Okwi hatihati kuivaa Mbeya City

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi jana alilazimika kurudishwa tena Hospitali ya Taifa Muhimbili kufanyiwa kipimo cha CT scan kujiridhisha iwapo ataweza kucheza kesho mechi dhidi ya Mbeya City.
Okwi aliumia dakika ya 62, na kupoteza fahamu wakati wa mchezo kati ya Simba dhidi ya Azam juzi mechi iliyomalizika kwa sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Daktari wa Simba, Yassin Gembe alisema wamelazimika kufanya vipimo tena ili kujiridhisha kutokana na hali aliyokuwa nayo uwanjani jana (juzi).
“Hali ya Okwi siyo mbaya ingawa tunahitaji kujiridhisha kwa kumfanyia uchunguzi zaidi kama kwa hali aliyonayo ataweza kucheza kwenye mechi ya Jumatano dhidi ya Mbeya City au la,” alisema Daktari Gembe aliyeambatana na mchezaji huyo Muhimbili jana asubuhi.
Kufuatia tukio hilo, uongozi wa Simba ulikutana na kujadili kitendo hicho huku ukijipanga kutoa tamko.
Katibu mkuu wa timu hiyo, Steven Ally alisema kitendo alichofanyiwa mchezaji wao kwenye mechi hiyo siyo cha kiungwana na kusisitiza kuwa, wakati wowote kuanzia sasa uongozi utatoa tamko kuhusu tukio alilofanyiwa mchezaji wao.
Gazeti hili lilifikia makao makuu ya Simba, Kariakoo na kushuhudia mashabiki wa timu hiyo wakiwa vikundi vikundi wakijadili kitendo alichofanyiwa Okwi na wakautaka uongozi kutolifumbia macho suala hilo.
Wakati huohuo. African Sports imejiweka katika mazingira mazuri ya kupanda Ligi Kuu msimu ujao baada ya kuichapa Majimaji kwa bao 1-0 jana kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Bao pekee la African Sports lilifungwa dakika ya 70 na Ramadhani Msheli akiunganisha kwa umakini krosi ya James Mendi.
Powered by Blogger.