Muhongo aachia ngazi


Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akitangaza kujiuzuru nafasi yake ya Uwaziri, kutokana na kasha ya uchotwaji wa fedha katika akauti ya  Tegeta escrow, wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari ofisini kwake, Dar es Salaam, jana. Picha na Emmanuel Herman
Dar es Salaam. Dakika 50 zilimtosha Profesa Sospeter Muhongo kujieleza kwa urefu wakati akitangaza uamuzi wake wa kujiuzulu uwaziri wa Nishati na Madini akisema “anataka nchi isonge mbele” baada ya kashfa ya uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow kutikisa Taifa.
Muhongo, ambaye aliteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa mbunge Mei 3, 2012 na siku nne baadaye kuteuliwa kuwa waziri, alitangaza uamuzi huo jana saa chache kabla ya kutangazwa Baraza la Mawaziri lenye mabadiliko 13, ikiwa ni kuziba nafasi za mawaziri wawili- mwingine ni Profesa Anna Tibaijuka- waliotajwa kwenye kashfa hiyo. Mawaziri hao waliapishwa jana baada ya kutangazwa.
“Sasa ni lazima kila kitu kiwe na tamati, na ninadhani mimi ninaweza kuwa sehemu ya suluhisho la malumbano yasiyokuwa na mwisho,” alisema Profesa Muhongo mbele ya waandishi wa habari waliojaa kwenye chumba cha mikutano cha Wizara ya Nishati na Madini na ambao walimsubiri kwa takriban saa moja na nusu.
Profesa Muhongo aliingia kwenye chumba hicho na kabla hata hajakaa vizuri akasema utaratibu wa kujitambulisha hautakuwapo kutokana na idadi ya watu waliopo.
“Sasa ndugu zangu waandishi wa habari na wageni waalikwa nadhani kwa muda mrefu sana hamjanisikia naongea jambo lolote kuhusu mambo ya escrow baada ya kutoka bungeni,” alisema.
Kama ambavyo amekuwa akijieleza kwa staili ya kusifia kazi aliyofanya kwa mafanikio, Profesa Muhongo alianza hotuba yake ya kutangaza kujizulu kwa kuzungumzia mafanikio yake kwa muda wa miaka miwili na nusu aliyokaa kwenye wizara hiyo, ambayo sasa imepoteza mawaziri wanne katika Serikali ya awamu ya nne.
Akizungumzia uamuzi wake wa kujiuzulu, mbunge huyo wa kuteuliwa alisema ameamua kuchukua uamuzi huo ili kuipa nafasi Serikali iwatumikie wananchi badala ya kushinda kwenye vikao visivyokuwa na mwisho kujadili sakata hilo.
“Chama changu cha Mapinduzi ni lazima kiendelee kuwatumika wananchi hasa wale walio maskini kuliko kila siku CCM kukaa kwenye vikao wanaongelea suala la escrow,” alisema.
Alisema hata Bunge haliwezi kuendelea kuongea kitu ambacho hakina mwisho kwa sababu alipozungumza bungeni alitoa tamko la Serikali.
Alisema hakutaka kulizungumzia suala la escrow baada ya vikao vya Bunge kwa kuwa alidhani siyo busara kuendelea kulumbana wakati Watanzania wanataka kupumzika. Aliongeza kuwa baada ya Rais Kikwete kuzungumzia suala hilo, alidhani kuwa ingekuwa mwisho, lakini ameona mjadala unaendelea.
“Na leo navyotaka kuliongea hili, nadhani kama tunalipenda Taifa letu na kama tunataka kufuta umaskini basi mjadala wa escrow tutakuwa tumeiachia mahakama au watu wengine wanaohusika,” alisema.
Alieleza kuwa mkataba wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco) na escrow ulikuwa Mei, 1995 wakati huo alikuwa akifanya kazi ya utafiti nchini Ujerumani.
“Akaunti ya escrow imefunguliwa mwaka 2006, ndugu zangu mwaka huo sikuwa nchini nilikuwa Pretoria nina majukumu ya kusimamia maendeleo ya sayansi kwenye bara la Afrika. Kwa hiyo kuanzishwa kwa IPTL nchini sikuwapo, kuanzishwa kwa escrow sikuwapo, lakini nikapewa majukumu ambayo yananifanya nisogelee IPTL na escrow,” alisema Profesa Muhongo.
Bunge halikumtuhumu Profesa Muhongo kuwa alichukua rushwa, lakini alitumia muda mwingi jana kueleza kuwa hajawahi kupokea na hawezi kupokea rushwa.
Alisema aliisoma mara nne ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikalia (CAG) iliyochunguza sakata la escrow na aliona hakuna sehemu yoyote anahusika au ana hatia.
Alifafanua kuwa hata baada ya watu kugawana fedha za escrow kutoka kwenye mabenki yanayotajwa, hakuwa na nyaraka zozote zinazoonyesha kuwa alipewa fedha hizo.
“Nendeni kwenye benki ambazo zinahisiwa zilichukua fedha za escrow, msichukue maelezo ya mitandaoni ambako mtu anaandika akaunti feki tu anasema sijui mtu fulani, hapana nendeni benki. Sijachukua senti popote,” alisema.
“Na isitoshe ndugu zangu Watanzania haiwezekani uanze kuiba kwenye umri kama wa kwangu hivi, nadhani mwizi anaanza zamani,” alisema Profesa Muhongo mwenye umri wa miaka 61 huku akiacha kicheko ukumbini.
Alieleza kuwa hata katika nchi za Ujerumani, Ufaransa ambako alitunukiwa nishani ya Napoleon na China hakuna hata siku moja alikopa au kuiba fedha za utafiti.
“Sijawahi kuiba hela mahali popote pale na wote waliofanya kazi na mimi wananielewa mimi siingiliki kwa rushwa. Haiwezekani unipatie rushwa na kama kuna Mtanzania amenipatia rushwa ajitokeze kama yupo,” alisema.
“Na siyo rahisi wewe kunipatia rushwa, haiwezekani. Huenda watu wengine hali kama hiyo hawaipendi.”
Bunge lilimuingiza Profesa Muhongo kwenye kashfa hiyo kwa kumtuhumu kuwa alishindwa kushughulikia vizuri sakata la escrow kwa makusudi au uzembe na kusababisha Taifa kupoteza fedha kutokana na kodi. Pia, alidaiwa kushindwa kuhakiki ununuzi wa hisa za IPTL kwa kuwa nyaraka zilizotumika kuuza hisa kutoka Mechmar Corporation na Piper Links zilikuwa za kughushi, uhakiki ambao Bunge liliambiwa kuwa unatakiwa ufanywe na waziri husika.
Kuhusu tuhuma kwamba waziri huyo ndiye aliwakutanisha watu waliochota fedha za escrow, Profesa Muhongo alisema kama ingekuwa ni kweli yeye ndiye angekuwa wa kwanza kupewa fedha za shukrani.
Katika sakata hilo, zaidi ya Sh306 bilioni zilichotwa kwenye akaunti hiyo iliyofunguliwa Benki Kuu (BoT) kuhifadhi fedha ambazo Tanesco ilitakiwa kuilipa IPTL baada ya pande hizo mbili kuingia kwenye mzozo wa kiwango cha tozo ya umeme unaozalishwa na IPTL na kufungua kesi.
Uamuzi wa kesi hiyo ulitaka pande hizo mbili zikokotea upya viwango hivyo, lakini fedha hizo ikachotwa mwishoni mwa mwaka juzi na kulipwa kwa Kampuni ya Pan African Power Solutions ambayo ilinunua hisa zote za IPTL na baadaye baadhi ya fedha hizo kugawanywa kwa vigogo wa Serikali, mawaziri wa zamani, watendaji waandamizi wa Serikali na viongozi wa kidini.
Kabla ya kuchotwa kwa fedha hizo, Mamlaka ya Mapato (TRA) iliiandikia BoT kutaka isifanye malipo hadi ikate kodi ambayo Tanesco ilitakiwa ilipe, lakini Mwanasheria Mkuu wa wakati huo, Frederick Werema alishauri fedha hizo zisikatwe. TRA pia ilibaini kuwapo wa udanganyifu wa kiwango cha kodi kilichotozwa wakati wa kuuza hisa za IPTL kwa kampuni ya PAP na hivyo kulikosesha Taifa mapato.
Tayari Anna Tibaijuka, aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, amevuliwa madaraka hayo wakati Werema amejiuzulu wadhifa wake wa Mwanasheria Mkuu, huku Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliackim Maswi amesimamishwa kwa uchunguzi. Maofisa waandamizi watano wa Tanesco, TRA na BoT wamefikishwa mahakama kwa tuhuma za kupokea rushwa inayofikia jumla ya Sh1.9 bilioni.
Pia wenyeviti wanne wa kamati za Bunge, Andrew Chenge, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu, William Ngeleja, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Victor Mwambalaswa aliyekuwa mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na wakati huohuo mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Tanesco, wamejiuzulu.
Kuhusu kuitwa kwake kuja kuwa mbunge na baadaye waziri, Profesa Muhongo alisema alilazimika kuiacha kazi aliyokuwa anaifanya mjini Pretoria, Afrika Kusini.
“Nilijua ninaitwa kuja kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa hili ya 2025 inayosema kuwa ukifika mwaka huo umaskini uwe umetoweka nchini, alisema.
Kiini kashfa ya escrow
Profesa Muhongo alisema hoja ya escrow imebeba mambo mengi ndani yake, ambapo sasa imeibuka mivutano ya kisiasa isiyokuwa na mwisho huku wananchi wakionekana kuchoshwa na hali hiyo.
Alikumbusha kuwa mwaka 1969 wakati mtu wa kwanza kutua mwezini, Mwasisi wa Taifa, Julius Nyerere alisema wakati wengine wanatua mwezini, sisi twende vijijini.
“Mimi nilikuwa natekeleza wazo la Nyerere,” alisema.
Alisema kwa muda wote aliokuwa wizarani hapo alitumia muda mwingi kupeleka umeme vijijini na kwamba ifikapo Juni mwaka huu vijiji 1,5000 vitakuwa na umeme.
“Ndiyo kazi niliyoisimamia kwa miaka miwili na nusu niliyokaa hapa wizarani,” alisema.
Aliongeza kuwa wakati nchi za Afrika zinapata uhuru, baadhi ya viongozi walitaka kujenga barabara zitakazounganisha Afrika nzima, lakini yeye amejenga barabara za umeme.
“Kuna watu wana mambo yao binafsi, Watanzania wamechoka, Serikali imechoka, CCM imechoka na hata mimi nimechoka… ndani ya escrow kuna wivu, kuna chuki, kuna fitina. Kama kweli dira yetu ya maendeleo miaka 10 ijayo tunataka Tanzania lisiwe taifa la umasikini, hatuwezi kuendelea kwa kuendeleza vitu hivi vinne ambavyo ni siasa, biashara, ubinafsi, wizi, chuki na fitina lazima tufike mwisho,” alisema.
“Ambaye anaweza kuwa suluhisho la kufika mwisho ni mimi hapa. Tunalumbana na mambo ya escrow, lakini mimi ninayezunguka mikoani kukagua miradi ya maendeleo, nilikuwa Tabora, Shinyanga, Simiyu na Mara, sikuulizwa kuhusu escrow.
“Baada ya kutafakari na kujadiliana na wakubwa zangu, lazima taifa langu liwe juu ya kazi niliyopewa, lazima maslahi ya taifa hili yawe ni muhimu zaidi kuliko cheo cha mtu mmoja kwa maneno mengine ndugu zangu walioko vijijini wanataka umaskni uwatoke.
“Viwanda vinataka kupata umeme, vijana wanataka kupata ajira na ndiyo maana nimejiona ni sehemu ya suluhisho na ndiyo maana nimemwaomba rais niachane na nafasi ya uwaziri ili taifa lisonge mbele hakuna sababu ya kuendelea kulumbana. Tunapoteza muda na rasilimali zetu.”
Aliongeza kusema: “Uamuzi nimeufanya kwa sabahu nataka Serikali ibaki inashughulikia matatizo ya wananchi badala ya Serikali kuu kushughulikia escrow. Naachia ngazi ya uwaziri kwa sababu nataka chama changu CCM kiendelee kutatua kero za wananchi badala ya kukaa vikao kujadili suala la escrow, nataka bungeni niwe mbunge wa kawaida na hii itatoa fursa kwa Bunge letu kutumia muda vizuri na rasilimali.
“Naachia hii kwa sababu Watanzania wamechoka, escrow haifuti umaskini na ninyi waandishi wa habari leo anzeni kuwapatia habari zao na mimi nina familia familia yangu haiwezi kuamka inakuta escrow, escrow kuna watu wanasoma watashindwa kusoma.”
Zitto na Kafulila
Akizungumzia uamuzi wa kujiuzulu, Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe alisema: “PAC tulichokuwa tunakitaka ni kuona utekelezaji tu wa maazimio ya Bunge na wala hatuna chuki na mtu yeyote… na PAC tukifika Dodoma tutapokea taarifa rasmi ya utekelezaji wa maazimio hayo.”
Aliongeza: “Tumeshuhudia watu wamefikishwa mahakamani, lakini bado ni vidagaa, tunataka wakubwa wapelekwe mahakamani. Hiyo ni busara aliyochukua ambayo ninaamini itasaidia harakati za kujenga demokrasia yenye uwajibikaji na kulinda heshima ya Bunge na maazimio yake.”
Zitto, ambaye pia ni mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), alisema: “Muhongo si mmoja tu kati ya waliotajwa kwani tumeona Tibaijuka, Werema na sasa Muhongo hivyo kama kamati tutakaa na kujadili utekelezaji wa maazimio hayo manane ya Bunge. Hata Ngeleja, Chenge Spika (Anne Makinda) tumesikia amekwishawaandikia barua ya kamati zao kufanya uchaguzi.”
Mwasisi wa sakata hilo bungeni, David Kafulila alisema: “Kujiuzulu ni jambo la busara na kwa kiongozi inaonyesha uwajibikaji na ni heshima lakini Profesa Muhongo alichelewa sana hivyo kuwapo kwa taswira tofauti kwa taifa na wananchi.”
“Hakuna serikali duniani iliyoshindana na Bunge na Serikali ikashinda. Hii ni changamoto kwa watendaji kuwa Bunge halishindani na Serikali hata siku moja, Muhongo alikuwa anapima mabavu ya Bunge sasa ameshindwa.”
Kafulila alisema alibainisha mambo matatu ambayo yalitakiwa kufanyika kuwa; waliohusika kujiuzulu au kufukuzwa kazi, kurudisha fedha kama ilivyokuwa katika kashfa ya Akaunti ya Benki ya Madeni ya Nje (EPA) pamoja na kufikishwa mahakamani.
Wasomi
Mtaalamu wa Maendeleo na Utawala wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dk Emmanuel Mallya alisema: “Ni uamuzi mzuri na wakati mwingine unawajibika hata kama hukukosea wewe.”
“Amefanya jambo la busara kwani watu walikuwa wameanza kupoteza imani naye na amechelewa kuchukua uamuzi huo na hii ni hulka ya jamii yetu tunayotoka.”
Profesa George Shumbusho wa Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema: “Amechukua uamuzi sahihi lakini amechelewa. Viongozi wetu wanatakiwa kuiga dhana ya uwajibikaji, siyo hadi maneno yanasemwa hadi yasiyotakiwa.”
Powered by Blogger.