Mwijage: Sikushtuka, sikubabaika


Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage
Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage amesema hakushtuka wala kubabaika Rais Jakaya Kikwete alipomwambia kuwa anataka ampe kazi katika wizara hiyo, badala yake alifurahi kupewa kazi anayoielewa.
“Haikunishtua kwa sababu naijua hiyo sekta, nimeingia nishati tangu mwaka 1984 na ninafahamu mambo mengi. Ninachoweza kuwaahidi wananchi ni kuwa, nitafanya kazi,” alisema Mwijage.
Waziri huyo mpya alisema jana kuwa, miongoni mwa mambo atakayoyafanyia kazi kwa nguvu ni kubuni njia za kuzalisha umeme nchi nzima.
Pia, alisema atahakikisha mafuta yanapatikana kwa bei nzuri na kwa viwango vinavyotakiwa.
“Nimepewa kazi, nitamsaidia kazi waziri, kwa kifupi nimewekwa kitengo ninachokiweza,” alisema
Mbunge huyo wa Muleba Kaskazini alisema hadi kufikia Machi mwaka huu, gesi itakuwa imefika Dar es Salaam na kuzalisha umeme kwenye gridi ya Taifa, hivyo nchi itakuwa na umeme wa kutosha.
“Si kwamba tumeanza leo, suala la gesi ni la mchakato kwa sababu tulishaanza kulifanyia kazi muda mrefu,” alisema.
Akizungumzia changamoto za wizara hiyo likiwamo suala la mikataba mibovu, alisema kuzungumzia changamoto za nyuma ni sawa na kufukua makaburi, hivyo anachokifanya ni kuendelea na kazi iliyo mbele yake. Naibu Waziri mpya wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anna Kilango Malecela alipopigiwa simu ili azungumze, alisema anaingia darasani na kutaka apigiwe simu baadaye, lakini alipopigiwa simu iliita bila kupokewa.Naibu Waziri wa Sheria na Katiba, Ummy Mwalimu ambaye alihamishwa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), alimshukuru Rais kwa kuwa na imani naye kumweka katika wizara hiyo yenye masuala nyeti ya kikatiba na kisheria.
“Nitasaidiana na Migiro katika Wizara ya Sheria na Katiba, kazi ambayo ina changamoto nyingi hasa katika wakati huu ambao Taifa linakwenda katika mchakato wa Katiba mpya,” alisema.
Alisema atatumia uwezo, uadilifu, juhudi na taaluma yake kuhakikisha kila kitu kinakwenda kisheria huku akitolea mfano masuala atakayoyafanyia kazi kuwa ni sheria kandamizi na sheria ya ndoa inayoruhusu wasichana wenye umri mdogo kuolewa.
“Tulianza kuifanyia kazi sheria hii wakati nipo Wizara ya Jinsia, Wanawake na Watoto na kwa sasa nitaifanyia kazi vizuri zaidi katika upande huu wa Wizara ya Katiba na Sheria,” alisema.
Powered by Blogger.