Ripoti ya wizara yazidi kuiweka pabaya IMTU

Dar es Salaam. Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesema Hospitali ya Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Tiba na Teknolojia (IMTU) hakitafunguliwa mpaka pale upungufu ulioainishwa utakapofanyiwa kazi.
Kwa mujibu wa ripoti ya Kamati Maalumu ya Ukaguzi iliyoundwa na wizara hiyo, IMTU iliyofungiwa Julai mwaka jana, haitaweza kuendelea na huduma kutokana na ukaguzi uliofanyika Desemba 19 kubaini kwamba bado ina upungufu kwa asilimia 50 licha ya kufanyiwa ukarabati.
Ripoti hiyo ilibainisha pia kuwa, licha ya kupewa muda wa kufanya marekebisho, bado sehemu nyingi za kutolea huduma zinakosa nafasi ya kutosha, mazingira yasiyo rafiki kwa watu wenye mahitaji maalumu pamoja na mfumo wa maji kuwa mbovu huku majengo yakiwa bado na nyufa.
Ilithibitishwa kwamba, hakuna mfamasia aliyeajiriwa kwa mkataba wa kudumu huku idadi ya wauguzi 16 waliopo ni wachache na kwamba haikidhi mahitaji ya hospitali.
Pia taarifa hiyo ilieleza kwamba kuna watumishi waliopewa majukumu bila sifa stahiki na wengine kupatiwa mafunzo kazini na upungufu katika wodi za upasuaji.
“Licha ya kukosekana kwa uboreshaji wa huduma za afya hospitalini hapo, timu haikuona mpango mkakati wala mpango wa utekelezaji wa mwaka na ilibainika kwamba, miongozo hii muhimu ni siri ya wachache,” ilisema sehemu ya ripoti hiyo.
Mkurugenzi wa Hospitali ya IMTU, Profesa Yasini Mgonda alisema wameshakamilisha ukarabati wa kituo hicho, lakini bado hawajaweza kufungua hadi watakapopata tamko kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii. Profesa Mngoda alisema kasoro zilizoainishwa zimeshatekelezwa na wanachosubiri ni ruhusa kutoka wizarani.
Powered by Blogger.