Wafuasi 30 wa CUF wapata dhamana Kisutu


Wafuasi wa Chama cha Wananchi CUF, wakiwa katika chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. Picha na Maktaba 
Dar es Salaam. Wafuasi 30 wa Chama cha Wananchi CUF wanaokabiliwa na    mashtaka matatu ya kula njama na kukaidi  amri halali ya polisi na kufanya maandamano katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wameachiwa huru  baada ya kukamilisha masharti ya dhamana waliyopewa.
Hakimu  Mkazi, Emillius Mchauru jana aliwaachia huru washtakiwa  hao  baada ya  kukamilisha masharti ya dhamana  ya  kila mshtakiwa kuwa  na mdhamini mmoja anayeaminika na  kila mdhamini asaini hati ya dhamana ya maneno ya Sh 100,000.
Baada ya washtakwia hao kukamilisha masharti hayo ya dhamana, Hakimu aliiahirisha kesi hiyo hadi Februari 12,2015 kwa ajili ya kuangalia kama upelelezi utakuwa umekamilika ama la.
Juzi, Mawakili wa Serikali, Joseph Maugo na Hellen Mushi,  katika shtaka la kwanza alidai  kuwa Januari 27,2015 katika eneo la Temeke  washtakiwa hao  kwa pamoja walikula njama  ya kufanya uhalifu.
Akisoma hati hiyo ya mashtaka, Maugo katika shtaka la pili alidai kuwa  siku hiyo ya tukio, washtakiwa 28 kati ya 30 wanaokabiliwa na kesi hiyo, wakiwa katika ofisi ya CUF  karibu na Hospitali ya Wilaya ya Temeke bila ya kuwa na uhalali walifanya  mkusanyiko kwa nia ya kufanya maandamano kuelekea  Mbagala Zakhem.
Katika shtaka la tatu,  ambalo nalo pia linawakabili washtakiwa 28 kati ya 30 , Wakili huyo wa Serikali, Maugo alidai kuwa siku hiyo hiyo ya tukio katika eneo la Mtoni Mtongani waligoma na kutojali  tangazo halali lililotolewa na polisi lisilowaruhusu kuandamana  na hata kufanya mkusanyiko usio halali.
Washtakiwa wanaokabiliwa katika kesi hii ni  Shabani Ngurangwa (56), Shabani Tano(29), Shabani  Abdallah (40), Juma Mattar (54), Muhamed Kirungi (40), Athuman Ngumwai (40), Shaweji Mohamed(39), Abdul Juma(40), Hassan Said (37), Hemed Joho (46) na  Mohamed Ibrahim (31).
Pamoja na  Issa Hassan (53), Allan Ally(53), Kaisi Kaisi (51), Abdina Abdina (47), Allawi Msenga (47), Mohamed Mtutuma (33), Salehe Ally (43), Abd Hatibu (34), Bakari Malija (43), Abdallah Ally(32) , Said Mohamed (40), Salim Mwafisi, Salehe Rashid (25), Abdallah Said(45),Rehema Kawambwa (47), Salma  Ndewa (42), Athuman Said (39).
Kwa upande wa washtakiwa  Dickson Leasson (37) na Nurdin Msati (37) wao hawahusiki katika shtaka la pili na tatu ambayo yanawakabili wenzake.
Powered by Blogger.