Nyumba 30 zabomolewa na mvua Mara


Mafuriko
Serengeti. Mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali, imesababisha nyumba zaidi ya 30 kuanguka, ng’ombe saba kufa katika vitongoji vya Maganana na Mgenda Msirori katika Kijiji cha Gusuhi, Kata ya Nyambureti Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.
Ofisa mtendaji wa kijiji hicho, Juma Kitorobo alisema jana kuwa mvua hiyo ya dakika tano, ilinyesha kijijini hapo mwishoni mwa wiki iliyopita na kusababisha madhara hayo makubwa.
Alisema mbali na mvua hiyo kusababisha uharibifu mkubwa, pia ilimjeruhi mtu mmoja, ambaye kwa sasa amelazwa Hospitali Teule ya Wilaya ya Serengeti.
“Madhara ni mengi baada ya mvua kubwa kunyesha, lakini kubwa ni kuharibika kwa nyumba nyingi na mazao kijiji hapa,” alisema Kitorobo.
Alisema nyumba 29, zikiwemo za nyasi 12 na bati 10, zilianguka kabisa, huku nyumba sita zikiezuliwa na ghala moja la vyakula kubomoka.
“Ng’ombe saba, mbuzi watatu walikufa kutokana na mvua hiyo, huku pia mazao yakiharibika,” alisema na kuongeza:
“Tukio hilo limeacha maswali kwa wananchi kwa kuwa mvua ilinyesha muda mfupi na upepo ulikuwa mkali kama kimbunga.”
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Maganana, Ndori Motiba alisema wanakijiji wamekubaliana kumjengea nyumba mwanakijiji mwenzao, Mgaya Motika ambaye mke wake amejeruhiwa vibaya wakati akijaribu kuwaokoa watoto wake kutoka kwenye nyumba ambayo iliangushwa na mvua hiyo.
“Mwenzetu hana makazi kutokana na mvua hii, lakini pia mke wake amejeruhiwa, hivyo tumekubaliana kumsaidia kujenga nyumba nyingine,” alisema.-
Powered by Blogger.