Madiwani wataka mkurugenzi asimamishwe

Moshi. Baraza la Madiwani Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, limepitisha maazimio ya kumtaka Rais Jakaya Kikwete, kumsimamisha kazi kwa muda mkurugenzi wa manispaa hiyo, Shaban Ntarambe.
Mbali na kusimamishwa kazi kwa mkurugenzi huyo, lakini baraza hilo limeunda kamati ya madiwani wanne kuchunguza mchakato mzima wa kuhamisha miliki ya kiwanja kinachodaiwa ni cha Umma. Maazimio hayo yaliyosomwa jana alasiri baada ya kumalizika kwa kikao maalumu cha baraza hilo kilichoitishwa mahsusi kujadili ajenda moja tu ya umiliki wa kiwanja hicho kilichoibua mgogoro.
Wakati halmashauri ikidai kukimiliki kiwanja hicho kilichopo ofisi za kata ya Mawenzi, Jumuiya ya Wazazi ya CCM na Mawenzi Sports Club nazo kwa nyakati tofauti zimeibuka na kudai ni wamiliki.
Akisoma maazimio hayo, ambayo baadaye yalisahihishwa na Meya, Jaffar Michael na msoma maazimio, Sophia Mshiu alisema theluthi moja ya madiwani ndiyo walioonyesha kutokuwa na imani na Ntarambe.
Alisema madiwani hao ni wale wanaotokana na Chadema na kwamba wamemtaka Rais kumsimamisha kazi mkurugenzi huyo ili kupisha uchunguzi utakaofanywa na kamati ya madiwani hao wanne.
Madiwani wanaounda kamati hiyo ni Dk Charles Mmbando (Naibu Meya), ambaye atakuwa mwenyekiti na wajumbe Priscus Tarimo, Raymond Mboya na Peter Kimaro.
Pia, kamati hiyo itawahusisha wataalamu watatu wa halmashauri, ambao ni Erick Mapunda, Ofisa Utumishi, Anitha Bureta, Afisa Ushirika na Peter Mbwambo, Ofisa Elimu.
Baraza hilo pia limeiagiza ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri hiyo, kuweka zuio la kisheria katika kiwanja hicho, ambacho zamani kilikuwa kikitumika kama ofisi ya Shule ya Sekondari ya Kibo.
Baada ya kusomwa kwa maazimio hayo, Meya alisema ni vyema kumbukumbu ikawekwa sawa kuwa theluthi mbili ya madiwani wote ndiyo waliokosa imani na mkurugenzi na wanne wa CCM walipinga.
Katibu wa Madiwani wa CCM, Michael Mwita alisimama na kuungwa mkono na wenzake kuwa wao hawakuunga mkono azimio la kuwamwajibisha mkurugenzi, kwa vile halikufuata sheria.
Kabla ya kufungwa kwa kikao hicho, mkurugenzi aliomba nyaraka zote alizoziwasilisha katika kikao hicho zisichukuliwe kuwa ndio utetezi wake bali yalikuwa ni mawasiliano ya wataalamu wa Serikali.
Akifunga kikao hicho, Meya alisema amewaelewa madiwani hao na kusema moja ya hadidu za rejea za kamati hiyo itakuwa kuchunguza mchakato mzima wa umiliki wa kiwanja hicho.
Powered by Blogger.