HISTORIA YA MUZIKI WA HIP HOP NA BONGO FLEVA NA JINSI UNAVYOONEKANA KUATHIRIWA ZAIDI NA WASHAIRI WA KIMAPOKEO KULIKO WANAUSASA


Hivyo basi tukiwaangalia mambo yanayosisitizwa na wanajadi na wanausasa, tunakubaliana na hoja kuwa, muziki wa Hip Hop na Bongo Fleva unaonekana kuathiriwa zaidi na wanajadi kuliko wanausasa. Na vipengele ambavyo wanajadi wanasisitiza kuzingatiwa katika ushairi ambavyo vinaonekana kujitokeza katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva kama tulivyoona hapo awali ni, Mizani, vina, kituo na kujitosheleza. Hebu tuangalie vipengele hivyo namna vinavyojitokeza katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva ambavyo ndivyo vinavyotufanya kushadidia hoja hii kuwa muziki wa kizazi kipya unaonekana kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa tukianza na;

Vina, tunaelezwa na Amri Abeid (1952:4) kuwa ni silabi za namna moja zinazotokea baada ya kila mizani kadha katika mstari wa shairi. Kwa upande wake, Wamitila (2003:345) anasema vina ni, dhana inayotumiwa katika taaluma ya ushairi kuelezea silabi zinazofanana katika sehemu sawa katika mpangilio wa ubeti wa shairi. Anaendelea kufafanua kuwa shairi linaweza kugawika katika vipande viwili na kuwa na vina vya kipande kimoja na kipande kingine. Hiki ndiyo kipengele kinachoonesha kuwa wasanii wengi wa muziki wa kizazi kipya (Hip Hop na Bongo Fleva) kwa kiasi kikubwa kuonekana kuathiriwa na ujadi.

Kati ya vitu ambavyo wanajadi wanasisitiza katika mashairi ni urari wa vina na mizani, kwa mfano Mnyampala (1962: Dibaji) anasema, Ushairi ni msingi wa maneno ya hekima tangu kale. Ndicho kitu kilicho bora sana katika maongozi ya dunia kwa kutumia maneno ya mkato na lugha nzito yenye kunata iliyopangwa kwa urari wa mizani na vina maalumu kwa shairi. Hapa Mnyampala pamoja na kuongelea suala la shairi kutumia maneno ya mkato na lugha nzito lakini maneno hayo yanatakiwa kupangwa kwa urari wa vina na mizani. Suala la urari wa vina pia linashadidiwa na Shabaan Robert ( 1958) akinukuliwa na Massamba (1983:54) janaposema, Ushairi ni sanaa ya vina inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi.Zaidi ya kuwa sanaa ya vina ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari.

Kama tulivyoona kwa wanajadi, vina ni kigezo kinachozingatiwa sana na wasanii wa Hip Hop/Bongo Fleva katika tungo zao. Hiki ndicho kigezo ambacho kwa asilimia kubwa ndicho kinatufanya kushadidia hoja hii kuwa mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva yanaonekana kuathiriwa sana na wanajadi kuliko wanausasa. Katika muziki huu, wasanii wasiozingatia matumizi ya vina katika tungo zao zinaonekana hazina maana kama wanajadi wanavyoona kuwa mashairi yasiyozingatia vina kuwa si chochote, kama anavyosema Afande Sele katika wimbo wake wa Mtazamo;
 Au wengine mmetumwa kama mamluki,
 maana yake hamna maana mnarap mradi rap,
 mistari imekosa vina yenye vina haina maana.

Aidha katika wimbo wake mwingine, Darubini Kali Afande Sele, anawashangaa wasanii wenzake wanaoimba bila vina kama anavyosema,
Mi nacheka sana kuna vitu vya kuimba vyenye maana kila kona,
(Sasa) inakuwa vipi unataja taja majina tu nyimbo nzima
Tena kwa mistari isiyo na vina!

Kwa mtazamo wa Afande Sele msanii asipozingatia matumizi ya vina anaonekana kama mamluki na mtu asiye na maana kwenye sanaa. Kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya hususani wa Hip hop, matumizi ya vina yanasisitizwa zaidi na hata wengine kujinasibisha kuwa wao ni wataalamu wa kutumia vina kama anavyojinasibisha Solo Thang katika wimbo wao Tumerudi Tena (Wateule) anaposema, Ona wakali wa vina, ona tumerudi tena... msanii mwingine Juma Nature katika wimbo alioshirikishwa na Rich One unaojulikana kwa jina la Hatuna Kitu anajigamba kuwa yeye ni mkali wa vina anaposema, “...Juma Nature, Sir Nature a.k.a msitu wa vina, yeah Watanzania mahili tuliokomaa kimashairi...” Hii yote inaonesha kwa namna gani wasanii wa kizazi kipya (Hip Hop/Bongo Fleva) wanaonekana kuathiriwa na wanajadi kutokana na kuzingatia matumizi ya vina katika tungo zao na hata kujinasibisha kuwa ili uwe msanii mzuri lazima ujue namna ya kuandika na kutunga mashairi yenye vina.
>>>>>INAENDELEA>>>>>>>>>>
Powered by Blogger.