Ukatili: Mama amtesa mwanae na kumpa majeraha mengi mwilini....

Mwanamke mmoja mkazi wa Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam, Violet Manyondo (40) anadaiwa kumtesa na kumfanyia vitendo vya kikatili mtoto wake wa kumzaa, anayejulikana kwa jina la David (14).David ambaye ni mwanafunzi wa darasa la tano katika shule moja ya msingi iliyopo Mzambarauni, Dar kwa sasa haendi shule kutokana na majereha aliyonayo kiasi cha kuwaliza majirani.

Akizungumza na Amani,  mmoja wa majirani aliyeomba hifadhi ya jina lake, alisema ni mara yake ya kwanza kushuhudia  mama akimtesa  mtoto wake wa kumzaa kama anavyofanya mama huyo.
 
“Tunaomba vyombo vya haki za binadamu hata Jeshi la Polisi kushughulikia tukio hili haraka iwezekanavyo vinginevyo mtoto  huyo ataathirika kisaikolojia, halafu cha kushangaza, ana watoto watatu, lakini ni huyu tu ndiye anayekutana na kipigo,” alisema jirani huyo.
 
Alisema katika kumsaidia kijana huyo, wamewahi kwenda kituo cha polisi Gongo la Mboto, lakini polisi jamii walipokwenda nyumbani hapo, waliambulia matusi.
 
Mtoto David alimwambia mwandishi  kuwa ni kweli mama yake anamtesa kwa muda mrefu na kwamba hivi karibuni alikwenda kumshtaki katika kanisa lao liitwalo Universal Ufalme wa Mungu, Mzambarauni, Ilala, Dar na alipotakiwa kumwita mama yake alikataa kwenda.

“Baada ya mama kupata wito ule hata kanisani ameacha kwenda kwa kuhofia kikao na ushauri wa viongozi wa  kanisa. Sina cha kufanya wala pa kwenda, namuomba Mungu anisaidie nimalize shule,” alisema kijana huyo.
 
Kuhusu sababu za kuteswa, alisema hafahamu chochote, ingawa alihisi huenda ni kwa sababu ya baba yake kutopeleka hela ya matumizi nyumbani, kitu ambacho hata hivyo hafahamu kwani hamfahamu mzazi wake, zaidi ya kusikia kuwa ni dereva wa daladala.
 
Katika hali ya kushangaza, mama huyo alipotafutwa na mwandishi, alijibu kijeuri;
 
“Yule ni mwanangu, naweza kumfanya lolote lile. Mimi ni mzazi wake, natakiwa kumrekebisha kwa njia yoyote.”
Powered by Blogger.