Wananchi Njombe wahofia kukosa kuandikishwa

Wananchi mkoani Njombe, wameanza kuwa na wasiwasi huenda wakashindwa kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, kutokana na kazi hiyo kufanyika taratibu kwa sababu ya uchache wa mashine za kuandikishia na kasi ndogo ya maofisa uandikishaji.
Katika Halmashauri ya Mji wa Njombe, ambako kazi hiyo wiki hii inafanyika katika vituo 31 vya kata tatu za Mjimwema, Yakobi na Kifanya, wakazi wa maeneo hayo wameanza kupiga hesabu ya kuhama vituo ili wakajiandikishe katika kata nyingine ambazo hazijaanza uandikishaji.
Mwandishi alishuhudia msongamano mkubwa wa watu katika Kata ya Mjimwema.
Wakizungumza na gazeti hili jana, baadhi ya wananchi waliokuwa wakijiandikisha katika vituo vya Nazareth, Joshoni, Mpechi na Mjimwema, walidai kuwa kazi hiyo haiwezi kukamilika wiki hii kama ilivyopangwa kutokana na kufanyika taratibu.
Imebainika kuwa mtu mmoja anatumia dakika 15 hadi 20 kuandikishwa, wameiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kuongeza muda zaidi ili kutoa fursa kwa wananchi wote waliojitokeza kuandikishwa katika daftari hilo.
“Mpaka leo (jana), bado wanananchi wengi hawajaandikishwa, unafikiria kazi hii itaisha Jumapili kama ilivyopangwa?” alihoji Emmanuel Kayombo mkazi wa Mtaa wa Joshoni.
Lucian Maarifa, alisema kwa kasi iliyopo katika uandikishaji huo, ni dhahiri kuwa haiwezekani kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa mwezi ujao.
“Serikali na NEC wasitufanye kama watoto wadogo, wanasema daftari hili litatumika katika kuipigia kura Katiba mwezi ujao, kwa kasi hii ni uongo, labda kama wameamua kugawa zawadi ya vitambulisho kwa wananchi,” alisema Maarifa na kuongeza: “Kama Njombe pekee inatumia siku nyingi hivi itakuweje kwenye mikoa yenye halmashauri zaidi ya moja?
“Kama itafika Jumapili sijaandikishwa nitahamia kata nyingine au nitaenda kijijini kwetu nikajiandikishe maana mjini watu wengi mno halafu mashine zenyewe chache,” alisema Rehema Mfugale.
Jana asubuhi, gazeti hili lilitembelea kituo cha Joshoni na kukuta watu 250 wakisukumana kwenye foleni, wote wakitaka kujiandikisha, wakati mashine zina uwezo wa kuandikisha watu 120 hadi 150 kwa siku.
Kitendo cha wananchi hao kusukumana kiliwafanya viongozi wa Tume kulazimika kuongeza mashine ya pili kwenye kituo hicho ili kazi iende haraka.
ADVERTISEMENT
Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe, Gideon Mwinami akizungumzia kazi hiyo, alisema wamekuwa wakikabiliana na changamoto nyingi ikiwamo ya BVR wakati mwingine kutoa picha au kutosoma vidole katika halmashauri zote tano ambako kazi hiyo inaendelea.
“Na Idadi ya wanaojiandikisha inaongezeka kila siku baada ya kuviona vitambulisho vya wenzao waliojiandikisha tayari,” alisema Mwinami.
Alisema tangu kazi hiyo ianze Machi 16 hadi 19, wameandikisha wakazi 48,743 kwa halmashauri zote tano za mkoa huo.
Alisema katika Halmashauri ya Mji wa Makambako ambako kazi hiyo imeshakamilika Machi 17, mwaka huu, wamefanikiwa kuandikisha watu 58,692.
Pamoja na wasiwasi wa Watanzania kuwa Daftrai hilo haliwezi kutumika kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa, jana Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu, Damian Lubuva alisema tarehe ya kuipigia kura Katiba iko palepale, Aprili 30, mwaka huu.
Alisema kama kutakuwa na mabadiliko, wananchi watajulishwa ila kwa sasa waiache Tume ifanye kazi yake.
“Nawaomba Watanzania watuache tufanye kazi yetu ya kuandikisha, waache minong’ono ya kwamba kuwa kazi hii haiwezi kukamilika nchi nzima kabla ya tarehe ya kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa,” alisema Lubuva na kuongeza:
“Huu siyo Msahafu lazima tuwe flexible (huru); la kwanza kwetu ni kuhakikisha kuwa Daftari hili linaboreshwa halafu mengine yatafuata yakiwamo hayo ya tarehe ya kuipigia kura Katiba na Uchaguzi Mkuu.
Lakini kwa sasa tarehe ile iliyopangwa haijabadilishwa, siku hiyo ikifika kazi hii haijakamilika nitasema kazi ya msingi sijakamilisha,” alisema Lubuva.
Alisema mfumo mpya huo wameanza baada ya kupata malalamiko mengi kutoka kwa wadau ambao ni vyama vya siasa, Serikali, asasi za kiraia na wapigakura katika chaguzi zilizopita.
Alisema walidai kuwa kuna watu walioandikishwa mara mbili, wengine wametimiza umri wa miaka 18 hawajaandikishwa na wengine kufariki dunia na baada ya kufanya utafiti wakaamua kuja na mfumo huo mpya wa Biometric Voters Registration (BVR) ili kumaliza tatizo hilo lililokuwa likilalamikiwa.
Powered by Blogger.