Mafuriko yaikumba Mtwara, nyumba 200 zazingirwa na maji, RC atoa saa 24 yaondolewe



 




Wakazi wa Mtaa wa Kiangu Manispaa ya Mtwara Mikindani wakipita kwenye maji  kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humo. Picha na Haika Kimaro
Mtwara. Zaidi ya nyumba 200 zimezingirwa na maji katika Manispaa ya Mtwara Mikindani kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha na kusababisha hasara kubwa ambayo thamani yake bado  haijajulikana.
Kufuatia  hali hiyo Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Halima Dendegu ametoa saa 24 kwa wataalam kuhakikisha wanayaondoa maji ndani ya makazi ya watu.
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Wilaman Ndile amemwambia mkuu huyo wa mkoa alipotembelea maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko hayo kuwa zaidi ya nyumba 200 zimezingirwa na maji katika mitaa mbalimbali ya manispaa hiyo.
Alisema kuwa hakuna mtu aliyeripotiwa kupoteza maisha kutokana na mafuriko hayo lakini kumetokea uharibifu mkubwa wa mali na vyakula.
 “Mvua kubwa zilizonyesha jana usiku zimeshababisha mafuriko haya…tatizo kubwa mji wetu hauna mifereji ya kupeleka maji baharini…athari ni kubwa sana,” alisema Ndile.
ADVERTISEMENT
Aliongeza kuwa “Mitaa ya Magomeni, Chuno, Kiangu, Skoya,Kisutu Nabwada ndiyo yaliyoathiriwa zaidi na tatizo hili”
Alia Mussa ni mmoja wa waathirika wa mafuriko hayo kutoka Mtaa wa Kisutu eneo la Nabwada alisema kuwa amepoteza fedha kiasi cha Sh300,000, nguo, chakula na vyombo vya ndani.
“Tunaomba msaada kwa viongozi kunusuru hali hii, tunaona serikali yetu kama imetutupa, hatuna chakula, wala fedha za kununua chakula, kila kitu kimeloa,” alisema Mussa.
Dendegu amewaagiza wataalam wa mipango miji, zimamoto na manispaa kuhakikisha ndani ya saa 24 wanayaondoa maji hayo katika ya makazi ya watu.
Powered by Blogger.