Spika Anna Makinda achachamaa

Spika wa Bunge, Anne Makinda. Picha na Maktaba
Dar es Salaam. Spika wa Bunge, Anne Makinda amezitaka kamati tatu za Bunge ambazo wenyeviti wake walitakiwa kuwajibika kutokana na kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow, kufanya uchaguzi wa wenyeviti wengine kabla ya kuanza kwa Mkutano wa 18 wa Bunge, Januari 27 mwaka huu mjini Dodoma.
Uamuzi huo wa Spika Makinda umekuja baada ya wenyeviti wa kamati hizo waliotakiwa kuwajibika, William Ngeleja (Katiba, Sheria na Utawala), Victor Mwabalaswa (Nishati na Madini) na Andrew Chenge (Bajeti) kujitambulisha kuwa bado ni wenyeviti, huku Ngeleja akiendelea kuongoza vikao hadi juzi.
Siku mbili zilizopita Spika Makinda alikaririwa akisema wenyeviti hao wameshajiuzulu, lakini wajumbe wake waliibuka siku moja baadaye na kusema hawatafanya uchaguzi hadi watakapopata maelekezo kutoka Ofisi ya Spika.
Katika Azimio lake la tatu kuhusu kashfa hiyo, kati ya maazimio manane, Bunge liliazimia: “Kamati husika za Kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya Mkutano wa 18 wa Bunge, kuwavua nyadhifa zao wenyeviti tajwa wa kamati husika za kudumu za Bunge.”
Taarifa zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah zilieleza kuwa Spika Makinda ametoa agizo hilo jana mchana.
Awali, wajumbe wa kamati hizo tatu walilithibitishia gazeti hili kuwa walipokea maelekezo kutoka ofisi ya Spika wakiwataka kufanya uchaguzi huo kabla ya Januari 27.
“Binafsi sisi Kamati ya Nishati na Madini tutafanya uchaguzi wetu mjini Dodoma Jumatatu ijayo. Tumepewa maelekezo hayo leo (jana).
Powered by Blogger.