Lowassa: Nimeshawishika kuwania urais

>Mbunge wa Monduli ,Edward Lowassa akiagana na Masheikh wa wailayani Bagamoyo mkoani Pwani baada ya kumkabidhi mchango wa kuchukua fomu ya kuwania urais nyumbani kwake,Dodoma jana.
ADVERTISEMENT
Hatimaye mbunge wa Monduli, Edward Lowassa amesema “ameshawishika” na kuweka bayana kuwa atachukua fomu ya kugombea urais kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Awamu ya Nne, amekuwa akitajwa kuwa ni mmoja wa makada wa CCM wanaowania urais, lakini hakuwahi kutangaza nia ya kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi nchini.
Lakini jana, alilazimika kufunguka kuhusu suala la urais ambalo lilimfanya yeye na wenzake watano wafungiwe kwa kipindi cha miezi 12 kujihusisha na harakati hizo baada ya Kamati Kuu ya CCM kuwatia hatiani kuwa walianza kampeni mapema kabla ya muda kufika.
“Nimepata barua za ushawishi kutoka kwa watu wengi, lakini nyinyi nimeshawishika,” alisema Lowassa nyumbani kwake mjini Dodoma wakati alipokuwa anazungumza na masheikh wa misikiti ya Wilaya ya Bagamoyo wanaokadiriwa kuwa kama 50 hivi ambao pia walikuja mjini hapa kwa ajili ya kumshawishi aingie kwenye kinyang’anyiro cha urais na kumkabidhi mchango wa Sh700,000 za kuchukulia fomu.
“Lakini bado kuna taratibu za chama za kuheshimu. Nangojea pale watakaposema sasa tuwe, basi itakuwa.”
Lowassa alifungiwa na CCM Februari 18, 2014 pamoja na Bernard Membe, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Steven Wasira (Kilimo, Chakula na Ushirika), na January Makamba (Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia).
Wengine waliofungiwa ni Frederick Sumaye, ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya Awamu ya Tatu na William Ngeleja (Mbunge wa Sengerema).
Pamoja na adhabu hiyo kumalizika Februari 18, CCM imesema Kamati ya Maadili inaendelea na uchunguzi kwa ajili ya kujiridhisha kama miongoni mwao kuna waliokiuka adhabu hiyo kabla ya kuwasilisha mapendekezo kwenye Kamati Kuu ambayo itafanya uamuzi.
Masheikh waliofika jana nyumbani kwake wanatoka maeneo ya Mlingotini, Kondo, Kaole, mjini Bagamoyo, Lugoba na Chalinze wilayani Bagamoyo.
Mbali na kumuomba atangaze nia, masheikh hao pia walimsomea dua ya kumtakia heri katika harakati hizo.
“Nyie ni special (maalum), mnatoka Bagamoyo na inajulikana kwa historia na ni nyumbani kwa Rais (Jakaya Kikwete). Namimi nimepata baraka zake na nyie mmemuwakilisha,” alisema Lowassa.
“Tumetoka naye mbali sana, lakini Mwenyezi Mungu akinijalia nitaanzia pale alikomalizia. Amefanya kazi kubwa na ya heshima kwa kweli. Kwa hiyo kitendo cha kutoka nyumbani kwenu kuja kuniona kwa kweli kimenipa nguvu kwamba wenzangu wa Bagamoyo wako pamoja na mimi.”
Alisema anaheshimu sana maneno waliyomwambia masheikh hao na anayakubali.
“Kwamba siku ikifika muda kwa mujibu wa taratibu za chama, nitachukua hiyo fomu. Lakini haitoshi tu kunishawishi, naomba mniombee dua… kuliko yote hili ni jambo la msingi sana. Kura zitapatikana kwa dua zenu,” alisema.
Lowassa pia alimsifia Rais Kikwete kwa kufanya mambo makubwa nchini na kwamba kati ya maeneo aliyoshughulika nayo sana ni elimu.
“Lakini elimu ni mtandao mkubwa, kuna matatizo mengi kunahitaji bado kushughulikiwa. Nikifanikiwa, inshallah nitaanza na suala la elimu kwa kufanya elimu iwe kipaumbele chetu katika Taifa letu,” alisema Lowassa ambaye alikuwa mstari wa mbele kuanzisha shule za kata na ndiye aliyeongoza ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma.
“Nikianza na elimu nitashughulikia mambo mengine mengi; kilimo kwanza, afya, ajira kwa vijana msingi wa hayo ukiwa ni elimu bora unaweza kuyashughulikia vizuri sana.”
Alisema pia akifanikiwa ataangalia jinsi ya kushirikisha dini katika muundo wa Serikali ili mambo ya Serikali na ya dini yaende vizuri bila mijadala nje ambayo inatishia amani na utulivu.
“Kuna nchi nyingine, mahali kama Pakistan mambo ya dini yana wizara yake ndani ya serikali. Kwa sababu mambo haya ni magumu sana, ukiyaendea vibaya yanaleta tabu katika nchi, yanaleta mauaji, vifo na vitu vingine,” alisema Lowasa.
Alisisitiza kuwa hata kama alikuwa na mawazo nusu nusu ujio wao umemuimarisha sana.
“Niseme kwamba ujumbe umefika, mkikutana naye msikitini pelekeni salamu kwa mheshimiwa Rais (Kikwete), mwambieni mlikuja Dodoma. Mie nimesema nitaendeleza pale alipomalizia kama Mwenyezi Mungu atanijalia,” alisema.
ADVERTISEMENT
Mmoja wa viongozi wa msafara huo, Sheikh, Hassan Kilemba alimsifu Lowassa kuwa alipokuwa Waziri Mkuu alilibeba tatizo la wanafunzi kukosa elimu ya sekondari kwa uchungu na kutekeleza kwa vitendo.
“Kama ungeendelea kubaki madarakani, shule zote za sekondari zingekuwa na mfano wa ajabu,” alisema.
Alisema pia matatizo ya maji katika Kanda ya Magharibi yaliweza kupungua na kuisha kwa jitihada zake na wananchi.
“Mheshimiwa Lowasa ulikubali kuachia ngazi lakini bado ukawa mtiifu kwa chama chako na bado ukawa mwadilifu kwa kuwapenda wananchi,” alisema.
Alisema mkoani Mwanza, Waislamu walitaka kuanzisha redio yao lakini bila kujali tofauti ya dini alikwenda kwenye harambee ya kuchangia redio hiyo.
Pia alisema msikiti wa Mtambani walipopata tatizo la moto, alikwenda kuwafariji, jambo ambalo ni kubwa sana kwa waumini wa dini ya Kiislamu.
“Sisi pasipo kushawishiwa na mtu yeyote tumeamua kuja kukushawishi uwanie urais. Tafadhali tafadhali wala usipate kigugumizi chukua fomu. Bagamoyo hauko pekee yao. Sisi masheikh wa Bagamoyo tumeamua kujichangisha ili fedha zikusaidie katika harakati zako,“ alisema.
Naye Sheikh Yusuph Suruhu alisema Lowasa alikuwa kiongozi wa vitendo na hakuwa mtu wa kulalamika.
Lowassa alijiuzulu wadhifa wa Waziri Mkuu mwaka 2008 baada ya kutajwa kwenye kashfa ya mkataba wa kampuni ya uzalishaji umeme ya Richmond Development Company ya Houston Marekani, ambayo ilionekana haikuwa na uwezo wa kutekeleza utashi wa mkataba wa kuzalisha umeme wa dharura wakati nchi ikiwa kwenye tatizo kubwa la nishati hiyo. Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza kashfa hiyo ilimtaka Lowassa apime ushiriki wake katika kuingia mkataba huo na afanye uamuzi.
Katika hotuba yake ya kutangaza kuachia ngazi, Lowassa alisema ameamua kujiuzulu ili kulinda heshima ya Serikali katika kashfa hiyo kubwa iliyotikisa nchi na kusababisha mawaziri wengine wawili kuwajibika pia.
Kikundi hicho cha masheikh wa wilayani Bagamoyo ni hitimisho la mlolongo wa vikundi ambavyo vimekuwa vikipishana mjini Dodoma na jimboni kwake Monduli mkoani Arusha kumshawishi achukue fomu ya kuwania urais, lakini amekuwa akieleza kuwa muda ukifika atafanya uamuzi huo.
Waziri huyo wa zamani wa Maji na Maendeleo ya Mifugo alipata shahada yake ya sanaa kwenye Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na shahada ya umahiri wa masomo ya maendeleo kwenye Chuo Kikuu cha Bath nchini Uingereza.
Lowassa alikuwa waziri wa Nchi, Ofisi ya waziri Mkuu wakati wa kipindi cha pili cha Serikali ya Awamu ya Pili. Wakati Rais Ali Hassan Mwinyi alipomaliza muda wake, Lowassa alijitokeza kuwania urais kwa tiketi ya CCM mwaka 1995, lakini alishindwa katika hatua za mwanzo na Benjamin Mkapa alishinda na kuongoza kwa vipindi viwili.
Alirejea bungeni na hakuteuliwa kuwa waziri hadi mwaka 1997 alipoteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Kupambana na Umaskini).
Baada ya uchaguzi wa mwaka 2000, aliteuliwa kuwa Waziri wa Maji na Maendeleo ya Mifugo, wizara ambayo alijitengenezea jina kama mchapakazi.
Uchaguzi uliofuata, Lowassa hakujitosa kwenye mbio za urais, na badala yake akawa kitovu cha kampeni cha mgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete ambaye alikuwa rafiki yake wa muda mrefu na haikuwa ajabu kwa Kikwete kumteua kuwa waziri wake mkuu wa kwanza baada ya kushinda uchaguzi.
Lowassa ameingia kwenye historia kama Waziri Mkuu wa kwanza kujiuzulu wadhifa wake kutokana na kashfa dhidi ya Serikali iliyosababisha rais avunje Baraza la Mawaziri.
Lowassa ni nani?
Jina lake kamili ni Edward Ngoyai Lowassa. Alizaliwa Agosti 26 mwaka 1953 na kusoma katika Shule ya Msingi Monduli kati ya mwaka 1961 na 1967. Mwaka 1968 hadi mwaka 1971, alisoma katika Shule ya Sekondari Arusha, kabla ya kujiunga na Elimu ya Juu ya Sekondari katika Shule ya Milambo Tabora kati ya mwaka 1972 na 1973.
Baada ya kuhitimu, Milambo, alijiunga na Masomo ya Shahada ya Ualimu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya mwaka 1974 na 1977, kabla hajaingia katika Chuo kikuu cha Bath kilichoko nchini Uingereza kwa ajili ya Masomo ya Shahada ya Pili ya Sayansi mwaka 1983 hadi 1984, na baadaye kuendelea chuoni hapo kwa Shahada nyingine ya Pili ya Elimu ya Maendeleo.
Baada ya kuhitimu kozi hiyo, Lowassa alirudi nchini na kuanza ajira yake ya kwanza katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha jijini Arusha (AICC) akiwa Mkurugenzi Mtendaji na baadaye kuwa Waziri wa Katiba na Mambo ya Bunge kati ya mwaka 1990 na 1993. Mwaka 1993 hadi 1995 Lowassa alikuwa Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi na kati ya mwaka 1997 na 2000, alikuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mazingira na Umaskini) kabla hajateuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa Waziri Mkuu mwaka 2005 hadi 2008. Amekuwa Mbunge wa Monduli kwa kipindi cha miaka 20 sasa.
Powered by Blogger.