Madiwani walaani jaribio la kumuua mkurugenzi

Singida. Madiwani wa CCM wilayani Iramba wamelaani vikali jaribio la kutaka kuuawa kwa bomu mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba.
Mkurugenzi huyo, Halima Hanjali Mpita alinusurika baada ya kitu kilichokuwa kwenye bahasha kulipuka kitandani kwake wakati akijiandaa kutoka. Bahasha hiyo alipewa na katibu muhtasi wake ikiwa na kadi ya pongezi iliyopelekwa ofisini kwake na watu wasiojulikana.
Jana, madiwani hao pamoja na kulaani kitendo hicho, wameomba Polisi kuwasaka na kuwakamata wote waliohusika na njama hizo na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi, katibu wa madiwani wa CCM ambaye anatoka Kata ya Urughu, Simon Tyosela alisema umoja wao ulitoa tamko hilo kwenye kikao kilichofanyika Alhamisi iliyopita.
“Kwa ujumla sisi madiwani wa CCM tupo pamoja na mkurugenzi wetu Halima Mpita na vilevile watendaji wote. Kwa umoja huo sote kwa pamoja tutaendeleza gurudumu la maendeleo ya wilaya ya Iramba,” alisema.
Aidha, Tyosela ameiomba polisi pamoja na kufanya uchunguzi wa jaribio hilo, ichunguze kwa kina ujumbe aliopewa mkurugenzi huyo kwamba amedhulumu Sh90 milioni kutokana na ‘dili’ walilofanya pamoja ili ukweli ufahamike.
Katibu huyo alisema wananchi wanataka kufahamu kwa kina suala hilo.
na hatua za kisheria zitakazochukuliwa dhidi ya watuhumiwa watakaokamatwa kuhusika na jaribio hilo na juu ya ‘dili’ la shilingi 90 milioni.
Katika hatua nyingine,Tyosela alisema madiwani wa chama tawala hawafurahishii wala hawapendezwi na msuguano uliopo kwenye halmashauri hiyo wa watendaji kwa watendaji na watendaji na mkurugenzi wao.
“Kuna uvumi kwamba baadhi ya watendaji wanataka kuomba kuhama kwa madai kwamba sisi madiwani hatuwapendi.Hapana sisi tunawapenda sana watendaji wetu na hatupo radhi kuona mtendaji ye yote anahama kutokana na misuguano ya ndani kwa ndani ambayo haina tija kwa wananchi wa wilaya ya Iramba.
Powered by Blogger.