DC awasimamisha kazi mgambo kwa kupokea rushwa

Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, mkoani Geita, Amani Mwenegoha amewasimamisha kazi mgambo wa Kata ya Igulwa baada ya kutuhumiwa kupokea rushwa na kuwaachia wahalifu.
Mwenegoha alifanya uamuzi huo baada ya Kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya kubaini kuwa, watuhumiwa walikiuka maadili na wamekuwa wakikamata watu bila kibali.
Pia imebainika kuwa, wakiagizwa kukamata wahalifu huwaachia baada ya kupokea rushwa.
Aliwataja mgambo waliosimamishwa kuwa ni Juma Makenzi, Kesi John, Bembenya Kumba na Wilson Kapango ambao hawaruhusiwi kufanya kazi wilayani hapo.
Mkuu huyo wa wilaya alisema adhabu hiyo ni fundisho kwa wengine wanaopenda kukiuka maadili ya kazi na kuongeza kuwa, mgambo wanatambulika kama askari halali na kuwataka wazingatie viapo vyao.
Aliwataka mgambo wote kuhakikisha kuwa, kama askari wa akiba ni lazima wafanye kazi kwa weledi kwa kulinda haki na mali za wananchi.
Pia, Mwenegoha alitoa wito kwa wakazi wa wilaya hiyo kutoa ushirikiano na ofisi yake pindi wanapoona watendaji wa Serikali wanakiuka maadili ya kazi zao ili wachukuliwe hatua stahili.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, mgambo waliosimamishwa kazi walikiri kupokea barua za kusimamishwa kufanya kazi.
Juma Makenzi alisema uamuzi wa Kamati siyo sahihi kwani hawakuitwa kujitetea na wamekuwa wakifanya kazi kwa kushirikiana na watumishi wa Mahakama na polisi.
Naye Bembenya Kumba alikana  kupokea rushwa katika tukio alilodai walishiriki wenzake watatu bila yeye.
Kumba alisema wenzake hao  walipokea Sh1 milioni huku katika kesi nyingine ya jinai walipokea Sh1 milioni na nyingine Sh200,000 katika kesi ya uhamiaji.
Naye Ofisa Mtendaji Kata ya Igulwa, Amos Abed alisema ametekeleza agizo la mkuu wa wilaya kwa kuwasimamisha kazi na kuongeza kuwa, wamekuwa na tabia ya kukamata watu bila kuhusisha ofisi yake na kusababisha malalamiko kutoka kwa wananchi na watendaji wa vijiji.
Mwisho
-
Powered by Blogger.