Walimu Mbeya waandamana

Mbeya. Zaidi ya walimu 150 wa shule mbalimbali mjini hapa jana waliandamana kuelekea katika ofisi ya mkurugenzi wa jiji kudai madeni ya fedha yaliyolimbikizwa kwa muda mrefu.
Walimu hao walitokea katika Ofisi za Chama cha Walimu (CWT), Wilaya ya Mbeya baada ya kutoridhishwa na maelezo ya Katibu wa CWT, Felix Mnyanyi kuhusu fedha zao. Hata hivyo, jitihada zao za kufika katika ofisi ya mkurugenzi ziligonga mwamba baada ya kujikuta wakiishia mikononi mwa polisi.
Walimu hao walizuiwa na polisi wakiwa wamebakiza mita chache kufika katika ofisi hiyo.
Mmoja wa askari alisikika akisema:
“Jamani kuandamana ni haki yenu, lakini leo hii ofisi ya jiji imezingirwa na polisi ili kulinda usalama zaidi kwani wafanyabiashara nao wamejazana mahakamani, hivyo hatujui hatima yao.
“Mkionekana pale mtadhaniwa ni wafanyabiashara, hivyo mtazua jambo lingine ni vyema muondoke,” alisikika askari huyo akiwaambia walimu hao.
Awali, wakiwa katika ofisi za CWT, mmoja wa walimu hao, Isaack Mwalwajo alisema wanataka kufika kwa mkurugenzi wa jiji ambaye ndiye mwajiri wao ili wakazungumze naye kwa kuwa hawana imani na chama chao.
“Tumewachagua viongozi ili mshughulikie matatizo yetu lakini hatuoni kitu chochote mnachokifanya, watu tunadai malimbikizo mengi... tukienda kwa mwajiri wetu tunajibiwa ovyo hata nyinyi viongozi wetu. Tunaomba mtueleze kama mmeshindwa kazi,” alisema mmoja wa walimu hao.
Mnyanyi alikiri kuwa wanadai Sh1.3 bilioni zilizotokana na malimbikizo mbalimbali tangu mwaka 2007.
“Nimewasikia kilio chenu, ni kweli mnadai fedha hizo na haya ni madeni ambayo yamehakikiwa.
Powered by Blogger.