Dk Kahangwa: Nitawania urais NCCR- Mageuzi


Dk.Kahangwa
Majuma mawili tangu Umoja wa Vijana wa Chama cha NCCR-Mageuzi umtake, Dk George Kahangwa (46) kugombea urais, mhadhiri huyo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema ameridhia wito huo.
Machi 8, mwaka huu Kitengo cha Vijana cha NCCR - Mageuzi kilimpendekeza Dk Kahangwa kugombea nafasi hiyo kwa kuwa kimeridhishwa na utendaji wake wa kazi, ujana na ucha Mungu wake.
Akizungumzia mapendekezo hayo mwishoni mwa wiki, Dk Kahangwa alisema: “Mwanzoni yalikuwa mapendekezo tu ya vijana na mpaka sasa nilikuwa sijatoa kauli rasmi, lakini baada ya kupata ushauri na kutafakari, nimeona sina kikwazo katika jambo hilo.”
Msomi huyo wa masuala ya elimu, alisema inawezekana akasita kwa kuwa jukumu hilo ni kubwa lakini uungwaji mkono na hamasa anayopata na kauli wanazomwambia zinaonyesha inawezekana na wanamwamini.
Vipaumbele vyake
Alitaja vipaumbele vyake kuwa ni kuzalisha rasilimali watu bora, elimu isiyo na ubaguzi, uchumi wa ushirika mamboleo utakaosisitiza kujitegemea na afya bora wakati wote.
Pia, ujenzi wa miundombinu ya kuleta maendeleo kwa kasi, demokrasia huru na ya kweli, umoja wa kitaifa na michezo ambayo siyo tu itailetea sifa Tanzania, bali kutoa ajira kwa vijana.
Alipoulizwa anaionaje changamoto ya uteuzi wa wagombea ndani ya Ukawa, Dk Kahangwa alisema umoja huo utadumu iwapo wataweka mbele masilahi ya Taifa na wananchi badala ya ubinafsi.
“Tunatambua kugombea ni kushindana lakini tutangulize masilahi ya Taifa, masilahi ya wananchi kabla ya masilahi ya chama kimoja ndani ya Ukawa,” alisema.
ADVERTISEMENT
Sitishwi na umaarufu
Dk Kahangwa alipuuza madai kwamba umaarufu wake ni mdogo na hivyo atakuwa na wakati mgumu kupambana na wagombea wengine wa Ukawa na CCM ambao ama wametajwa au kujitangaza wenyewe kuwania urais.
“Umaarufu una sura nyingi; wapo wanaojulikana kwa mambo ya hasara ambayo hayana msaada kwa Taifa. Unaweza usiwe na jina maarufu lakini una sifa za uongozi na uadilifu, kwa hiyo sina hofu kupambanishwa na mgombea mwingine yeyote ndani na nje ya Ukawa,” alisema.
Alitolea mfano wa Rais, Benjamin Mkapa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein kuwa ni miongoni mwa watu ambao hawakuwa maarufu, lakini walishinda uchaguzi.
Msimamo wa NCCR- Mageuzi
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema amefarijika kusikia Dk Kahangwa amekubali kuwania nafasi hiyo akimtaja kuwa ni miongoni mwa makada ambao ni nguzo ya chama hicho.
“Dk Kahangwa hatujamwokota barabarani, ni mtu tunayemfahamu, kumheshimu na kuthamini mchango wake ndani ya chama na yeye anakijua chama hiki vizuri,” alisema Nyambabe.
Alipoulizwa anamlinganishaje Dk Kahangwa na wagombea wengine kutoka vyama vinavyounda Ukawa na CCM, alisema: “Mimi namtia moyo kwa sababu hata nikimlinganisha na wagombea wengine naona anafaa zaidi. Kama hoja ya urais ni ujana, huyu ni kijana mwenzao na kama hoja ni kwenda na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia, huyu ni msomi aliyebobea.”
Alitoa wito kwa makada wengine wa NCCR-Mageuzi kujitokeza kuchukua fomu ili kuleta ushindani wenye tija ndani ya chama hicho. Dk Kahangwa ana Shahada ya Udaktari wa Falsafa (PhD) katika masuala ya elimu.
Powered by Blogger.