FastJet yashindwa tena kutua Uwanja wa Songwe


ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Kwa mara nyingine, hali ya hewa mjini Mbeya jana ilisababisha ndege ya kampuni ya FastJet, iliyokuwa na abiria 120, kushindwa kutua kwenye Uwanja Ndege wa Kimataifa wa Songwe na kurejea Dar es Salaam.
Hii ni mara ya pili katika kipindi cha takriban wiki mbili kwa tukio hilo kujirudia baada ya ndege nyingine ya FastJet, iliyokuwa na abiria 131 Januari 12, kushindwa kutua uwanjani hapo kutokana na hali mbaya ya hewa.
Kwa mujibu wa ratiba, ndege hiyo iliondoka Dar es Salaam saa 3.05 asubuhi na kutakiwa kutua saa 4.30 asubuhi kwenye uwanja huo wa Songwe, takribani mwendo wa saa moja na dakika ishirini.
Meneja mkuu wa Fastjet Tanzania, James Kibati alisema ndege hiyo ilishindwa kutua kutokana na hali mbaya ya hewa na kulazimika kurudi Dar es Salaam.
“Tunasubiri kibali cha watu wanaohusika na hali ya hewa hapa uwanjani, wakituruhusu tutaondoka tena leo (jana),” alisema Kibati.
ADVERTISEMENT
Baadaye ndege hiyo iliruhusiwa kuondoka Dar es Salaam saa 10.00 jioni na ilifika salama. Umbali kutoka Dar es Salaam hadi Mbeya kwa njia ya anga ni kilomita 672 na kwa barabara ni kilomita 828.
Mmoja wa abiria waliokuwamo kwenye ndege hiyo, Joseph Mbilinyi, ambaye ni mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), alisema waliondoka Dar es Salaam saa 1.00 asubuhi na Mbeya walifika saa 2.15 asubuhi. Alisema kabla ya kutua walikuta kuna ukungu mkubwa uliaombatana na mvua za rasharasha na kufanya ndege hiyo kushindwa kutua.
“Wahudumu wa ndege walitutangazia kwamba tusiwe na wasiwasi kwani mafuta ya kurudi Dar es Salaam yapo ya kutosha. Tunawashukuru wahudumu wa ndege hiyo kwani walijitahidi sana kutuondoa hofu.
“Hakuna kilichoharibika tu zaidi ya ratiba kwani unapotoka huku unakwenda umepanga kufanya jambo fulani lakini kwa dharura hii imeshindikana,” alisema.
Kwa takriban wiki tatu sasa hali ya hewa ya mkoani Mbeya imekuwa ya mvua na mawingu, hali ambayo siyo nzuri kwa usafiri wa anga. Tayari Mamlaka ya Hali ya Hewa imeshatahadharisha kuhusu mvua kubwa katika kipindi hiki.
Powered by Blogger.