo lugha nyingine za kimagharibi                                    zilivyokuwepo karne nyingi kabla ya majilio ya ukristo. Kiingereza au        Kijerumani si ukristo, wala Kiarabu si uislamu ila tunaweza kutumia lugha kufasili dini lakini hatuwezi kutumia dini kufasili lugha.


5.         Kiswahili ni kibantu

Kswahili kimetambulishwa kuwa ni lugha mojawapo ya lugha za kibantu. Neno Bantu lina maana ya mtu (wingi:Abantu) katika lugha nyingi za waafrika wanaoishi kusini mwa jangwa la sahara . Lugha za watu wanaoishi katika eneo hili huitwa lugha za kibantu.  Lugha za kibantu zina ufanano katika msamiati  na
Muundo wa sentensi.

 Mfano:

Neno ‘wana’ (watoto) – Kiswahili
           Vana     -   kingoni
            B’ana   - kihaya
Pia muundo wa sentensi ya Kiswahili
“wana ( watoto) wawili wanaoga” unafanana na miundo ya :

i)  Kingoni (vana bavili visamba)
                       N      V         T
           ii)Kichaga( wana  wawi wakesamba)
                           N       V          T
iii)  Kizigua (Wana  waidi wahaka)
                          N        V       T
iv) Kihaya  ( Abana   babili    mb’oga)
                         N        V                T            

   Nadharia hii huiangalia lugha ya Kiswahili kuwa ni Kibantu.            Wanaounga mkono mtazamo huu hutumia zaidi ushahidi wa kiisimu. Huichunguza lugha ya Kiswahili katika mfumo mzima wa historia ya mgawanyiko na kusambaa kwa lugha za Kibantu na huhitimisha kuwa Kiswahili ni mojawapo ya lugha katika jamii kubwa ya lugha za Kibantu.
Ubantu wa Kiswahili
               Ushahidi wa kiisimu unathibitisha ubantu wa Kiswahili. Ushahidi wa kiisimu ni ushahidi unaothibitishwa kwa misingi inayohusu sayansi ya lugha. Isimu ni taaluma inayoangalia lugha kwa undani (kisayansi) kuzungukia tanzu kama vile isimu historia, isimu linganishi ,isimu  jamii, isimu nafsi,isimu matumizi na isimu fafanuzi.    
Lugha ya Kiswahili ilifanyiwa utafiti na uchambuzi na wanataaluma kadhaa kwa madhumuni ya kuiainisha kama ilikuwa yenye misingi ya Kibantu au la.Vipengele vifuatavyo vinathibitisha ubantu wa Kiswahili.


1.         MSAMIATI

Msamiati wa msingi wa lugha ya Kiswahili na lugha za Kibantu       unafanana kabisa. Msamiati wa msingi ni ule unaohusu mambo ambayo hayabadiliki badiliki kutokana na shughuli za utamaduni. Tofauti zinaweza kujitokeza katika matamshi au mabadiliko kidogo ya viambishi vyake, lakini si mzizi.

            Mfano:
Kswahili:  Mtu     mtoto (Mwana)      maji
Kizigua  Umunu          Umwana       manzi            Kihehe    Muntu       Umwana            amanji
Kikurya   Omonto     Omona         amanche
                     


1.                  Tungo (sentensi) za Kiswahili

Miundo ya tungo (sentensi) za Kiswahili inafanana  sana na miundo ya tungo za Kibantu. Sentensi za kiswahili na lugha za Kibantu zina kiima na kiarifu.
                          K                   A
Kiswahili: watoto wawili / wanaoga
Kingoni: vana bavili / visamba
Kizigua: wana waidi / wahaka
Kichaga: wana wawi / wakesamba

3.         Ngeli za majina

Hapa kuna makubaliano kufuatana na ngeli katika maumbo ya nomino (umoja na wingi wa majina) pamoja na upatanisho wa kisarufi.

            (i)Maumbo ya majina
Kigezo hiki hufuata maumbo ya umoja na uwingi katika       kuyaainisha majina. Majina mengi katika lugha ya Kiswahili na lugha za Kibantu hufuata mkondo wa umoja na wingi. Majina ya lugha ya Kiswahili na lugha za Kibantu  mengi yana maumbo dhahiri ya umoja na uwing

Mfano:
                                                                           Umoja                                Wingi

Kiswahili  mtu                                   Watu
                                                                            Mtoto                              Watoto

Kibena Umwana                              Vana         umunu                                 Vanu
                                                                                   
Kikuyu    Omonto                banto(abanto)        Omona                   Bana(abana)                 

Kizigua  Mwana                      bhana              


(ii)        Upatanisho wa kisarufi

Katika kigezo hiki tunaangalia uhusiano uliopo kati ya nomino/ vivumishi na viambishi awali vya nafsi katika vitenzi vya Kiswahili na         Kibantu. Vivumishi, majina pamoja na vitenzi hivyo hubadilika kutokana na maumbo ya umoja na wingi.






Mfano:
Umoja                               wingi

Kiswahili baba analima    Baba wanalima
                                   
Kindali            tata akulima/ Abhatata chakulima
KikuryaTata ararema/Batata (tata) bararema
Kijita   tata kalima  /Batata kabalima

4.Vitenzi vya Kiswahili na Kibantu

Kuna uhusiano mkubwa sana kati ya vitenzi vya  Kiswahili na vile vya Kibantu.     Vipengele vinavyothibitisha uhusiano huu ni:viambishi, mnyumbuliko, pamoja na mwanzo / mwisho wa vitenzi.

(i)         viambishi

Lugha ya kiswahili na lugha za kibantu vitenzi vyake hujengwa na mzizi (kiini) pamoja na viambishi vyake (awali na tamati)


Mfano:

Kiswahili: -analima – A – na – lim- a
Kikuvya – ararema –A- ra_ rem –a
                                   1   2     3      4
1. kiambishi awali kipatanishi cha nafsi
2. kiambishi awali cha njeo (wakati  uliopo)
3. mzizi / kiini
4. kiambishi tamati



(ii)Mnyambuliko wa vitenzi

Mnyambuliko wa vitenzi vya lugha ya Kibantu hufafanana na ule wa vitenzi vya lugha ya Kiswahili

.
Mfano:

Kiswahili – kucheka – kuchekesha kuchekelea
Kibena – kuheka – kuhekesha – kuhekelela
Kinyamwezi – kuseka – kusekesha – kusekelela

(iii)mwanzo wa vitenzi

Vitenzi vingi vya Kiswahili na vitenzi vya lugha za Kibantu huanza na        viambishi amabavyo ni viwakilishi vya nafsi:

mfano:

Kiswahili         Ninakwenda
   Kihaya             Ningenda
Kiyao              Ngwenda


(iv)       Mwishilizo wa vitenzi

Vitenzi vya lugha za Kibantu na Kiswahili huishia na irabu – a

mfano:
Kiswahili - kukimbia  
Kisukuma – kupela
Kiswahili  - kula
Kizigua – kudya

                 Zoezi

1.Kwa kutumia mifano jadili asili ya kiswahili.
2.Kwa kutumia lugha yako (kibantu) jadili ubantu wa kiswahili.

3.“Uarabu wa kiswahili una hoja zake”, zitaje na zielezee.

4.“Kiswahili ni Kiarabu kwa jina lake, lakini ni Kibantu toka nitoke kwa asili yake” Thibitisha kauli hii kwa hoja madhubuti.

CHIMBUKO LA KISWAHILI

            Neno chimbuko lina maana ya mahali kitu au jambo lilipoanziaAma kuhusu suala la mahali hasa ambapo ndiyo chimbuko la lugha ya Kiswahili wataalamu wanahitilafiana. Wengine wanadai kuwa lugha ya Kiswahili inatokana na Kingozi lugha ya kaskazini mashariki mwa Kenya, na wengine wamesema kuwa Kiswahili chimbuko  lake ni Kishomvi kilichozungumzwa na watu wa Bagamoyo na Mzizima eneo linalojulikana kwa jina la Dar –es Salaam hadi Kilwa.
Wengine wanadai kuwa baadhi ya wabantu walifanya maskani yao ya kudumu katika mabonde ya kaskazini mwa mto Tana. Kikundi hiki cha wabantu ndicho kinasadikiwa kuwa chimbuko la Kiswahili katika mabonde hayo, wabantu walianzisha makazi yao Shupate na Shungwaya.
Mnamo miaka 500 AD, makazi ya mto Tana yalivamiwa na kushambuliwa na kabila la Wagala. Uvamizi huu uliwafanya wenyeji wake kukimbia na kusambaa katika sehemu mbali mbali za pwani ya bahari ya Hindi.
Lakini ikumbukwe kwamba kuna wakazi ambao walikuwa wakiishi maeneo mbali mbali katika upwa wa Africa mashariki waliokuwa wakizungumza lugha zao mbali mbali. Lakini kwa kuwa lugha hizo zote zilikuwa za Kibantu zilikuwa hazitofautiani sana. Sasa basi, katika kuwasiliana wao kwa wao katika masuala ya kibiashara wasemaji wa lugha hizo mbali mbali walilazimika kurahisisha lugha zao kwa kiasi fulani ili waweze kuelewana na wenzao katika kurahisisha lugha zao hizo katika maeneo mbali mbali kukazuka lugha moja iliyoeleweka kwa watu wote wa eneo hilo.
Hali hii ilitokea katika sehemu yote ya upwa wa Afrika mashariki kuanzia kaskazini hadi kusini. Matokeo yake yakawa ni lugha ambazo baadaye zilikuja julikana kama lahaja za kiswahili. Hivi ndivyo ilivyotokea lahaja ya Kibajuni Kitikuu katika sehemu za kusini mwa Somalia hadi kaskazini mwa Kenya. Kisiu sehemu za Pate, Kiamu katika Lamu, Chichifundi, Kimvita .
Katika sehemu za Mombasa, Kivumba, Kimtang’ata katika  sehemu za pwani ya kaskazini mwa Tanzania, Kimakunduchi, Kihadimu, Kitumbatu katika sehemu za Unguja na Pemba n.k. Hilo ndilo lilikuwa Chimbuko la lugha ya Kiswahili kama tuijuavyo leo.
Ukizichunguza kwa makini lahaja hizo za Kiswahili ni dhahiri kuwa ni lugha kamili zinazojitegemea. Vile vile lahaja hizo zinafanana zaidi na lugha nyingine za Kibantu kuliko zinavyofanana na lahaja ya Kiswahili sanifu ambayo ina maneno mengi ya kigeni.

ZOEZI

1.   Eleza maana ya lahaja, kisha taja lahaja zisizopungua tano na utaje mahali zinakozungumzwa.

2. Kwanini lahaja za pwani ziliitwa Kiswahili?

3. Kiswahili ni matokeo ya lahaja mbali mbali, je ni mushkeli gani unazikumba lahaja hizo baada ya tokeo hilo?

KUKUA NA KUENEA KWA KISWAHILI WAKATI WA WAARABU

            Waarabu walifika pwani ya Afrika ya Mashariki karne ya 8, Walipofika waliwakuta wenyeji wakizungumza lugha zao za Kibantu kikiwemo Kiswahili. Waarabu walipofika na dini ya kiislamu walijikuta wakishirikiana na wenyeji wa upwa huu katika mambo makuu matatu: Dini, biashara na kuoana (ndoa). Ili waweze kueneza dini yao vyema, Waarabu walijifunza kwa dhati lugha ya Kiswahili kwa vile walijishughulisha pia na biashara, waarabu waliweza kujumuisha mambo mengi kwa mara moja.

BIASHARA
            Ikumbukwe kwamba wenyeji wa pwani na wenyeji wa bara walikuwa na mawasiliano ya karne nyingi. Kulikuwa na safari za kibiashara baina ya pwani na bara zilizokuwa zikifanywa na waafrika wenyewe.
            Wageni walipofika katika upwa huu waliongozwa kwenda bara na wafanyabiashara wenyeji wa pwani na bara. Wafanyabiashara hao ndio walioanza kuieneza lugha ya kiswahili.
            Watu waliofuatia katika kuineza lugha hii walikuwa wale wafanya biashara wa kiarabu waliofuata pembe za ndovu na watumwa. Na hapa inabidi ikumbukwe kwamba ingawa biashara ya pembe za ndovu na watumwa iliendeshwa na waarabu wao sio walioineza lugha hii. Wao wenyewe hawakuijua, walikuwa wakifundishwa na wenyeji wao. Walioieneza lugha hii katika misafara hiyo ya kwenda bara walikuwa wenyeji wa pwani na bara ambao walikuwa wapagazi wa waarabu.
(Ramani kuonyesha misafara ya biashara ichorwe hapa)

DINI
            Mbali na shughuli za biashara uenezaji wa dini za kigeni pia ulichukua nafasi muhimu sana katika kueneza lugha ya Kiswahili. Waarabu walipoleta dini ya kiislamu walitumia sana lugha ya Kiswahili katika kuwashawishi wenyeji wa pwani kuslimu. Kwa kuwa mafundisho ya dini ya kiislamu yalikuwa katika Kiarabu, na kwa kuwa wenyeji wengi wa pwani hawakujua kiarabu wahubiri wa dini walilazimika  kujifunza Kiswahili ili waweze kutoa mafundishop na fasili za Kurani katika lugha iliyoeleweka kwa wengi. Baada ya hapo Waarabu waliojua
Kiswahili pamoja na ndugu zao wenyeji wa pwani wakapeleka uislamu bara kwa kutumia Kiswahili. Mashehe na Maulama wakaanzisha matumizi ya maandishi ya Kiswahili kwa kutumia alfabeti ya kiarabu. Kwa kufanya hivyo, wakawa wamesaidia sana katika kukineza Kiswahili.


Zoezi

1   Ni jinsi gani shughuli za waarabu zilichangia kukua na kuenea kwa lugha ya Kiswahili nchini Tanzania?



KUKUA NA KUENEA KWA KISWAHILI WAKATI WA  UTAWALA WA WAJERUMANI


Lugha hukua inapojiongezea msamiati wa kutosha . Wajerumani walikuza lugha ya Kiswahili kwa kuiongezea msamiati kama vile shule , mashine ,hela nk.
Kuenea kwa lugha maana yake ni lugha kuwa na eneo pana kimatumizi pamja na watumiaji wengi.
            Wajerumani walipoingia Tanganyika walikuta tayari kuna misingi mizuri ya lugha ya Kiswahili, hivyo utawala wa kijerumani ulipoanzishawa nchini Kiswahili kilikuwa tayari kimeimarika.
            Kwa misingi hiyo wajerumani waliona bora watumie lugha ya Kiswahili katika shughuli zao, licha ya jambo hili kupingwa sana huko ujerumani ambako waliona kuwa katika makoloni ilikuwa ni lazima lugha ya Kijerumanii ienezwe ili hatimaye kujengwa dola ya Kijerumani iliyo imara katika misingi yote ya kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni. Aidha baadhi ya wajerumani waliona lugha ya Kiswahili ilihusiana sana na dini ya kiislamu; kwa hiyo hawakuipenda kabisa. Jambo hili halikufanikiwa kwani wajerumani wenyewe walitumia lugha ya Kiswahili katika shughuli zao, ikiwa ni pamoja na mahubiri ya dini ya kikristo.
Katika shughuli za utawala walilazimisha kila Akida afahamu Kiswahili barabara ili aweze kutumwa na kufanya kazi mahali popote, siyo tu katika sehemu aliyozaliwa na kukulia. Hivyo wajerumani waliweka Kiswahili kama chombo cha kuwasiliana na watawaliwa wao na walilazimisha wafanyakazi wote wa serikali kujua Kiswahili. Wajerumani wenyewe walijifunza kiswahili huko kwao kabla ya kuja Tanganyika.
Shuleni Kiswahili kilitumika kama lugha ya kufundishia na Wajerumani walijenga shule Tabora, ujiji, Kilimatinde, Usangu mwaka 1905 na hatimaye Bukoba , Mpwapwa, Iringa, Mwanza, Kilosa, Tukuyu, na Moshi. Vyuo vya kufundishia walimu vilianzishwa huko Tabora na Bukoba.
Vile vile wajerumani walianzisha mashamba makubwa ya mazao ya biashara na wakalazimisha watanganyika kutoka bara na pwani kufanya kazi ya kulima katika  mashamba hayo. Kwa kuwa walikuwa watu wa makabila mbali mbali Kiswahili kilitumika sana katika mawasiliano na wale waliobahatika kurejea nyumbani walisaidia kukieneza Kiswahili huko kwao.
Kutokana na wajerumani kusisitiza matumizi ya Kiswahili katika shughuli za utawala, shule, mahakama na hata katika kuwasiliana na wananchi walisaidia sana kukieneza sehemu mbali mbali za Tanganyika.





ZOEZI


1.         Eleza kwa vipi wajerumani walikuza na kueneza lugha ya kiswahili nchini   Tanzania. 

2.         Waarabu na wajerumani ni taifa lipi lilitoa mchango mkubwa katika kukuza na kueneza lugha ya kiswahili Tanzania?.
Powered by Blogger.