Zitto ahusisha hukumu yake na escrow


 
 Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe 
Dar es Salaam. Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe amewaaga wapigakura wake kuwa hatakuwa tena mbunge wao, akisema kuwa kesi ya dhidi ya Chadema ilitupwa na Mahakama Kuu kutokana na baadhi ya majaji kutajwa kwenye kashfa ya escrow.
Chadema ilimvua Zitto uanachama saa chache baada ya Mahakama Kuu kutupa shauri lake alilofungua akitaka chombo hicho cha sheria kimlazimishe katibu mkuu wa chama hicho kumpa nyaraka za mwenendo wa vikao vya Kamati Kuu vilivyomvua nyadhifa zote, huku akifanikiwa kupata amri ya muda ya kuizuia Chadema kumjadili.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Mwandiga mkoani Kigoma jana, Zitto alisema hatakuwa mbunge wa jimbo hilo baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, na akatumia fursa hiyo kueleza safari yake ya kisiasa ndani ya Chadema na mtazamo wake baada ya kufukuzwa uanachama.
“Nimejifunza mengi nikiwa mbunge. Katika utumishi wangu kwenu, bungeni nimejifunza namna nchi yetu inavyoendeshwa. Katika kujifunza huko kuna mambo kadhaa nimefanya ya kujivunia na mengine ni makosa,” alisema Zitto ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chadema.
 “Nimejifunza kuwa mzalendo zaidi kwa nchi yangu na kuwatumikia watu wa nchi hii. Ndiyo maana hamkunisikia tu nikitetea watu wa Kigoma pekee, bali watu maeneo mengine ya nchi yetu na makundi mbalimbali ya kijamii.”
Alisema safari yake ya ubunge ilikuwa ngumu yenye mafunzo makubwa na imemfanya apevuke kifikra na kupata mafunzo.
Awali, akizungumza na waandishi wa habari, Zitto alisema: “Bado nina nia ya dhati ya kuendelea kuwatumika Watanzania kama mwakilishi wao kupitia jimbo lolote nchini.
Nitaendelea kuwapo kwa uwezo wa Mungu katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba. Itakuwa kwa tiketi gani na jukwaa gani watu watayajua hayo wiki hii.”
 Akizungumzia sakata la escrow lililowahusisha watendaji mbalimbali wa Serikali, wakiwamo majaji na hukumu ya kesi yake, Zitto alirudia tena kauli yake kuwa hukumu hiyo imetolewa bila yeye kujua. “Kwa kazi ninazozifanya kuna miguu ya watu wengi ninayoikanyaga.
Moja ya ninaowakanyaga ni mahakama. Kuna majaji ambao taarifa ya kamati ya PAC imewataja kuhusika na escrow na wanatakiwa kuchunguzwa,” alisema.
Alisema inawezekana ndani ya mahakama wameona hukumu ya kesi hiyo ndiyo eneo zuri la kumkomoa.
“Inawezekana pia watu ambao kupitia kazi za PAC, nimesababisha wachukuliwe hatua nao pia wanaweza kuwa wameshiriki kwa njia moja au nyingine. Lakini pia inawezekana ni taratibu za kawaida za mahakama. Mpaka hukumu inatolewa kuna maswali mengi hayana majibu,” alisema.
Alisema wanatilia shaka hukumu hiyo kutokana na mahusiano ya karibu yaliyokuwapo kati ya mahakama na mawakili wa Chadema kwa maelezo kuwa yeye na wakili wake hawakuwa nayo na kwamba hawakupata taarifa za kuitwa mahakamani.
“Kwetu sisi hukumu hii ni mshangao. Tulivyoenda kutaka hukumu ya kesi siku mbili mfululizo tulinyimwa, siku ya tatu tulivyoitaka tulielezwa kuwa faili limechukuliwa na jaji kiongozi kwa ajili ya mapitio,” alisema.
Alisema kilichotokea kimempa funzo na kwamba iwapo atapata fursa ya kufanya mabadiliko nchini, idara ya mahakama ni sehemu ambayo ataifanyia mabadiliko makubwa kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa wananchi.
Kuhusu uhuasiano wake na Freeman Mbowe ambaye ni mwenyekiti wa Chadema, Zitto alimponda kiongozi huyo kuwa ana tabia za ‘undumilakuwili’, na kusisitiza mara kadhaa amekuwa akimtumia (mbunge wa Moshi Mjini, Philemon) Ndesamburo kuwasuluhisha, lakini akiwa pembeni amekuwa akitoa kauli za kumponda yeye (Zitto) kuwa amemsadia mambo mengi. “Nikikaa peke yangu huwa najiuliza ni nini ambacho kimetokea, sipati jibu. Ninachokiona ni ugomvi wa madaraka na juhudi za watu kutaka kuwaondoa wengine katika ulingo. Katika mazingira kama hayo watu wanaweza kutafsiri nina ugomvi naye,” alisema. Zitto pia aliponda kanuni za Chadema zinazoeleza kuwa mwanachama akifungua kesi mahakamani kupinga uamuzi wa chama anafukuzwa uanachama na kuwataka wana-Chadema kuipinga kanuni hiyo.
Akizungumzia madai ya kutumiwa na CCM na usalama wa Taifa, Zitto alianza kwa kueleza jinsi alivyoibua hoja nzito bungeni na kuongoza kamati yake ya PAC kuibua mambo yaliyowang’oa mawaziri mara tatu kwa nyakati tofauti, na kuhoji kuwa kama angekuwa anatumiwa na CCM asingeweza kuibua hoja za kuiangusha Serikali ya chama hicho tawala ndani ya miaka mitano bungeni.
Powered by Blogger.