Serikali yafungia gazeti la The EastAfrican

Gazeti la The EastAfrican limepigwa marufuku kusambazwa Tanzania, ikiwa ni miaka 20 baada ya
Picha ya mbele ya gazeti la The EastAfrican. Picha na Maktaba
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Gazeti la The EastAfrican limepigwa marufuku kusambazwa Tanzania, ikiwa ni miaka 20 baada ya kuanzishwa kwake kwa ajili ya kuandika habari za ukanda wa Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa barua iliyotumwa mwakilishi wa The EastAfrican nchini, uamuzi huo umechukuliwa kwa sababu gazeti hilo “limekuwa likisambazwa nchini bila ya kuwa na usajili, kinyume na kifungu cha 6 cha Sheria ya Magazeti, Namba 3 ya mwaka 1976”.
Uongozi wa Nation Media Group, ambao unamiliki gazeti la The EastAfrican, umeelezea hatua hiyo kuwa ni ya kushangaza na isiyokubalika.
Barua hiyo ya Januari 21, 2015 inaagiza kusimamishwa mara moja kwa uchapishaji na usambazaji wa gazeti hilo nchini Tanzania ‘’hadi litakaposajiliwa rasmi na Msajili wa Magazeti, Idara ya Habari’’.
Kabla ya kutolewa kwa barua hiyo, mwakilishi wa gazeti hilo nchini, Christopher Kidanka aliitwa Jumatano na kuhojiwa na mkurugenzi wa Idara ya Habari, ambaye pia ni msemaji wa Serikali, Assa Mwambene.
Katika mahojiano hayo, Serikali ilieleza kutofurahishwa na jinsi gazeti hilo linavyoripoti habari na uchambuzi wake (zikiwamo safu za maoni).
Mwambene alilituhumu gazeti hilo kwa kuwa na mtazamo hasi dhidi ya Tanzania. Alitoa mfano wa maoni ya hivi karibuni ambayo yalikosoa msimamo wa Serikali kuhusu waasi wa Rwanda, FDLR walioko nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kama mfano wa mtazamo wa gazeti dhidi ya nchi.
Mwambene pia alielezea katuni iliyotoka kwenye toleo la wiki hii la The EastAfrican, kuwa ilionyesha kutozingatia utamaduni na kwamba ilionyesha kutomuheshimu Rais.
Matokeo yake, The EastAfrican halitakuwa likisambazwa hadi masuala ya kisheria yatakapotatuliwa.
Akizungumzia uamuzi huo wa Serikali, mwenyekiti wa Bodi ya NMG Group, Wilfred Kiboro alisema sababu zilizotolewa na Serikali zinashangaza kwa sababu gazeti hilo limekuwa likisambazwa tangu miaka 20 iliyopita.
“Kwa hakika hawawezi kuamka leo na kututangaza kuwa hatuko kihalali. Kama ingekuwa ni suala la kuweka sawa mafaili, hilo halihitaji hatua za kikatili za kufungia gazeti,” alisema.
Alisema kwamba sababu halisi “ziko sehemu nyingine “ na zinaweza tu kuhusishwa na msimamo ambao gazeti hilo, na mengine ya kampuni NMG, limechukua katika kuripoti rushwa, wizi wa mali za umma na utoaji duni wa huduma kwa watu wa Afrika Mashariki.
“Mwaka jana, Serikali ilifungia gazeti letu la Mwananchi kwa wiki mbili kwa sababu ambazo hazijawahi kuwekwa bayana,” alisema.
Kiboro aliongeza kuwa sera za habari za NMG ziko wazi kuhusu uhuru wa vyombo vyake, kitu ambacho kitaendelea kuongoza magazeti yetu katika kuripoti wakati wote.
“Tunajua kuwa kuna wakati tulifanya makosa katika uamuzi na tumefanya haraka kuomba radhi, kama ilivyokuwa katika suala la katuni inayozungumziwa. Makosa kama hayo, hata hivyo, hayatakiwi kuhalalisha kufungia gazeti kwa sababu kufungia vyombo vya habari kunafanywa na madikteta wasiowajibika,” alisema.
Alisema kuwa ana matumaini Serikali ya Tanzania, kwa kuheshimu dhamira yake ya uhuru wa vyombo vya habari na kuunga mkono demokrasia, itaharakisha kuliruhusu gazeti la The EastAfrican kurejea sokoni.
Kampuni ya NMG, kwa kupitia kampuni yake ya Mwananchi Communications Ltd, pia inachapisha magazeti ya Mwananchi, the Citizen na Mwanaspoti ya Tanzania.
Powered by Blogger.