Mvua yazua balaa Buguruni, watu 1,163 hawana mahali pa kuishi

> Mkazi wa eneo la Buguruni kwa Mnyamani akihamisha vitu vyake jana baada ya makazi yao kukumbwa na mafurika kutokana na mvua inayoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam. Picha na Said Khamis
ADVERTISEMENT
Zaidi ya wakazi 1,163 wa eneo la Buguruni kwa Mnyamani hawana mahali pa kuishi baada ya nyumba zao 517 kukumbwa na mafuriko.
Akizungumza jana na gazeti hili, Mwenyekiti wa Mtaa wa Buguruni kwa Mnyamani, Abdallah Mng’ae alisema maji hayo yanaendelea kuongezeka na madhara zaidi yanaweza kutokea kutokana na mvua kuendelea kunyesha.
Alisema siku ya kwanza, nyumba 30 zilikumbwa na mafuriko, lakini kadri mvua inavyozidi kuendelea ndivyo maafa nayo yanaongezeka.
“Wengi wao waliokumbwa na mafuriko hayo kwa sasa wanalala katika vibaraza vya watu wakiwa na watoto wadogo, wanapigwa na baridi usiku kucha,” alisema Mng’ae na kuongeza:
“Hadi sasa hawajapata msaada wowote kutoka serikalini, tunaomba msaada hasa chakula, mavazi na dawa.”
Alisema watu waliojitokeza kutoa msaada ni Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba aliyetoa Sh500,000.
ADVERTISEMENT
Eneo la Vingunguti, mwandishi alishuhudia nyumba nyingi zikiwa zimejaa maji, huku wamiliki wakilalamika kuwa vitu vingi vimeharibika.
Mkazi wa eneo hilo, Amina Salehe alisema tangu juzi hadi jana maji ya mvua yameendelea kuingia ndani ya nyumba yake na kumsababishia kukosa sehemu ya kulala.
Wakati huohuo, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imesema mvua itaendelea kunyesha kwa siku tatu mfululizo katika mikoa ya Pwani, Mtwara, Lindi, Dar es Salaam na Tanga.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Hali Hewa jana, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agness Kijazi aliwataka wananchi wanaoishi mabondeni kuhama ili kuepuka madhara yanayoweza kuwakumba.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Samwel Mwampashe alisema polisi wanaendelea kufanya doria ili kubaini madhara zaidi.
Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema hawajapata taarifa ya kutokea kwa vifo mkoani humo zaidi ya zile za baadhi ya watu kukosa makazi baada ya nyumba zao kujaa maji.
Powered by Blogger.