Marsh aagwa Dar kuzikwa Mwanza


 Dar es Salaam. Aliyekuwa kocha msaidizi wa Taifa Stars, Silvester Marsh ameelezwa kujitabiria kifo chake saa chache kabla ya kutokea juzi asubuhi kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Akizungumza katika ibada ya mazishi iliyofanyika jana, Katekista wa Kanisa Katoliki Muhimbili, Rogatus Fussi alisema Ijumaa asubuhi alipokea barua ya Marsh akiomba kufanyiwa sala ya toba.
“Barua hiyo ilikuwa na majina matatu likiwamo la Marsh ambaye aliomba padri akamuombee sala ya toba, kwa kuwa Padri hakuwepo, saa tisa alasiri nilikwenda mimi.
“Nilimkuta Marsh akiwa katika hali mbaya, nilifanya nae sala hadi saa 11 jioni na kupitia yeye pia kuna baadhi ya watu kwenye wodi aliyolazwa walipata huduma hiyo.
“Asubuhi jana (juzi Jumamosi) nilikwenda kumtembelea kama nilivyoahidi na nesi kuniambia tayari Marsh amefariki, hii ni ishara tosha kuwa mpendwa wetu alijiandaa kabla ya kifo chake hivyo na sisi tuliobaki tunatakiwa kujiandaa,” alisema katekista huyo.
Mwili wa Marsh uliwasili kanisani majira ya saa 5:30 asubuhi tayari kwa ibada ya mazishi ambayo ilianza saa 6:30 kanisani hapo na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa soka akiwamo Kocha wa Yanga, Charles Mkwassa, Kocha wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage, mwakilishi kutoka Idara ya Maendeleo ya Michezo, Juliana Yasoda, wanafamilia na wadau wengine.
Katika hali ya kushangaza, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lilikosa mwakilishi wa kutoa salamu za rambirambi katika ibaada hiyo baada ya katekista kumtaka mwakilishi wa familia na yule wa TFF kutoa salamu hizo na kwa upande wa familia, kaka wa Marehemu, Zablon Marsh alisema taratibu za mazishi zitajulikana baada ya mwili wa marehemu kuwasili jijini Mwanza huku upande wa TFF wakikosa mtu na katekista kuamua kuendelea na taratibu za kuuga.
Hata hivyo, gari la TFF (Hiace) ambalo lilitarajiwa kuusafirisha mwili wa Marsh halikuwepo eneo la Hospitali, hivyo kulazimika mwili wa Marsh kusubiri kwa saa kadhaa baada ya kuagwa kwa kile ambacho kilielezwa dereva alikuwa njia kutoka Morogoro.

Powered by Blogger.