‘Asilimia 80 ya wabunge hawafai’

> Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa akifafanua jambo alipokuwa akifanyiwa mahojiano maalumu na waandishi na wahariri wa magazeti ya Mwananchi Communications Limited, alipotembelea ofisi za magazeti hayo Tabata Relini, Dar es Salaam jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
ADVERTISEMENT
Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa amesema zaidi ya asilimia 80 ya wabunge waliopo bungeni sasa hawakustahili kuwa wabunge kwa sababu baadhi yao wana uwezo mdogo kiakili alioulinganisha na GB moja ya kompyuta.
Msigwa alisema kwa maoni yake, ni asilimia 20 pekee ya wabunge ndiyo wenye uwezo na vigezo vinavyostahili kupata nafasi hiyo ya uwakilishi wa wananchi katika chombo hicho cha kutunga sheria.
Mchungaji Msigwa alikuwa akizungumza na wahariri alipotembelea ofisi za Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd inayochapisha magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti, Tabata Relini, Dar es Salaam jana.
Alisema wakati umefika kwa Taifa kuweka viwango maalumu vya kuwapata viongozi wa kisiasa wakiwamo wabunge na Rais.
“Tatizo kubwa Watanzania hatuna ‘standards’ (viwango) na vigezo tunavyoviweka kwa mtu anayetaka kuwa kiongozi, yaani tujue kuwa mtu anayekuja kuomba uongozi anapaswa awe mtu wa aina gani.
“Tutakuwa tunafanya makosa makubwa kama Taifa, ikiwa hatutakuwa na ‘standards’. Vinginevyo tutapata hata wasio na sifa ndiyo hawa wanaojitengenezea maandamano kwa kujifanya kuwa ni maarufu.”
Alisema kigezo kinachozingatiwa katika siasa ili kuwa mbunge cha kujua kusoma na kuandika hakitoshi na siyo sahihi, hivyo kinapaswa kitazamwe upya ili kupata wawakilishi watakaoweza kutimiza wajibu wao ipasavyo wakiwa watungaji wa sheria na watetezi wa rasilimali za Taifa.
“Tunaambiwa kigezo muhimu cha kuwa kiongozi akiwamo mbunge ni kujua kusoma na kuandika, hii siyo sahihi kwani kujua kusoma na kuandika pekee hakutoshi kuwa kigezo cha mtu kuwa mbunge au kiongozi,” alisema.
“Kujua kusoma na kuandika siyo kigezo cha kupitia vifungu vya sheria. Unajua kuna baadhi ya wabunge kutokana na upeo mdogo, mtu kama Tundu Lissu akiongea kule ndani (bungeni) hawaelewi, ndiyo maana unakuta wanaishia kumwona kama kichaa.
“Wabunge wengi hawamuelewi Tundu Lissu, kwa sababu vichwa vyao vina ‘GB’ moja za ubongo. Sasa ‘kucontain’ (kukusanya) mambo yote yale ya Bunge, kichwa kinapata moto na ili kupata majibu rahisi, wanasema ni (Lissu) kichaa, maana hawawezi kufikiri kiwango kile kutokana na akili yao kuwa ni ndogo sana,” alisema Msigwa bila kutaja majina ya wabunge hao.
Alisema mbunge anapaswa kuwa na uwezo wa kujieleza, kuelewa mambo, kusoma mambo mengi, akisisitiza kuwa kwa ilivyo sasa ni kama asilimia 20 ya wabunge wote, ndiyo wenye sifa na uwezo wa kujadili mambo.
“Wengi wao wamekaa kaa tu, hawawezi kusema lolote, wabunge wengine tunaposafiri nao, tunashuhudia mambo ya aibu tupu. Wengi wanakuwa kama mabubu, wamekaa kaa tu, hawasemi chochote, hawana michango yoyote, wanasubiri kufanya ‘shopping’ tu kana kwamba wamekwenda kwa ajili hiyo,” alisema Msigwa.
Alisema wapo wabunge ambao tangu walipochaguliwa hawaonekani kuwa na thamani kwani hawachangii lolote bungeni.
Suti za wabunge
Alipoulizwa jambo analojutia katika maisha ya siasa, Mchungaji Msigwa alisema kabla ya kuwa mbunge hakufahamu haiba ya wabunge waliopo, akivutiwa na suti zao, hadi alipopata fursa ya kuingia bungeni na kushuhudia udhaifu wa wabunge walio wengi.
“Nilipokuwa naona wabunge wanavaa suti kule ndani, nilikuwa navutiwa nao na kutamani niwe mbunge… baada ya kuwa mbunge na kuingia ndani kule, nimegundua wabunge wengi hawana sifa zinazofanana na suti wanazovaa. Hawapo makini na wanawadanganya Watanzania na suti zao, zile suti zao ni kuficha uhalisia wao, lakini hawana nia na dhamira ya dhati ya kuleta mabadiliko,” alisema.
Aliongeza: “Wengi wao hawajui wanachokitaka, ndiyo maana unaona mbunge anasema akitoka chama hiki, anakwenda kile, maana lengo lake ni kuendelea kuwa mbunge tu.”
Kuhusu jambo analojivunia alisema: “Nimefanya kazi kubwa ya ‘kuchange mind set’ (kubadilisha fikra za watu). Hiyo ndiyo ilikuwa hoja yangu jimboni, naamini hata bungeni nimelifanya hilo.”
Vigezo vya Chadema kushinda
Akizungumza kwa kujiamini, mchungaji huyo aliyeingia bungeni mwaka 2010 alisema katika Uchaguzi Mkuu ujao Chadema kina uhakika wa kushinda kutokana na vigezo walivyonavyo huku akiviainisha.
ADVERTISEMENT
“CCM imeendelea kushuka, kwa mfano, jimbo langu pale, CCM imekuwa ‘unpopular’ (siyo maarufu tena). Wanashindwa hata kufanya mikutano kwenye jimbo, lakini kibaya zaidi Serikali imeshindwa kabisa kutimiza malengo na matumaini ambayo wananchi walikuwa nayo.
“Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, chama chetu kimekua sana. Kwa muda mrefu chama chetu kilikuwa kinasubiri Zitto Kabwe, Dk Willibrod Slaa au Freeman Mbowe wafanye mikutano, lakini baada ya kuunda kanda 10, chama chetu kimepanuka sana.
“Kimepanuka kwa sehemu kwa sana kama vile matofali yakichomwa likianza moja mengine yanaanza kujiunguza yenyewe. Mikutano ya Chadema haimsubiri mtu. Hiyo siyo kwa Iringa pekee, ukienda Mufindi, Kilolo, Ludewa ndiyo hivyohivyo… ni kila mahala hata maeneo ambayo hatuna mbunge, moto umesambaa… wananchi wameendelea kuiamini Chadema.
“Jingine, katika uchaguzi wa mwisho wa mwaka 2010, Rais Jakaya Kikwete ameingia madarakani baada ya kupata asilimia 62 ya kura wakati alikuwa anatoka Ikulu. Alikuwa na ‘control’ (udhibiti) wa ‘machinery’ (mifumo) yote. Sasa anakuja mwingine kukutana na adui yuleyule ambaye ameimarika zaidi na pale Ikulu inakwenda kuwa Ikulu ambayo haina mwenyewe,” alisema. “Tunakwenda kwenye majimbo ambayo kila mtu anakwenda kufa peke yake. Hautakuwa kama uchaguzi wa Kalenga ambao walikuja wote kushambulia, sasa hivi kila mtu anakwenda kupambana mwenyewe. Ndiyo maana tunasema, tuna kila sababu ya kusema uchaguzi huu kama utakuwa wa huru na haki hawa jamaa hawachomoki.”
Akitaja kigezo kingine cha ushindi wa Chadema Mchungaji Msigwa alisema: “Kwa msuguano uliopo ndani ya CCM… haitatoka salama. Kama wakati ule makundi ya Kikwete yalidumu kwa miaka 10 hata sasa, makundi ndani ya chama hicho hayatakosekana. Kwa hiyo kugawanyika kwao ni faida kwetu.”
Ukomo wa ubunge
Akizungumzia majaliwa yake kisiasa, Mchungaji Msigwa aliyesema ana uhakika wa kushinda ubunge kwa kipindi cha pili, endapo chama hicho hakitashinda urais Oktoba mwaka huu, kitakuwa kipindi chake cha mwisho kwa ubunge.
“Labda tukishinda nchi (urais) nitagombea tena,” alisema Mchungaji Msigwa.
Alipoulizwa iwapo kauli yake kuwa ataendelea kuwania ubunge iwapo watatwaa urais inaonyesha wasiwasi wake wa kutoshinda nafasi hiyo, Msigwa alisema:
“Siwezi kusema nina wasiwasi, lakini katika chaguzi za kiafrika ‘anything can happen’ yaani unaweza ukashinda ukanyang’anywa, hata katika uchaguzi uliopita nilikuwa katika hatari ya kunyang’anywa.
“Nilishinda tangu saa mbili usiku, lakini matokeo yakatangazwa siku ya pili saa 10 jioni na hapo niliambiwa na vijana wa Usalama wa Taifa, unajua kuna Usalama wa Taifa ni wazuri. Waliniambia umeshinda lakini wanataka kukunyang’anya ushindi. Sikulala siku hiyo vijana waliniletea ‘Red Bull’ 10,” alisema Msigwa.
Manispaa ya Iringa
Alisema katika uchaguzi ujao, mbali na ilani ya chama, atafanya kampeni ya kuchukua Manispaa ya Iringa Mjini.
“Nataka tuongeze pato la Iringa Mjini. Wakati ninaingia, manispaa ilikuwa inaingiza Sh900 milioni na sasa tunaingiza Sh3.2 bilioni, tunataka mapato yaongezeke na kufikia Sh7 bilioni ili Iringa mjini tuweze kujijengea miundombinu. Tujue ‘pedestrian’ (waenda kwa miguu) wanatembeaje hata waendesha baiskeli, badala ya kutegemea Serikali Kuu,” alisema.
Alipoulizwa kuhusu hatima ya Ukawa katika uchaguzi na anavyompima mpinzani wake kisiasa kutoka CCM, David Mwakalebela, ambaye sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe kama ni tishio kwake, alisema:
“Nianze na jimbo. Kwa Mwakalebela siyo ‘threat’ (tishio) kwangu hata kidogo. Sasa hivi CCM wanagombana kuhusu ubunge. Wakati ule walisema nilishinda kwa sababu eti Mwakalebela hakugombea.
Sasa Kikwete (Rais) angefanya vizuri sana asingempeleka Wanging’ombe, angemleta Mwakalebela pale Iringa Mjini kuwa mkuu wa wilaya, tuwe wote pale yeye anakuwa na cheo cha DC, mimi mbunge. Angefanya vizuri sana kampeni zake za ubunge. Nasema hivi kwa sababu ‘he is not a threat at all’ (yeye siyo tishio kwangu kabisa).”
Aliongeza: “…Kinana alivyokuwa Iringa Mjini aliwaambia watu wa Iringa mjini huyu Msigwa alishindaje? Mmemchaguaje wakati ninyi ni watu wa CCM, mmefanya makosa… Walimdanganya, lakini majibu ya hoja aliyoijenga mwenyewe wameyapata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliopita. Mimi nilishinda ubunge nikiwa na mwenyekiti mmoja wa Serikali za Mtaa, sasa nina wenyeviti wa mitaa 67 kati ya 130.
“Hiyo ni ishara tosha kuwa wananiamini. Hiyo ni ishara tosha ya kwamba nakubalika. Hayo yametokea baada ya Kinana kusema mimi nina mwenyekiti mmoja. Nimewapa maneno ambayo hayatoki kichwani. Hata vijiweni wanani-quote (wananinukuu). Utawasikia, hata Mchungaji Msigwa alisema... niliwaambia mimi sitawapa samaki, nitawafundisha kuvua samaki na ndiyo maana niliwaambia mimi siyo ATM, miezi sita ya mwanzo nilikuwa ‘unpopular. Kiongozi ni yule anayefanya mambo sahihi, siyo mambo mazuri.”
Imeandikwa na Joyce Mmasi, Suzan Mwillo na Exuperius Kachenje
Powered by Blogger.