Muswada wa Kadhi balaa, Jukwaa la Wakristo laupinga


Dar/Dodoma. Wakati mjadala mkali ukitarajiwa kuibuka katika Mkutano wa 18 wa Bunge unaoanza leo kuhusu uanzishaji Mahakama ya Kadhi, Jukwaa la Wakristo Tanzania limeitaka Serikali kuachana na muswada huo ili kuepusha kuvunja misingi ya Taifa inayopinga ubaguzi na kutofungamana na dini yoyote.
Suala la kuanzisha Mahakama ya Kadhi limo katika Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali unaotarajiwa kuwasilishwa bungeni wiki ijayo na unalenga kufanya mabadiliko katika Sheria ya Tamko ya Sheria za Kiislamu Sura ya 375 ili suala hilo litambuliwe kisheria.
Endapo muswada huo ambao tayari umechambuliwa na wadau utapitishwa, katika sheria hiyo kutafanyika marekebisho kwenye kifungu cha tatu baada ya maneno ‘all courts’ (Mahakama zote) wataongeza maneno ‘including Kadhi Courts’ (Ikijumuishwa na Mahakama ya Kadhi).
Hata hivyo, Jukwaa la Wakristo linaloundwa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste nchini (CPCT) limesema mapendekezo hayo “yanaibua mambo mazito ya kikatiba ambayo hayawezi kuamuliwa na Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali na sheria hiyo itawaathiri hata wenye imani tofauti.”
Tamko la Jukwaa hilo lililokutana Januari 20 kujadili uanzishwaji wa mahakama hiyo ni mtihani kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye Septemba 29, mwaka jana katika mkutano wa Bunge la Katiba aliahidi kuliwasilisha suala hilo katika mkutano wa Bunge unaoanza leo ili kuanza mchakato wa uanzishwaji wa chombo hicho.
Pinda alitoa ahadi hiyo kuwapoza wajumbe wa Bunge hilo kutokana na baadhi yao kuhamasishana kuipigia kura ya kukataa Rasimu ya Katiba, iwapo chombo hicho kisingeingizwa katika Katiba.
Pinda aliahidi ifikapo Januari 2015, Sheria ya Mahakimu, sura ya 11 na Sheria ya Kiislamu sura ya 375 zitafanyiwa marekebisho ili kutambua Mahakama ya Kadhi kwa lengo la kuhakikisha umoja na mshikamano vinadumu kwa Watanzania.
Wapingwa katika Kamati
Uanzishwaji wa mahakama hiyo pia uliibua mvutano mkali katika vikao vya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala wiki iliyopita na wajumbe walisema uwezekano wa kuanzishwa kwake ni mgumu.
Katika vikao hivyo, ilielezwa kuwa kati ya wadau 15 kutoka taasisi za dini, wanaharakati, wanasiasa, wanasheria na wasomi waliofika mbele ya kamati hiyo, ni mdau mmoja tu aliyekubali kuanzishwa kwa mahakama hiyo.
Miongoni mwa wadau hao ni; Islamic Propagation Centre (IPC), Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, CCT, TEC, Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania.
Wengine ni Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (BMKT), Mwakilishi wa Kanisa la Wasabato (SDA),  Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Profesa Abdallah Safari na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata).
Tamko la Jukwaa
Katika tamko lake, Jukwaa wa Wakristo limetoa hoja nane likieleza kuwa ni mapendekezo makubwa yatakayokuwa na athari kubwa na nzito kwa kuwa yanahoji msingi wa dola ya Tanzania kama dola isiyokuwa ya kidini.
Sababu nane
Kwanza, licha ya sababu na madhumuni ya muswada huo kuwa ni kutambua Mahakama ya Kadhi, kwa utaratibu wa sasa wa kisheria, Mahakama za Kadhi hazipo.
“Kwa maana hiyo, hoja ya kutambua uwepo wa mahakama hizo si sahihi. Kama inavyofahamika, Mahakama za Kadhi, pamoja na Mahakama za Wenyeji (Native Courts), zilizokuwapo wakati wa ukoloni, zilifutwa na Sheria ya Mahakama za Mahakimu ya mwaka 1963.  Tangu wakati huo, mahakama hizi hazipo na hazitambuliwi na sheria yoyote na mapendekezo ya muswada huu yakipitishwa ndiyo yatazianzisha.”
Pili, kwa mapendekezo hayo, ni wazi kuwa Serikali inachukua jukumu la kuanzisha yenyewe taasisi za kidini kinyume na utaratibu wa kikatiba na Serikali imekuwa haijishughulishi na uanzishwaji na uendeshaji wa taasisi za kidini.
“Sheria ya tamko la Sheria za Kiislamu (Inayorekebishwa) haikuanzisha mahakama au taasisi nyingine yoyote ya kusimamia sheria hiyo bali iliweka utaratibu wa mahakama za kawaida kuitambua na kuisimamia sheria hiyo.”
Tatu, mapendekezo hayo yanampa Waziri Mkuu mamlaka ya kutunga kanuni za utekelezaji wa uamuzi, hukumu na amri za Mahakama za Kadhi.
“Kwa maana hiyo dola ya Tanzania, siyo tu inakusudia kuanzisha mahakama ya kidini, bali pia kuweka utaratibu wa kutekeleza uamuzi, hukumu na amri za mahakama hizo.”
Nne, mapendekezo hayo yanafuta utaratibu ambao umekuwepo kwa zaidi ya miaka hamsini, ambao unatambua matumizi ya sheria za dini zisizokuwa za Kikristo katika masuala ya hadhi ya mtu, mirathi, ndoa na talaka kwa mujibu wa Sheria ya Ndoa, Mirathi na Talaka.
Tano, kwa mapendekezo ya muswada huo, hakuna uhakika kama mamlaka za mahakama za sasa za kusikiliza na kuamua masuala ya hadhi ya mtu, mirathi na ndoa kwa mujibu wa Sheria ya Tamko la Sheria za Kiislamu itaendelea kuwapo.
“Aidha mapendekezo ya muswada huu yako kimya juu ya uhusiano wa Mahakama za Kadhi na mahakama za kawaida. Kwa mfano, haieleweki kama kutakuwa na utaratibu wa rufaa, marejeo na mapitio ya uamuzi wa mahakama hizo…”
Sita, mapendekezo hayo yako kimya juu ya kesi zinazohusu Waislamu na watu wa imani nyingine, kwamba hata kwa wadaiwa ambao ni Waislamu, ikiwa upande mmoja (mdai) unakwenda kwa hiari ila upande mwingine (mdaiwa) unataka shauri lisikilizwe na mahakama ya kawaida, muswada hautoi jibu nini kifanyike.
Saba, baadhi ya madhehebu na taasisi za Kiislamu hazikubaliani na mamlaka ya Mufti kwenye masuala yao, hivyo kumpa Mufti mamlaka ya kutunga kanuni zitakazotumika katika Mahakama za Kadhi na kuwateua makadhi, kunaweza kusababisha migongano na migogoro ndani ya jamii za Waislamu.
Nane, haturidhiki na hoja kwamba mahakama hizo hazitatumia fedha za umma.
“Mfano, Waziri atakapokuwa anatunga kanuni atatumia fedha na rasilimali mbalimbali za umma. Vilevile, utekelezaji wa amri na hukumu za mahakama hizi utahitaji polisi na madalali wa mahakama ambao wanalipwa kwa fedha za umma.”
Imeandikwa na Fidelis Butahe, Boniface Meena na Sharon Sauwa
Powered by Blogger.