Riwaya mpya ya Kiswahili


UTANDAWAZI AU UTANDAWIZI? JINSI LUGHA YA RIWAYA MPYA YA KISWAHILI INAVYODAI Said A.M. Khamis 1.0 Utangulizi Kuzuka kwa riwaya mpya ya Kiswahili katika miaka ya 1990 kunaelezwa kwa viwango mbalimbali na wahakiki kama vile Wamitila (1991, 1997), Gromov (1998, 2004), Khamis (1999, 2001, 2003, 2004), Bertoncini (2002), Topan (2002), King’ei (2002), Dittemer (2002/2003) na Rettová (2004). Hapa, hatuna nafasi ya kurejelea tabia za ‘kimaumbo’, ‘kimiundo’ na ‘kimaudhui’ zinazoitofautisha riwaya hii ya Kiswahili na nyingine, ila tutajishughulisha na kipengele kimoja tu cha msingi, nacho ni kipengele cha lugha kama alama mojawapo ya mtindo1 au mwelekeo wa riwaya hii – lugha katika uhusiano wake na utandawazi au utandawizi. Katika makala haya tunatilia mkazo kwamba aina ya lugha inayotumika katika kazi fulani ya fasihi huathiriwa na nini kinachotokea katika jamii yenyewe ambamo mwandishi huchota fikira, maudhui, falsafa, itikadi, jazanda, mitindo, maumbo na miundo-lugha –hasa inapokuwa jamii yenyewe imo katika kasi ya mabadiliko makubwa kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia kuanzia wakati riwaya hii ilipoibuka katika miaka ya 1990 hadi leo. 2.0 Riwaya Mpya na Utandawazi Riwaya ya Kiswahili tunayoizungumzia imezaliwa mwanzoni mwa miaka ya 1990, muda mfupi tu baada ya neno utandawazi kuingia masikioni na kuzama akilini mwetu kuanzia miaka 1980. Utandawazi ni neno dhahania mno, lenye maana nyingi zenye utata kutegemea msisitizo wa anayelitumia. Pamoja na tofauti za maana na matumizi ya neno hili, wataalamu wanakubaliana kwamba ni neno linaloelezea mfungamano na uhusiano uliojitokeza katika miaka 30 iliyopita; hasa katika biashara na uchumi, lakini pia katika utamaduni, miongoni mwa jamii tofauti za dunia. Mfungamano na uhusianao huu unatofautishwa na mfungamano na mahusiano mengine ya aina hii yaliyojitokeza hapo awali, kwa sababu utandawazi umepata kasi kubwa ya kuwekeza mitaji na kuvuna bamvua la faida kiuchumi na kiutamaduni; ukisaidiwa na maendeleo makubwa ya kiteknolojia yaliyopatikana karibuni, hasa ya vyombo vya mawasiliano ambavyo vimefupisha au kuondoa vikwazo vya masafa na wakati (Jauch 2001, Offiong 2001). Kiutamaduni, utandawazi unahusishwa na kuenea kwa tamaduni za ki-Magharibi kwa njia ya kibiashara (k.m vinywaji vya Coca Cola, bia na pombe kali ambazo hapo zamani zilikuwa hazijulikani au zilijulikana kwa watu wachache tu wa Dunia ya Tatu na vyakula vya Kentucky na Mcdonald) au mtiririko wa muziki na taswira kupitia video, televisheni, mitandao ya kompyuta na simu, CD, DVD na VCD. Lakini kwa hakika si sahihi kuuchukulia utandawazi kijuujuu tu, au jinsi unavyofasiliwa na watetezi wake. Kwa hivyo, ipo haja hapa kuelezea, ingawa kwa ufupi, asili ya kuibuka kwake. Historia ya utandawazi haiwezi kuepushwa na misingi ya mikakati ya G7, Benki ya Dunia, IMF na WTO, vyombo vinavyosimamiwa, kuimarishwa na kuendelezwa na itikadi ya uliberali-mpya2 (Jauch 2001; 3-15; Offiong, 2001: 1-19). Kwa kweli, 1 Tunapenda kukumbusha kwamba hii ni maana moja tu ya mtindo – yaani mbinu ya pamoja inayotofautisha kundi la 2 Tafsiri ya ’neo-liberalism’ kinadharia, mfungamano na uhusiano huu wa utandawazi unafasiliwa kwa namna tofauti baina ya kambi mbili. Kambi ya kwanza inauchukulia utandawazi kuwa ni ‘baraka’ kwa nchi zote duniani, kwa sababu hatimaye utaboresha maisha ya watu wote duniani kote (Ruigrok & Van Tulder 1995:169). Kambi hii inadai kwamba utandawazi una faida kubwa hasa kwa nchi zinazoendelea3, na kwamba kufungua milango ya biashara, masoko huria ya bidhaa na kuufanya utamaduni wa taifa moja ukutane uso kwa uso na utamaduni wa mataifa mengine (sifa moja kubwa ya utandawazi), kunaleta fanaka kila pahala (Jauch, keshatajwa: 3). Kambi ya pili, ikitumia ithibati jarabati, inakanusha kabisa uhalali wa madai ya kambi ya kwanza, kwa kusema kwamba utandawazi si dhana mpya kamwe, bali ni upeo wa dhana kongwe yenye sifa mpya ya kutumia maendeleo makubwa yaliyopatikana kiteknolojia, kunyonya, kwa mapana na marefu, utajiri wa dunia na kuwaacha watu wa nchi masikini kuwa masikini zaidi kuliko walivyokuwa zamani. Na si kuwaacha masikini zaidi tu, bali pia kuchafua uchumi, tamaduni, mazingira na maisha yao vibayavibaya, hadi kufikia nchi hizo kudharauliwa na kuonekana si lolote si chochote katika fikra ya dunia hivi leo. Mabadiliko haya, kwa sehemu kubwa, yanatokana na upeo wa matatizo ya kiuchumi ya kimataifa yaliyotokea mwanzoni mwa miaka ya 1970, ambayo yalisababishwa na maslahi ya kibiashara na utashi wa mataifa makubwa yanayolenga kila siku kupata faida kubwa kupita kiasi (Murray 2000:7-8; ILRIG 1998). Jumla ya riwaya za Kiswahili tunazoita mpya ni zile za Euphrase Kezilahabi za Nagona (1990) na Mzingile (1990), riwaya moja ya Katama Mkangi ya Walenisi (1995), riwaya ya W. E. Mkufya ya Ziraili na Zirani (1999), riwaya moja ya Mohamed ya Babu Alipofufuka (2001) na miswada yake miwili4 ya Dunia Yao na Mkamandume, riwaya moja ya Wamitila ya Bina-Adamu (2002) na, kwa namna na kiwango fulani, riwaya ya Chachage ya Makuadi wa Soko Huria (2002). Sifa moja kubwa ya kimaudhui, miongoni mwa sifa kadha za riwaya hii, ni ile ya kushughulikia kwa kina matatizo ambayo yanaukabili ulimwengu wetu leo. Kwa namna nyingine tunaweza kusema, ingawa bado riwaya hii inajishughulisha kwa kiwango fulani, na matatizo ya ndani ya nchi na jamii husika, kwa kiasi kikubwa imekiuka mipaka ya kitaifa na kieneo. Kwenye jalada la nyuma la Bina-Adamu, tunaambiwa wazi kwamba… [n]i riwaya inayotumia sitiari ya kijiji kuangalia hali ya mataifa ya ulimwengu. Katika kuhitimisha makala yake Postmodernistic Elements in Recent Kiswahili Novels, Gromov (2004:13) anatuambia: [t]unaweza kusema kwamba fasihi ya Kiswahili inaendelea kuchukua dhima ya uchunguzi wa jamii –lakini, huku ikibeba silaha mpya za njia ya utunzi na fikra za majadiliano, inajishughulisha na matatizo mapya, na inachunguza, si jamii ya Afrika Mashariki tu, bali dunia yote kubwa (na) pumbavu, isiyoishika tena, lakini ndiyo pekee tuliyonayo– dunia yetu ya leo ... (tafsiri yangu). 3 Sina hakika kwamba neno hili tunaweza kuendelea kulitumia kurejelea nchi zetu za Kiafrika, lakini nitalitumia kwa kukosa neno linalofaa zaidi. 4 Dunia Yao ni mswada uliopelekwa Jomo Kenyatta Foundation tangu 2001 na kukubaliwa kuchapishwa lakini mwandishi aliuondoa huko, kwa kuchelewa kuchapishwa, akaupeleka OUP ambako nako umekaa tangu Julai, 2004. Ms wa Mkamandume ulimalizwa kuandikwa mwaka 2004 na bado haujawasilishwa kwa watoa vitabu wowote. Ingawa riwaya hii mpya, kama tulivyosema, inajishughulisha na mada mbalimbali za kimaudhui kuhusu matatizo yanayoikabili dunia yetu ya leo –hapa tumechagua kuzungumzia, kwa mujibu wa maoni yetu, tatizo kubwa na sugu kabisa la utandawazi– tatizo ambalo riwaya kama Nagona, Mzingile, Babu Alipofufuka, Dunia Yao, Bina- Adamu na Mkamandume, zinalijadili waziwazi. Kwa mfano, katika kuthibitisha namna gani dhamira ya utandawazi inavyotawala katika Bina-Adamu, Gromov (2004:8), akiteua kwa uangalifu lugha na picha zinazoelezea dhana ya utandawazi, anatambia hivi: Wakati wa safari yake ndefu, mbabe, akisaidiwa na sauti ya ajabu ya mwanamke mwenye sifa zisizo za kibinamu anayeitwa Hanna, anazuru Ulaya ambayo ‘inaishi jana’, Asia ya viwanda ambayo ‘inaishi kwa matumaini’ na Afrika, ambayo ‘inaishi mwishoni mwa kijiji cha utandawazi na imeharibiwaharibiwa na njaa na vita. Anapokuwa njiani, kila pahala anakutana na mambo yanayoonekana hayana mantiki, mambo ambayo hayaelezeki yanayofanywa na P. P mwenye miujiza –Ulaya P. P ameushinda ufashisti, lakini bado unaishi imara miongoni mwa wafuasi wake. Huko Asia ametupa bomu la Atomiki Hiroshima. Afrika, akitumia jiwe, amevigonga vichwa vya wanasiasa kuvitoa akili. Huko Urusi, ambako P. P anazuru kwa muda mfupi, hatuambii anafanya nini kwa vile anamwogopa Stalin. P. P anaiuza Afrika kwa watalii wa kigeni, anaharibu bahari kwa mafuta na mabaki machafu ya ‘radioactive’: Mwishoni mwa safari yake mbabe anaigundua Amerika –Bustani ya Adeni ya pili, ambamo wakazi wake, mapapa wa biashara za kimataifa, wanaishi (vizuri) kutokana na umasikini wa Nchi za Dunia ya Tatu, wakidai kwamba wanaishi leo na tena wanaishi katika uhalisia wa mambo ... (tafsiri yangu)


>>>>>INAENDELEA>>>>>

Powered by Blogger.