HISTORIA YA MUZIKI WA HIP HOP NA BONGO FLEVA NA JINSI UNAVYOONEKANA KUATHIRIWA ZAIDI NA WASHAIRI WA KIMAPOKEO KULIKO WANAUSASA

HISTORIA YA MUZIKI WA HIP HOP NA BONGO FLEVA NA JINSI UNAVYOONEKANA KUATHIRIWA ZAIDI NA WASHAIRI WA KIMAPOKEO KULIKO WANAUSASA

Katika makala haya tunakusudia kujadili namna muziki wa kizazi kipya (Bongo Fleva na Bongo Fleva) kuonekana kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa. Hivyo basi ili kukamilisha hilo, kazi hii tumeigawa katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza ni utangulizi ambapo tutaangalia maana ya istilahi muhimu zinazojitokeza katika mada yetu, tutaangalia historia ya muziki wa kizazi kipya lakini pia tutaangalia kwa ufupi wanajadi na wanausasa ni vitu au mambo gani wanayoyasimia. Sehemu ya pili ni kiini cha swali letu, katika sehemu hii tutaangalia vipengele vinavyoonesha kuwa wasanii wa kizazi kipya kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa na sehemu ya mwisho itakuwa ni hitimisho.

Maana ya Hip Hop na Bongo Fleva.
Wapo wanaouona muziki wa kizazi kipya yaani Hip Hop na Bongo Fleva kuwa ni kitu kimoja lakini wapo wanaopinga na kutofautisha kuwa Hip Hop na bongo fleva ni aina tofauti ya muziki (Omari 2009:5, Samwel 2012:12). Ama kuhusu neno Bongo Fleva mpaka sasa bado kuna utata kuhusu nani hasa mwasisi wa neno hili, inaelezwa kuwa, mwanamuziki wa regge, Jah Kimbute ndiye aliyeasisi neno hili pale alipoamua kuchanganya muziki wa asili na regge na kuziita Bongo Fleva. Mtayarishaji wa muziki P.Funk anaeleza kuwa mwasisi wa neno Bongo Fleva ni DJ Bonnie Love ambaye aliliasisi neno hilo mwaka 1998, Omari (keshatajwa, 10-11).

Madai haya kuhusu waasisi wa neno Bongo Fleva linaonekana kupingwa vikali na Mtangazaji wa siku nyingi, Michael Mhagama ambaye anadai kuwa yeye ndiye mwasisi wa neno hilo na aliliasisi katika kipindi chake cha DJ Show kilichokuwa kinarushwa na Redio One miaka ya 1990 hususani mwaka 1996. katika makala yake, Mhagama anasema, “Ilipofika dakika 30 za muziki wa R & B,siku hiyo nilikuwa kwenye usukani na kwa mbwembwe nilicheza nyimbo ya kundi la R&B lililoitwa 4Krewz Flava na baadaye kuiunganisha na nyimbo nyingine ya Unique Sistaz.Kwa vile midundo,mpangilio,lugha na utaalamu wa muziki wenyewe kamwe huwezi kuufananisha na ule wa Soul 4 Real au SWV kutoka Marekani,tulipenda tutofautishe kidogo kati ya aina hizi mbili na ndipo session hii niliibatiza jina ambalo lingetofautisha R&B ya Marekani na ile ya kwe tu….niliipa session hii jina la BONGO FLAVA.” Wengine wanaotajwa kuwa ni waasisi wa neno Bongo Fleva ni DJ. KBC, DJ. Phat Black, DJ. Venture na Steve B. (Reaster-Jahn na Hacke, 2014:24).

Ingawa lengo la kazi hii si kujikita katika mgogoro huo ila tumeona kwa umuhimu wake tuugusie japo kwa ufupi. Kama tulivyosema hapo awali kuwa wapo watu wanaouona muziki wa Hip Hop na Bongo Fleva kuwa ni muziki tofauti, Ramadhan Mponjika akinukuliwa na Samwel na wenzake (2013:55) anasema, muziki wa Bongo Fleva ni kapu ambamo ndani yake kuna miziki ya aina mbalimbali ikiwemo zouk, rhumba,regge, RnB, n.k. Kinachoelezwa hapa ni kuwa, muziki wa Bongo Fleva ni aina yoyote ya muziki wenye asili ya nje lakini unaimbwa kwa mahadhi ya Tanzania (Bongo) lakini si Hip Hop. Dai hili linaungwa mkono na Michael Muhagama (keshatajwa) kupitia andiko lake, anasema, “Hii ilikuwa mwaka 1996 na ndio ulikuwa mwanzo wa neno BONGO FLAVA likiwa na maana muziki wenye mahadhi ya nje lakini wenye vionjo na ladha ya Tanzania na si vinginevyo lengo kuu ni kuitofautisha na muziki ule wa Marekani. Hip Hop ya Tanzania ilibaki na itabaki vile vile kama ilivyo, ila muziki wowote ule wa nje, mbali ya Hip Hop na DANSI ya Tanzania niliuita na kuufahamishakwa umma wa watanzania kama BONGO FLAVA ndani ya kipindi cha DJ SHOW cha Radio One.” Hapa maana yake ni kuwa, jina la Bongo Fleva lilitumika tu, kutambulisha muziki wenye asili ya nje lakini wenye mahadhi ya Tanzania (Bongo) tofauti na muziki wa Hip Hop na dansi ambayo yenyewe ilitambulishwa kwa jina la Hip Hop ya Tanzania/Bongo au Bongo Hip Hop.
Ama kuhusu Hip Hop, Mahenge (2011:8) anasema, Hip Hop ni aina ya ushairi, usimuliaji au usemaji unaopangwa kivina kwa kufuata mdundo wa ala za muziki ambao ulisharekodiwa. Pamoja na kwamba fasili hii ya Mahenge inatupa mwanga kuhusiana na maana ya Hip Hop ambayo kwa kiasi kikubwa tunakubaliana nayo lakini dai la kusema usimuliaji au usemaji unapangwa kivina kwa kufuata mdundo wa ala za muziki ambao ulisharekediwa si sahihi kwani sasa hivi wasanii wengi wa Hip Hop wanaimba juu ya midundo ya muziki ambayo haijarekodiwa vyombo vya muziki vinapigwa sambamba na wao wakiimba na wakati mwingine hurap kwa mtindo unaojulikana kama mitindo huru yaani kutoa mashairi ya papo kwa papo kwa kufuata midundo ya muziki inayopigwa au bila kuwepo kwa midundo ya miziki yaani akapela.

Kwa maoni yetu, tunaona kuwa Hip Hop na Bongo Fleva ni muziki tofauti, muziki wa Hip Hop ni utamaduni unaombatana na elementi za, michoro, rap, Dj, mabreka, ni muziki ambao mashairi yake yanaganwa kwa kutumia mashairi yenye vina na midundo mizito wakati bongo fleva ni mkusanyiko wa muziki wenye asili kutoka nje ya Tanzania lakini yenye mahadhi na vionjo vya Tanzania ambayo hujumuisha Zouk, Kwaito, RnB, Kwaito, n.k. Kwa ujumla muziki huu Hip Hop na Bongo Fleva huitwa kwa jina la muziki wa kizazi kipya ikiwa na maana ya muziki unaopendwa na vijana kizazi cha sasa (Omari 2009:5, Samwel 2012:12).
>>>>>INAENDELEA>>>>>>>>>>>
Powered by Blogger.