Watafiti UDSM kusafisha majitaka kuwa ya kunywa

Dar Es Salaam. Kitengo cha Utafiti cha Idara ya Uhandisi, Teknolojia na Madini (COET) cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kipo katika mchakato wa kusafisha majitaka yanayotokana na kinyesi na kuyarejeleza kuwa safi na salama kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.
Mkuu wa COET, Profesa Jamidu Katima alisema hayo jana katika mkutano wa wanasayansi ulioandaliwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia (Costech).
Alisema idara hiyo inatarajia kukamilisha utafiti huo siku zijazo baada ya kufanikisha teknolojia hiyo ambayo maji yake pia yatafaa kwa umwagiliaji na mifugo.
Hivi karibuni kampuni ya nishati ya Marekani ya Janicki Bioenergy, ilizindua maji ya kunywa yaliyozalishwa kwa kutumia majitaka.
Akizungumzia teknolojia hiyo, mkurugenzi wa Costech, Dk Hassan Mshinda alisema huu ni wakati wa Taifa kutumia sayansi katika kukuza uchumi wa kilimo na viwanda.
“Huu ni mradi muhimu sana kwa sababu teknolojia hii inasaidia siyo tu kupata maji masafi yanayofaa kwa matumizi mengine, pia yanasafisha mazingira,” alisema.
Dk Mshinda alisema majitaka ya viwandani yanaharibu mazingira na iwapo yatasafishwa yataepusha mambo mengi ikiwemo maradhi.
Alisema Costech inajivunia kufanya kazi za kisayansi kwa kushirikiana na sekta binafsi na Serikali na kusisitiza kutumia tafiti za wanasayansi.
“Ufike wakati tafiti zinazofanywa na wanasayansi wazawa zisitumike kuibua hoja bungeni tu, bali matokeo ya tafiti hizo yatumike kutunga sera na sheria,” alisema.
Wanasayansi wa COET walitumia teknolojia hiyo katika kiwanda cha mvinyo cha Banana.
Walirejeleza majitaka ya ndizi zilizokamuliwa na kuwa majisafi yaliyofaa katika umwagiliaji, mbolea, kunywesha mifugo na kuoga.
Kabla ya mtambo wa kusafisha kujengwa, kiwanda hicho kilikuwa kikizalisha lita 80,000 za majitaka kwa wiki.
Powered by Blogger.