Nyalandu: Urais CCM, Ukawa ni kivumbi

Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu (kushoto) akizungumza na wahariri wa magazeti ya Mwananchi Communicatons Limited (MCL), alipoitembelea kampuni hiyo iliyopo Tabata, Dar es Salaam jana, kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa MCL, Francis Nanai.
ADVERTISEMENT
Dar es Salaam. Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu amesema uchaguzi wa Rais ajaye utakuwa na ushindani mkubwa ndani na nje ya CCM, huku akibainisha kuwa haogopi mtu kati ya wote wanaotajwa kwenye kinyang’anyiro hicho, bali anawaheshimu.
Lakini mbunge huyo wa Singida Kaskazini amesema mgombea pekee atakayemwogopa ni yule atakayekuwa anataka kulipiza kisasi dhidi ya wagombea wengine.
Waziri huyo alitoa kauli hiyo jana wakati alipofanya ziara kwenye makao makuu ya Ofisi za Mwananchi Communications inayozalisha magazeti ya The Citizen, Mwananchi na Mwanaspoti zilizoko Tabata Relini kando ya Barabara ya Mandela.
“Sipendi kulizungumzia sana jambo hilo,” alisema Waziri Nyalandu ambaye huzungumza kwa sauti ya chini na taratibu... “Kwenye chama chetu (CCM) muda wake bado. Lakini naweza kusema kuwa mwaka huu ni wa ushindani mkubwa ndani ya CCM na ‘opposition’,” aliwaambia wahariri wa Mwananchi Communications.
“Mwisho tutakuwa na kambi ya CCM. Kwaya ya CCM itapambana na kwaya nyingine ambayo ina sauti zote nne kama CCM,” alisema akimaanisha kuwa upinzani nao utakuwa umekamilika na kusisitiza muda ukifika atachukua fomu.
Kauli ya Nyalandu imekuja wakati nchi ikijiandaa kuingia kwenye Uchaguzi Mkuu utakaoiweka madarakani Serikali ya Awamu ya Tano, hali ambayo inaipa shida CCM kumpata mrithi wa Rais Jakaya Kikwete ambaye pia atalazimika kuachia uenyekiti wa chama hicho.
Tayari wanachama wanne wa CCM wameshatangaza nia, akiwamo Nyalandu. Wengine ni Hamisi Kigwangala, ambaye ni Mbunge wa Nzega, January Makamba (Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia) na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Hata hivyo, kinyang’anyiro kikubwa kinatarajiwa kuwa miongoni mwa makada wa muda mrefu wakiongozwa na Edward Lowassa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu na Bernard Membe (Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), ambao hawajatangaza nia, lakini wanatumikia adhabu ya kufungiwa kwa zaidi ya miezi 12 kwa makosa ya kukiuka taratibu za chama hicho kwa kuanza kampeni mapema.
Wengine wanaotajwa kwenye mbio hizo ni Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Waziri wa Fedha (Sera), Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira, Mbunge wa Songea Mjini, Emmanuel Nchimbi, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Wakati CCM ikiwa na kazi ya kumpata mgombea wake wa urais, hali ni ngumu zaidi safari hii nje ya chama hicho kutokana na vyama vinne vya upinzani kukubaliana kusimamisha mgombea mmoja kwenye kila nafasi.
Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD vimeunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na vimesaini makubaliano ya kusimamisha mgombea mmoja.
Nyalandu, ambaye alitangaza nia yake wakati akiwa jimboni kwake, alisema mjadala wa kuelekea Uchaguzi Mkuu unatakiwa ujikite kwenye masuala ya kuiondoa nchi kutoka hapa ilipo na kwenda juu zaidi.
“Baada ya miaka 50, ungetegemea mjadala uwe katika kufufua uchumi, kuongeza ajira, usalama wa wananchi, enlightment ya watu au elimu, afya na rasilimali. Huo ndiyo uwe mjadala kwa watakaowania nafasi ya urais,” alisema.
“Wagombea wote wa CCM na Ukawa tujadili namna gani tutaifanya Tanzania kuwa bora. Ni namna gani tutajibu maswali ya Watanzania kwa wakati uliopo.”
Akijibu swali kuwa kati ya wanaotajwa kuwania urais, ni yupi tishio kwake na anayemwogopa, Nyalandu alisema: “Hakuna cha kuogopa, wote nawaheshimu.
“Kwa sisi Walutheri, tunaambiwa ‘kisasi ni juu yangu, asema Bwana,” alisema akinukuu maandiko ya kitabu kitakatifu cha Kikristo cha Biblia.
“Ninayemwogopa zaidi ni atakayekuwa na revenge (kisasi). Ukiwa mtu wa kisasi ni hatari, lakini ‘daima mwombee adui yako uzima’ ili aone utakapofanikiwa na ajifunze.”
Hata hivyo, alisema ni vigumu kwa anayeshinda uchaguzi kutekeleza nia yake ya kulipa kisasi.
“Naamini yeyote atakayeongoza ataongoza kwa Katiba ya Tanzania. Uongozi (rais) ujao uwe wa maono juu ya nchi yetu, uzingatie uzalendo na heshima kwa wote.”
Kuhusu mjadala wa umri kwa nafasi ya urais, Nyalandu alisema hakuna mtu mwenye wakati wake.
“Nasikia maneno kuhusu ujana na uzee. Huu ni wakati wa wote. Uongozi wa nchi unategemea busara siyo umri, mdogo au mkubwa,” alisema Nyalandu, ambaye ana umri wa miaka 45.
Akizungumzia kauli ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana aliyempamba Lowassa na kumwita yeye kuwa mzururaji, Nyalandu alisema hawezi kuzungumzia hilo kwa kuwa hajamsikia akisema hayo, lakini akasema wanafanya kazi vizuri na alishawahi kumwagia sifa wakati alipotembelea jimboni kwake... “Kinana alikuja na Singida Kaskazini na kati ya watu aliowasifia sana alikuwa huyu Lazaro Nyalandu,” alisema waziri huyo na kuongeza: “Kinana alikuta kila kijiji kina maji kwa nguvu za wananchi, wafadhili au Serikali ilichangia. Nilipoanza ubunge miaka 15 iliyopita mtu akijenga kwa bati alikuwa anarogwa au anapata hofu ya kurogwa, lakini sasa nyumba za nyasi ni za kuhesabu. Mwandishi ambaye angechukua stori ya Singida Kaskazini, kwa kauli ya Kinana, angeandika: ‘Nyalandu mfanyakazi wa kutisha’.”
Utendaji wizarani
ADVERTISEMENT
Waziri Nyalandu alitumia muda mwingi kuelezea utendaji wa wizara yake, akisema ni ngumu kwa kuwa inagusa kila nyanja ya maisha ya Watanzania na inayomfanya awaonee huruma watoto wake kutokana na kutopata muda mwingi wa kuwa nao.
Alisema ni muhimu uhifadhi wa maliasili usaidie maisha ya kawaida ya kila siku kwa wananchi, lakini pia rafiki wa uhifadhi huo awe mwananchi mwenyewe.
Kuhusu mapambano dhidi ya ujangili alisema Serikali kupitia wizara yake inapambana na tatizo hilo ndani na nje ya nchi kwani lengo la dunia ni kukomesha mtandao wa ujangili.
“Hatua kubwa nilichukua kuagiza sensa ya tembo ili tuwe na uwazi. Sensa zilizofanyika Serengeti, Mara na Kenya zinaonyesha ongezeko kubwa la tembo. Kuna mahali tumefanikiwa, lakini kuna mahali wamepungua. Niliamua tupate ukweli kwanza. Mwezi ujao tutatangaza matokeo ya sensa hiyo,” alisema Nyalandu.
Akizungumzia hatua ya Kenya kuteketeza akiba ya meno yake ya tembo na Tanzania kutofanya hivyo, alisema Serikali iliamua meno hayo kutofanyiwa biashara, lakini akasema suala la historia pia ni muhimu kwa kuwa kuna meno ambayo ni ya tembo wa zamani na ni makubwa hayawezi kupatikana dunia ya sasa.
Alisema pia kuna meno ambayo hupatikana baada ya tembo wazee kufa na kwamba meno hayo zaidi 100,000, yote huwekewa alama ya utambuzi na kupimwa vinasaba (DNA) ili unapotokea uhalifu yaweze kutambulika kwa urahisi.
“Sisi hatutachoma moto meno yetu ya tembo, bali tutakuwa wawazi kitaifa na kimataifa,” alisema.
Alisema kuwa katika vita dhidi ya ujangili duniani ni habari njema kusikia kwamba China imeacha kuingiza meno ya tembo kwa mwaka mmoja na kuongeza kuwa ombi la Tanzania ni kuitaka nchi hiyo iache kabisa.
Pia alielezea jitihada mbalimbali zinazoendelea kufanyika kukabiliana na ujangili, ikiwa ni pamoja na ununuzi wa vifaa kama ndege pamoja na makubaliano na nchi jirani za Kenya, Zambia na Msumbiji ili kuwa na harakati za pamoja katika kuwanasa majangili na kukomesha usafirishaji kwa njia ya reli, bahari na ndege.
Alisema ulinzi wa asili pia ni muhimu katika hifadhi na mbuga za wanyama na kwamba ili kuimarisha ulinzi, mwaka uliopita wizara yake iliajiri askari wa wanyamapori 500 na wengine idadi kama hiyo walikuwa wa muda.
“Tatizo la ujangili ni kubwa, askari wanapoteza maisha kwa kushambuliwa na majangili. Lakini sasa tumeleta askari wa Marekani wanatoa mafunzo kwa askari wetu ili nao waweze kuwa walimu wa wenzao. Hayo ni mafunzo endelevu, majeshi yetu yanashirikiana na Marekani katika mafunzo ya kupambana na ujangili,” alisema.
Kukaa ofisini
Akizungumzia tuhuma kwamba hakai ofisini na kazi zake za uwaziri anazifanyia hotelini, Nyalandu alisema anatumia muda wake ofisini kama mawaziri wengine na kwamba hata angekaa ofisini, watu wangesema anashinda ofisini bila ya kuhudumia wananchi.
“Jambo hilo siyo kweli. Hizo ni siasa chafu. Hii inalenga kumchafua mtu na kuharibu sifa yake.”
Alibainisha kuwa kutokana na utendaji wake na walio chini yake, kwa mara ya kwanza wizara hiyo mwaka huu imeongoza kwa kuliingizia taifa fedha za kigeni.
“Pia inaongoza kwa kutoa ajira 500,000 za moja kwa moja na nyingine milioni mbili kupitia sekta zake. Dola 1.7 bilioni ziliingia katika uchumi. Unaweza usimpende mtu, lakini kwa anayofanya mafanikio yapo wazi,” alisema Nyalandu.
Alipoulizwa kuhusu kutowekwa hadharani kwa taarifa ya tume ya kimahakama iliyochunguza Operesheni Tokomeza, licha ya kukiri Nyalandu alisema kuwa wakati ukifika itawekwa hadharani.
“Hata mimi ilinihoji kwa saa tatu. Bado tunasubiri itolewe rasmi. Ni tume ya kimahakama, wote waliohusika walihojiwa,” alisema.
Kuhusu utalii waziri huyo alisema ni jukumu la kila Mtanzania kuutangaza. Alisema katika kuhakikisha Tanzania inajulikana zaidi kimataifa katika utalii, tangazo la viwango vya kimataifa lililotengenezwa Hollywood linakaribia kukamilika.
“Tangazo hilo limetengenezwa kwa gharama za wafadhili wenyewe na hakuna hata fedha ya Tanzania iliyotumika. Hivi sasa linafanyiwa editing (linahaririwa). Litakuwa la aina yake,” alisema.
Akizungumzia tozo la kodi kwa hoteli za kitalii jambo ambalo lilizua mjadala katika kikao cha Bunge Desemba mwaka uliopita, Nyalandu alikanusha tuhuma kwamba Februari mwaka huu alikutana na wamiliki wa hoteli hizo na kueleza kuwa alimwagiza Katibu Mkuu wa wizara yake kufanya hivyo.
Alisema awali, hoteli zilikuwa zikikatwa asilimia 10 kwa kila kitanda, lakini baadaye ikaondolewa na badala yake tozo ikawa ya makisio ambayo ilisababisha baadhi ya wamiliki wa hoteli kulalamika hivyo kumuagiza katibu wake kwenda kujadiliana nao ili kufikia muafaka.
“Ilikuwa lazima wakubaliane kuhusu njia ya ukokotoaji kodi husika na siyo makisio bila ya kuwa na msingi wa makisio. Tangazo la Serikali la mwaka 2009 lilihusu hoteli 27 tu, lakini tangu wakati huo kuna hoteli 30 zimejengwa na nyingine 15 zinaendelea kujengwa,” alisema.
Powered by Blogger.