Kitabu cha ‘urais’ wa Makamba


Dar es Salaam. Ni dhahiri mpambano wa kuwania urais ndani ya CCM unazidi kunoga, ikiwa imebakia miezi michache kabla ya kupulizwa rasmi kipenga.
Mmoja wa makada kutoka CCM waliotangaza nia ya kuwania kiti hicho, January Makamba ameandikiwa kitabu kinachoeleza nia yake hiyo.
Kitabu hicho pamoja na mambo mengine kinaeleza mikakati ya mwanasiasa huyo kijana iwapo atapitishwa na chama chake ili kuwania na hatimaye kushika nafasi hiyo ya juu ya uongozi kitaifa.
Katika kitabu hicho chenye kurasa 196, Makamba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Mbunge wa Bumbuli, Tanga anasema rais ajaye lazima awe na tafakuri pana na nia ya kuendeleza nchi na siyo kuwa na kaulimbiu nyepesi za afya bure, elimu bure zisizo na ufafanuzi ili kuwahadaa wananchi.
Kitabu hicho kilichoandikwa na mchambuzi na mwandishi wa makala za siasa, Padri Privatus Karugendo kimebeba sera na mikakati yake kiundani ya kuiongoza nchi iwapo atapatiwa dhamana na CCM kugombea urais.
Katika kitabu hicho kinachoitwa, ‘Maswali na Majibu 40: Mazungumzo na January Makamba kuhusu Tanzania Mpya’, mwanasiasa huyo anasema uongozi hauishii kwa kauli za juu juu za kuongeza ajira, kuboresha elimu kwani kila mtu anaweza kuyasema hayo.
Anamwonaje rais ajaye
Anasema katika tafakuri zake anaona rais ajaye anatakiwa kuzitambua kwa kina changamoto za nchi yake na kuwa na mikakati ya kuzitatua.
Changamoto hizo, Makamba anasema ni za kiuongozi na utatuzi wake unategemea kiongozi mwenyewe, hulka, mtazamo wake na usahihi wa uamuzi anaoufanya.
“Kuomba uongozi wa nchi siyo harakati binafsi na wafuasi wako kupata vyeo. Ni dhamana kubwa ya kujenga mustakabali wa nchi na kuwaunganisha Watanzania wote. Kwa hiyo, uamuzi wa kugombea lazima uupe heshima na nafasi inayolingana na dhamana yenyewe,” anasema Makamba kwenye kitabu hicho.
Anaongeza kuwa rais anatakiwa kuongeza kasi ya kuondoa umaskini, kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali, vyombo vya dola na mahakama na hayo yatadhihirika kwa vitendo vya kuchukua hatua dhidi ya viongozi wabadhirifu, walarushwa na kudhibiti matumizi ya Serikali.
Pia, Makamba anatumia fursa hiyo kuelezea mikakati yake kuhusu kutatua matatizo ya elimu, kusimamia muungano, umoja, mshikamano na upendo, kukuza ujasiriamali, umilikaji wa ardhi na unufaikaji wa rasilimali kwa wananchi na jinsi alivyo tayari kuboresha hali hiyo.
Hoja ya ujana
Mwanasiasa huyo aliyeingia kwa mtazamo wa uongozi wa kizazi kipya, anapoulizwa na mwandishi wa kitabu kuhusu mjadala kuhusu umri na urais na kwa nini vijana waaminiwe kwa nafasi hiyo wakati hawana uzoefu, anajibu kuwa haamini kuwa umri pekee ni sifa ya uongozi.
“Siamini kwenye dhana kwamba ukiwa mzee unafaa na ukiwa kijana hufai, au ukiwa mzee hufai na ukiwa kijana unafaa. Ujana si sifa na uzee si kashfa. Ujana si kashfa na uzee si sifa,” anasema.
Anabainisha kuwa wanapokubaliana umri si kigezo, maana yake ni kwamba mwenye miaka 40 asionekane hawezi kutokana na miaka yake, lakini anaongeza kuwa uongozi ni suala la rika. Anasema kila rika au kizazi kina wakati wake, wajibu wake na ndiyo maana Mwalimu Julius Nyerere aliamua kung’atuka urais akiwa na miaka 62 na siyo kwa kushindwa kuongoza, bali kwa ajili ya kuachia rika na kizazi kingine kiendeleze alipoishia.
“Uongozi ni kutengeneza kesho njema. Wenye kesho nyingi hawapaswi kukaa pembeni na kukunja mikono na kuwaachia wenye jana nyingi kazi ya kujenga kesho njema. “Wakifanya hivyo, uhakika wa kesho njema unaweza usiwe mkubwa kwa sababu wenye jana nyingi wanaweza kuhangaika na masaibu ya jana zao kuliko matumaini ya kesho,” anasema.
Uzoefu wa JK
Makamba aliyewahi kuwa mwandishi wa hotuba wa Rais Jakaya Kikwete, anasema ushiriki wake katika kampeni za urais mwaka 2005, akiwa msaidizi wake na baadaye kufanya naye kazi Ikulu, ulimpatia uzoefu mkubwa uliosadia kuyajua matatizo yanayowakabili Watanzania karibu kila eneo la nchi.
“Nilijifunza pia kwamba matumaini wanayowekeza Watanzania kwa viongozi wao ni makubwa na pale tunapowaangusha kwa kweli tunatenda makosa.
“Nilijifunza kwa Kikwete kwamba unaweza kuomba kura, kuelezea dira yako, fikra zako, sera na ilani ya chama chako bila kutumia matusi, kejeli, ulaghai na lugha kali na bado ukafanikiwa,” anasema Makamba katika kitabu hicho.
Anaongeza kuwa alipokuwa msaidizi wa JK wa kuandika hotuba, alijifunza namna Serikali inavyoendeshwa kwa kuhimili msisukosuko wakati wa vipindi vigumu na jinsi kiongozi wa juu anavyotakiwa kutotetereka.
Kwa mujibu wa Padri Karugendo, kitabu hicho ni sehemu ya mradi walioubuni wa kutaka kuwafahamu vijana, hasa wale waliochomoza kwenye medani za siasa na kushika nafasi za juu za uongozi serikalini wakiwa na umri mdogo na kiu ya kuleta mabadiliko katika nchi.
Anasema Karugendo kuwa wataendelea kuuliza maswali kwa kila kijana kutokana na umri wake na kwamba iwapo anayo miaka 40, basi ataulizwa maswali 40, vivyo hivyo kwa yule mwenye miaka 55 au zaidi.
Katika maswali hayo ya kichokozi, Makamba aliulizwa na Padri Karugendo kuwa haoni kuwa CCM imepoteza mwelekeo na inapata upinzani mkubwa na iwapo kuna sababu ya kuendelea kuaminiwa na Watanzania?
Katika majibu yake, Makamba anasema ni kweli ushindani umeongezeka na kwamba hali hiyo si ya ajabu kwa kuwa ndani ya miaka 22 ya mfumo wa vyama vingi ni lazima ushidani ungetokea, ila anapinga kuwa CCM imepoteza mwelekeo.
Anasema zipo changamoto kadhaa zilizo kawaida kwa kila taasisi ambazo zitatatuliwa kwa kuwasemea na kuwatetea wanyonge, kukemea rushwa na maovu katika chama chenyewe na kutekeleza ilani na ahadi za CCM.
“Ni kweli kwamba chama kimeingiliwa na wajanja wachache ambao wanataka kununua uongozi kwa ajili ya kujinufaisha.”
Makamba, katika kitabu hicho ambacho dibaji yake imeandikwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi au Mzee Ruksa, anasema haoni mbadala wa CCM kwa sasa katika utayari wa uongozi wa Taifa na kwamba amani, utulivu, umoja na maendeleo na salama ya nchi ipo mikononi mwa CCM.
Akielezea namna ya kupunguza makali ya umaskini kwa kukuza uchumi na ajira kwa vijana, Makamba anasema kuna haja ya kuweka muswada maalumu wa matumizi kwa uwezeshaji kiuchumi kwa vijana, utakaokuwa sheria maalumu ya matumizi ya Sh3.6 trilioni kwa ajili ya miaka mitatu.
Anasema sheria hiyo itasaidia kupanua ajira kwa kuchochea shughuli za uzalishaji mali na uchumi, zikiwamo kutoa motisha kwa biashara kubwa na viwanda vitakavyoongeza ajira rasmi 50 za kudumu kwa mwaka, pia kupunguza kodi ya mshahara (PAYE).
Dibaji ya Mwinyi
Katika dibaji kwenye kitabu hicho, Mzee Mwinyi anasema Makamba anaonekana dhahiri ameandaliwa au amejiandaa vilivyo kuwa kiongozi mkubwa wa nchi.
Mzee Mwinyi anasema kitabu hicho kimemfanya amfahamu zaidi kiongozi huyo kuliko awali alipokuwa kama kiongozi ndani ya chama na Serikali.
“Fursa ya kusoma mazungumzo yake imenisaidia kumfahamu zaidi kama mtu, pia fikra zake,” anasema Mzee Mwinyi.
Anaeleza kufarijika kwake kuona nchi na Rais Kikwete wameendeleza utamaduni aliouanzisha Mwalimu Nyerere na kuendelezwa naye wa kuwaamini vijana na kuwapatia fursa za uongozi ili kuwaanda kuongoza nchi.
Kauli ya Makamba
Akizungumzia kitabu hicho, Makamba alisema jana kuwa kilichoandikwa na Padri Karugendo kinaakisi mawazo yake na kwamba amewasilisha vyema mazungumzo yao.
“Amefanya kazi nzuri na imechukua muda mrefu kama mwaka mzima hivi. Kuna kipindi nilikata tamaa kwamba kitabu hakipo, lakini hatimaye amekikamilisha,” alisema Makamba na kuongeza:
“Watu wanaotaka kunifahamu wakisoma kitabu hicho watanielewa January ni nani.”
Anahimiza wanasiasa wengine wafanye hivyo ili wananchi wawajue viongozi wao ili iweze kusaidia nchi kupata kiongozi bora.
“Wananchi wengi wanawajua viongozi wao kwa vyeo walivyoshika, lakini hawawajui kwa undani,”anasema.
Anapoulizwa kwamba haoni vipaumbele vilivyomo kwenye kitabu hicho vinapingana na zuio la CCM kwa wanachama wake kufanya kampeni za urais mapema, Makamba anajibu kuwa hivyo ni vipaumbele vya Tanzania mpya na havihusiani na kampeni.
“Siyo kampeni za mapema kwani ni fikra zangu katika kuboresha nchi na jamii yetu. Haiendani kinyume na taratibu za CCM, ambazo tumewekewa kwani haya ni mawazo yangu na ndiyo ninayoyaamini,” alisema Makamba.
Anasema ameyaweka mawazo yake kwenye mfumo wa pamoja, hivyo mtu yeyote atakayesema hiyo ni kampeni atakuwa anafanya siasa.
Powered by Blogger.