Mbaroni kwa kukutwa na mifupa ya albino

Polisi mkoani Kagera wamedai kuwakamata watuhumiwa wawili wakiwa na mifupa inayodhamiwa kuwa ya binadamu mwenye ulemavu wa ngozi (albino), aliyefariki mwaka 2006 wa Kijiji cha Rushwa wilayani Muleba.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Henry Mwaibambe, alisema watuhumiwa wote ni wakazi wa Kijiji cha Kyota wilayani Muleba na kwamba walipata mifupa hiyo kwa msaada wa mganga wa jadi.
Alisema watuhumiwa walikamatwa na mfupa mmoja na baada ya kupekuliwa zaidi katika nyumba yao walikutwa na mifupa mingine miwili na walipohojiwa wanadaiwa kukiri kuwa ilikuwa ya albino.
“Walifukua kaburi mwaka 2008 kwa maelekezo ya mganga wa jadi,” alisema Mwaibambe.
Alieleza kuwa watuhumiwa walifukua kaburi la Zeuria Justus aliyefariki mwaka huo katika Kijiji cha Rushwa, Kata ya Mushabago, kazi iliyofanyika 2008 kwa maelekezo ya mganga wa jadi.
Kwa mujibu wa Mwaibambe, Zeuria alikufa muda mfupi baada ya kujifungua na polisi walilazimika kufukua kaburi hilo baada ya kupata kibali cha mahakama na kukuta baadhi ya viungo vimeondolewa.
Hata hivyo, Mwaibambe alisema mganga wa jadi ametoroka na anasakwa na polisi, huku watuhumiwa wakitarajiwa kufikishwa mahakamani. Majibu zaidi ya uchunguzi wa viungo hivyo yanasubiriwa kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.
Sangoma walaani wenzao
Waganga wa jadi mkoani Tabora, wamelaani wenzao wanaojishughulisha na kupiga ramli chonganishi kuwadanganya wateja wao kuwa viungo vya binadamu vinaleta utajiri.
Mwenyekiti wa Chama cha Waganga wa Jadi (Chawatiata) Mkoa wa Tabora, Yasin Mwarabu akitoa tamko la waganga hao alilaani baadhi ya wenzao wanaojihusisha na imani potofu kuwa, viungo vya binadamu vinaleta utajiri na kushiriki kupiga ramli chonganishi zinazosababisha mauaji.
Mwarabu alisema kama chama wanaungana na Serikali kwa jitihada zake za kuwabaini waganga matapeli na watashirikiana kukemea kwa nguvu zote.
“Kazi ya uganga ni kutibu siyo kuua, hivyo kama wapo wanaoua hao siyo wenzetu na kamwe hatuwahitaji kwa vile wanatuharibia,” alisema.
Hivi karibuni, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Suzan Kaganda alikutana na waganga wa jadi na kuwataka kufanya kazi zao kwa kuzingatia maadili na sheria za nchi.
Watoa onyo
Msako wa kukamata wapiga ramli chonganishi ukiwa unaendelea nchini, waganga wa jadi wametoa onyo kwa polisi kuhusu vifaa vinavyokamatwa wakati wa msako huo. Askari walipewa tahadhari ya kukumbana na hatari yoyote baadaye iwapo wataendelea kukamata vifaa hivyo vikiwamo vibuyu, vitambaa vyeupe na vyeusi, ngawo, mikuki na shanga huku wakitakiwa kuvirejesha mara moja.
Akizungumza na waganga wa jadi wa Wilaya ya Bariadi, Mkoa wa Simiyu juzi, Katibu Mwenezi wa Chawatiata Mkoa wa Mwanza, Stephen Sebastian alisema kukamata vifaa hivyo ni kitendo cha hatari.
Sebastian alikuwa akizungumza mbele ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, Charles Mkumbo na kusema kitendo kinachofanywa na polisi kukamata vifaa hivyo kinaweza kusababisha hali ya migogoro mikubwa kati ya polisi na jamii.
“Nitoe tahadhari mbele yako mkuu wa polisi, msako huu unaoendelea umelenga kusambaratisha jadi wakati ndizo zilizotumika kuleta uhuru, vifaa hivi vinavyokamatwa virejeshwe mara moja, wazee hawa wakikasirika hakuna atakayebaki ndani ya polisi, msitake kugombana na mila gombana na wanaopiga ramli chonganishi, lakini chondechonde rejesheni vibuyu vyetu haraka,” alisema.
Sebastian alidai wazee hao wanaweza kukasirika wakati wowote kuanzia sasa iwapo vibuyu vyao vitaendelea kukamatwa, huku vingine vikiwa havirejeshwi kwa wamiliki walioachiwa.
Naye Mkumbo alikanusha kwamba waganga wa jadi wanaonewa au kusingiziwa kuwa wanapiga ramli chonganishi, kwani kwa uchunguzi wao wamebainika ndiyo chanzo kikuu cha mauaji ya albino na vikongwe.
Mkumbo aliwataka waganga hao kuacha vitendo hivyo, huku akiwaelekeza ndani ya mwezi mmoja kila mganga awe amepata leseni au kujiandikisha kwa viongozi wake wa kijiji au mtaa ili kuweza kukwepa msako mkali utakaoanza.
Katika hatua nyingine, waganga hao walifanya uchaguzi katika mkutano huo na kumchagua Mayunga Kidoyai kuwa Mwenyekiti wao, Shinyanga Isamila (Makamu Mwenyekiti), Njile Kasula (Katibu) na John Kunini (Katibu Msaidizi).
Imeandikwa na Phinias Bashaya (Bukoba), Robert Kakwesi (Tabora) na Faustine Fabian (Bariadi)
Powered by Blogger.