Mimi ni waziri, nina haki zangu, ajitetea Wasira


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira amesema yeye ni waziri na ana haki zake, baada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kumtaka aachie nyumba anayoishi ya Bodi ya Sukari kwa kuwa haimuhusu kwa sasa.
Juzi, PAC iliiagiza Bodi ya Sukari Tanzania (SBT) kumwandikia barua ya kumtaka mwanasiasa huyo mkongwe aondoke kwenye nyumba ya bodi hiyo iliyopo Masaki jijini hapa, aliyoishi tangu akiwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika na iwapo haitawezekana, aanze kulipia tozo ya pango.
Hata hivyo jana, Wasira aliiambia gazeti hili kuwa hawezi kujibizana na PAC kwa kutumia magazeti na kwamba kama kuna maagizo yoyote yametolewa, kipo chombo kitakachoshughulikia.
“Mimi ni waziri nina haki zangu, PAC haihusiki na mtu binafsi wala siyo ofisa mahesabu. Kwa nini unaniuliza mimi, si uwaulize PAC?” alihoji Wasira.
Akijibu maelezo hayo ya Wasira, mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe alisema jana kuwa kamati yake haina nia ya kumshambulia waziri huyo kwa kuwa ana haki ya kupewa nyumba na Serikali.
Alisema iwapo Serikali bado inataka waziri huyo aendelee kukaa kwenye nyumba hiyo, ilipe kodi na kama ikishindwa wampe nyumba nyingine.
“Hapa suala siyo mzee Wasira binafsi, ni Serikali kukaa kwenye nyumba ya umma isiyolipia kodi,” alisema Zitto. Aliongeza kuwa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ndiyo iliyobaini kuwa nyumba hiyo hailipiwi kodi na kuitaka irejeshwe kwa Bodi ya Sukari.
Powered by Blogger.