Ukawa kujadili mustakabali wa siasa nchini leo

 Dar es Salaam. Wenyeviti wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), leo watakutana kwenye mkutano wa faragha kwa ajili ya kujadili ajenda mbalimbali zinazohusu mustakabali wake na hali ya kisiasa nchini.
Wenyeviti hao, Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia (NCCR Mageuzi), Emanuel Makaid (NLD) na Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) wanakutana kwenye mkutano huo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kalenda ya Ukawa.
Juhudi za kuwapata viongozi hao ili kuthibitisha ziligonga mwamba lakini Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi Bara, Mosena Nyambabe alisema jana kuwa mkutano huo utafanyika kama ilivyopangwa.
“Ninachofahamu mkutano huo lazima utafanyika lakini siwezi kujua utafanyikia wapi kwa hapa Dar es Salaam kwani ratibu zote wanazifahamu viongozi wenyewe,” alisema Nyambabe.
Awali, Mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia alimwambia mwandishi kuwa mkutano huo utakuwa na ajenda mbalimbali likiwamo suala la kuangalia mgombea wa nafasi ya urais kupitia umoja huo.
Ajenda nyingine alizotaja ni kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa, changamoto ya uandikishaji wa Daftari la Mpigakura, hali ya uchumi na tathmini ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliomalizika mwishoni mwa mwaka jana.
Mbatia alisema: “Ajenda hizo tunazijadili na lengo ni kuhakikisha tunatafuta majibu ya changamoto mbalimbali zilizopo kwa sasa,” alisema na kuongeza:
“Kuhusu suala la mgombea urais wa Ukawa, linaweza kuwa sehemu ya mazungumzo lakini halipo kwenye ajenda.”
Mbali na ajenda hizo, mwongozo wa umoja huo imekuwa ni jambo linalodaiwa kuwa changamoto katika utekelezaji wake. Kuhusu maandalizi ya mwongozo wa umoja, Mbatia alisema suala hilo pia litakuwa sehemu ya ajenda hizo.
Powered by Blogger.