Marufuku kuvuta sigara hadharani

 
> Mkazi wa jijini Dar es Salaam akiwasha sigara yake eneo la Buguruni Malapa.Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii jana imetoa agizo la kupiga marufuku uvutaji wa sigara kwenye maeneo ya umma.Picha na Edwin Mjwahuzi.
ADVERTISEMENT
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid amesisitiaza tamko la kupiga marufuku uvutaji wa sigara katika maeneo ya umma ili kuilinda jamii kutokana na madhara yatokanayo na moshi wa sigara.
Tamko la Waziri limekuja ikiwa ni siku moja tu baada ya maadhimisho ya Siku ya Kifua Kikuu Duniani, moja ya magonjwa yanayosababishwa na uvutaji wa tumbaku.
Agizo hilo limezingatia Sheria ya Usimamizi wa Bidhaa za Tumbaku, Sura ya 121 TL, ya mwaka 2003, Kipengele cha 12(1) ambacho kinakataza matumizi ya bidhaa hiyo katika maeneo ya umma.
“Agizo hili linawataka wananchi wanaotumia bidhaa za tumbaku, kupunguza au kuacha kabisa, pia linaijumuisha jamii yote kujua madhara ya matumizi ya tumbaku na umuhimu wa kuzuia uvutaji katika maeneo ya umma,” alisema Waziri katika tamko lake.
Uvutaji sigara ulianza kupigwa marufuku kwa mara ya kwanza mwaka 1575 na Kanisa la Katoliki lakini katika karne ya 20 harakati dhidi ya uvutaji sigara zilipamba moto kwa sababu za kiafya.
Sababu kubwa ya kupiga marufuku ni ukweli kwamba uvutaji sigara ni hiari wakati kuvuta pumzi ni lazima, hivyo mtu anayetumia kilevi hicho hana budi kukaa mbali ili kuepusha uwezekano wa kupata magonjwa kama ya moyo na saratani kwa wasiotumia na ambao kuvuta pumzi ni lazima.
Msemaji wa wizara hiyo, Nsachris Mwamaja alisema nia ya marufuku hiyo ni kuhakikisha wizara inatimiza kwa vitendo sheria hiyo ya bidhaa za tumbaku kwa kupiga marufuku na kuchukua hatua za kisheria. “Jamii itusaidie kutoa elimu katika hili, kuna suala la kujenga maeneo maalum ya kuvuta sigara na elimu kwa wale wanaovuta,” alisema.
Sheria ya usimamizi wa bidhaa za tumbaku ya mwaka 2003, inaeleza kuwa nia ni kuwalinda vijana wenye umri wa chini ya miaka 18 na wale wasiovuta wasishawishike kuvuta.
Kuwalinda wasiovuta wasipate madhara, kuifahamisha jamii juu ya madhara ya tumbaku na madhara ya kuvuta moshi wa sigara inayovutwa na mwingine na kuhakikisha jamii haina wavutaji sigara.
Maeneo ambayo yamepigwa marufuku kuvuta sigara yametajwa katika tamko hilo kuwa ni katika ofisi zote za serikali na taasisi zake, hospitali za umma, vyuo vikuu na shule za umma, vituo vya usafiri wa anga, mabasi, bandari na treni, bustani, fukwe na katika maeneo ya kupumzika ya umma.
Pia tamko hilo la wizara limekataza uvutaji wa sigara katika mikutano yote ya kiserikali.
“Wizara inawataka wale wote ambao wanataka kuacha kabisa kuvuta sigara, wawatafute wataalamu wa afya ili wapate ushauri wa kitaalamu,” alisema waziri katika tamko hilo.
Kadhalika, agizo hilo limewataka wafanyakazi wa sekta ya afya na watumishi wa umma kuhakikisha wanafanyia kazi na wanasimamia agizo hili.
“Tunataka kila mmoja ashiriki katika agizo hili la kuzuia bidhaa za tumbaku, sekta binafsi, asasi za kidini na wadau wengine wa afya watusaidie katika kufanikisha hili,” alisema Waziri
Wakati wizara ikitoa tamko hilo, Kampuni ya Sigara (TCCL) imekuwa moja ya kampuni zilizoongoza kwa kulipa kodi mwaka jana.
 
 
 
 
 
posted Wednesday, March 25, 2015 | by- Florence Majani
Powered by Blogger.