Majambazi yateka kituo cha polisi, yaua askari wawili, yapora SMG tano


Bunduki hizi sizo zilizoibwa na watu hao wanaoshukiwa kuwa ni Majambazi. Picha na Maktab
Rufiji:WATU 15 wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wakiwa na silaha za kivita na mabomu ya kurushwa kwa mkono wamevamia kituo cha polisi Ikwiriri  wilayani Rufiji Mkoani Pwani na kuua askari polisi wawili na kupora silaha tano za SMG na mbili za kufyatulia mabomu ya machozi zilizokuwepo kituo hapo na kutokomea kusikojulikana.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Ulrich Matei amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa majambazi hao wamefanikiwa kuchukua silaha tano za moto na mbili za mabomu ya machozi zilizokuwepo  kituoni hapo.
Amesema polisi wawili Koplo Edga na WP Judith wamethibitika kuuawa na majambazi hao katika tukio hilo na kwamba jitihada zinaendelea kuwatafuta waliohusika na tukio hilo.
Habari zilizopatikana eneo la tukio zimesema kuwa majambazi hao walivamia kituo hicho saa mbili usiku  na kuwakuta maofisa hao wa polisi wakiwa katika zamu ya usiku bila kuwaeleza chochote wakaanza kuwashambulia kwa risasi.
Majina ya polisi waliouawa yametajwa kuwa ni koplo  Edgar na askari wa kike Judith ambao walipigwa risasi .
Mmoja wa wakazi wa mji wa Ikwiririi Arafa Ngwaya amesema usiku wa kuamkia jana kulisikika milio kadhaa ya risasi na milipuko ya mabomu lengo likiwa ni kutisha wananchi na polisi kutotoka nje kutoa msaada wakati wa utekelezaji wa shambulio hilo. 
“Tumepatwa na taharuki kubwa katika tukio hili na inaonekana hawa jamaa walijizatiti vilivyo, Polisi kwa kutumia vitengo vyetu mahususi vya upelelezi tunaendelea kufanya uchunguzi, pia tunawaomba raia wema ambao wana taarifa zozote za majambazi hao watufahamishe”alisema Kamanda Matei.
Powered by Blogger.