Bagonza: Maaskofu hatujagawanyika kuhusu Katiba

Dar es Salaam. Mjadala kuhusu tamko la Jukwaa la Wakristo Tanzania umezidi kupamba moto baada ya Askofu Benson Bagonza wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzani (KKKT) Dayosisi ya Karagwe, kupinga kuwapo kwa mgawanyiko miongoni mwao kama unavyosemwa na Serikali.
Kauli ya Askofu Bagonza imekuja siku moja baada ya Serikali kupitia Waziri wa Uchukuzi anayekaimu nafasi ya Kiongozi wa Serikali bungeni, Samuel Sitta kueleza kuwa maaskofu wamegawanyika na mgawanyiko huo hauwezi kubadili msimamo wa Serikali.
Sitta, ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa Bunge Maalumu, alisema maaskofu hao wawaache wananchi waamue wenyewe aina ya kura wanayotaka kuipigia Katiba Inayopendekezwa.
Akizungumza na gazeti hili jana, Askofu Bagonza alisema hakuna mgawanyiko na Serikali imeandaa maaskofu wake mfukoni ambao huwatumia kujibu hoja mbalimbali za maaskofu.
Alitoa mfano wa askofu mmoja ambaye alisema hafahamiki kwa Kanisa la Pentekoste, Walutheri wala Wakatoliki.
Kauli ya Pengo
Akizungumzia kauli aliyotoa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo inayopingana na maoni ya Jukwaa la Wakristo Tanzania, Askofu Bagonza alisema hayo ni maoni yake binafsi na haiwezi kuwa sauti ya Wakatoliki wa Tanzania.
Askofu Bagonza alisema sauti ya Wakatoliki hutolewa na Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) ambalo ndilo mwanachama wa Jukwaa la Wakristo Tanzania.
ADVERTISEMENT
“Mwadhama yeye ni mjumbe wa TEC, alitoa tu maoni yake na aliagiza tamko letu la jukwaa lisomwe kwenye makanisa ya jimbo lake la Dar es Salaam,” alisema Askofu Bagonza na kufafanua kuwa tamko lililotolewa na jukwaa ndiyo kauli rasmi ya Wakristo.
Askofu huyo alisema kabla ya msimamo wa jukwaa hilo kutolewa, siku tatu kabla TEC ambayo Kardinali Pengo ni mjumbe, lilitoa tamko lenye ujumbe unaofanana na wa jukwaa, ukiitaka Serikali kuahirisha kura ya maoni la sivyo waumini wahamasishwe kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa.
Msimamo wa makundi
Askofu Bagonza alisema suala la Katiba ni la Watanzania wote, hivyo makundi katika jamii yana haki ya kutoa maoni yake yanayoweza kutofautiana na ya wengine.
“Kama CCM na Serikali yake wanashawishi watu wapige kura ya Ndiyo, Ukawa wamewaeleza watu wao wasusie, iweje iwe tatizo kwa Jukwaa la Wakristo kuwaeleza wafuasi wao wapige kura ya Hapana?” alihoji.
Hata hivyo, Askofu Bagonza alisema jukwaa katika mjadala wake halikujikita katika mambo yaliyomo katika Katiba Inayopendekezwa, bali yale yaliyoachwa na jinsi mchakato ulivyokwenda.
Mahakama ya Kadhi
Kuhusu Mahakama ya Kadhi, Askofu huyo alisema jukwaa hilo halina tatizo na uzuri au ubaya wa mahakama hiyo, bali Serikali kujihusisha na suala hilo na kuifanya kama ahadi ya kuwavutia Waislamu kuipitisha Katiba Inayopendekezwa katika Bunge la Katiba.
Powered by Blogger.