BSS haijafa, sasa kuja kivingine- Madam Rita Poulsen

Akizungumzia changamoto zilizolikabili shindano hilo, Rita alisema: “Lakini ninashukuru kwa sasa zimeanza kupungua na tunafanya kazi vizuri, nisingependa kukumbusha changamoto zilizomalizika ila ifahamike ipo siku BSS itateka soko la Bongo Fleva, wasanii wote wakubwa utaona wana nembo ya BSS.”
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Jaji kiongozi wa mashindano ya kusaka vipaji vya muziki, maarufu BSS, Rita Poulsen amewataka mashabiki na wapenda muziki kuondoa hofu akieleza kuwa mashindano hayo hayajafa.
Mwaka jana mashindano hayo hayakufanyika tofauti na ilivyozoeleka.
Hali hiyo ilizua hofu miongoni mwa mashabiki kwamba huenda mashindano hayo yamekufa.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana Rita alisema kuwa licha ya shindano hilo kuchelewa kuanza katika msimu huu, litafanyika na kwamba mipango inakamilishwa.
“Najua Watanzania wana hamu ya kushuhudia msimu mwingine wa ukianza. BSS ni mapinduzi hasa kwa vijana nayo hayaishi kwa siku moja, lakini kwa sasa kuna mambo tunayaweka sawa, hadi mwishoni mwa Februari mipango itakuwa imekamilika,”alisema Rita.
Alibainisha kuwa amekuwa akipokea simu nyingi kutoka kwa wadau na wapenzi wa mashindano hayo wakihoji kuhusu kuchelewa kuanza kwa msimu mpya wa BSS.
Jaji huyo maarufu kwa jina la Madam Rita alisema kuwa kuanza kwa msimu kutakwenda sanjari na udhamini mpya.
Rita ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Benchmark, alidokeza kwamba udhamini wa awali wa Kampuni ya Zantel kwa BSS umekwisha muda wake na msimu mpya utakuwa na wadhamini wapya.
Alifafanua pia tayari kampuni mbalimbali zimeomba kudhamini shindano hilo ambalo hujumisha washiriki kutoka mikoa mbalimbali nchini na baadhi ya nchi za Afrika Mashariki.
BSS ilianza mwaka 2006 kwa kusaka vipaji vya vijana wa Kitanzania na kufanikiwa kuibua vipaji mbalimbali vya wasanii huku baadhi wakiendelea kufanya vizuri.
Baadhi ya wasanii walioibuliwa na BSS na wanaendelea kufanya vizuri ni pamoja na; Kala Jeremiah, Peter Msechu, Baby Madaha, Meninah, David Rogers, Pascal Casian na Walter Chilambo na Emmanuel Msuya.
Kuhusu majaji wa shindano hilo, Rita alisema yeye ataendelea kuwa jaji kiongozi akiwa na Master J na Salama Jabir.
“Timu ya ushindi itakuwa ni ile ile, mimi nitakuwapo, Master J na Salama. Niwaondoe hofu mashabiki na wanaotaka kuibua vipaji vyao katika muziki.”
Mshindi wa msimu uliopita wa BSS alikuwa ni Emmanuel Msuya, huku wa msimu wa kwanza katika mashindano hayo mwaka 2007 akiwa Jumanne Iddi.
Mshindi wa msimu uliopita katika shindano hilo lililojulikana kwa jina la Epic Bongo Star Search alizawadiwa kitita cha Sh50 milioni, huku msindi wa msimu wa kwanza akizawadiwa gari.
Akizungumzia changamoto zilizolikabili shindano hilo, Rita alisema: “Lakini ninashukuru kwa sasa zimeanza kupungua na tunafanya kazi vizuri, nisingependa kukumbusha changamoto zilizomalizika ila ifahamike ipo siku BSS itateka soko la Bongo Fleva, wasanii wote wakubwa utaona wana nembo ya BSS.”
Aliongeza: “Haya ni mapinduzi subiri kidogo utakuja kuniambia,sitakata tamaa kwani mapinduzi hayafanyiki siku moja, sifanyi kwa manufaa ya kupata jina wala fedha ila ni kubadilisha maisha ya vijana kupitia vipaji vyao.”
Ritha alisema mbali na kutafuta vipaji mikoani wamekuwa wakitoa elimu ya vijana kujitambua na athari za magonjwa mbalimbali ikiwamo maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.-
Powered by Blogger.