HISTORIA YA MUZIKI WA HIP HOP NA BONGO FLEVA NA JINSI UNAVYOONEKANA KUATHIRIWA ZAIDI NA WASHAIRI WA KIMAPOKEO KULIKO WANAUSASA


Suala lingine ambalo linasisitizwa na wanajadi ni uwepo wa kituo katika shairi. Abedi (kashatajwa uk.4) anatueleza kuwa, kituo ni mstari wa mwisho wa kila ubeti. Anaendelea kufafanua kuwa, kutuo huweza kuwa ama kiini cha habari au kimalizio. Maana hii ya kituo haipishani sana na maana inayotolewa na Wamitila (2003:93) isipokuwa anaongezea kuwa, wahakiki wengi hukiita kitua kuwa ni kibwagizo. Wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva hupenda kutumia istilahi ya kiitikio. Kwa wanajadi kila baada ya ubeti kama ubeti utakuwa na mistari mine basi mstari wanne ndiyo huwa kiitikio/kituo, na kwa upande wa mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva huwa na kituo yaani kiitikio isipokuwa wao hawana mstari maalumu ambao unapaswa kituo kiwepo isipokuwa kituo/kiitikio huwekwa mara baada ya kukamilika kwa kila ubeti. Hebu rejea mfano wa wimbo wa Profesa Jay wa Kubwa Kuliko anatumia kiitikio kifuatacho kila baada ya kukamilika kwa ubeti.
Ninaposema jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zinduko,
Ninaposema jay kubwa kuliko
                                                                                                                                       
Wakati mwingine kiitikio si lazima kifuate kila baada ya ubeti kwisha, wapo wasanii wengine ambao hutumia fomula ya kuanza na kiitikio kikifuatiwa na ubeti, kiitikio ubeti kiitikio, rejea mfano wa Diamond Platznum wimbo wa Kesho, msanii ameanza na kiitikio ndiyo ubeti unafuata (rejea mfano wetu wa wimbo huo tulioutoa hapo awali, pia rejea shairi la Joh Makini Najiona Mimi naye kiitikio kinajitokeza kila baada ya ubeti).

Abeid (keshatajwa) anatueleza kuwa katika mashairi ya wanajadi, kituo/kiitikio kinaweza kubadilika badilika, hali hii pia hujitokeza katika mashairi ya wanamuziki wa Hip Hop na Bongo Fleva, mfano katika shairi la wimbo wa Profesa Jay Ndiyo Mzee tunaona kiitikio cha ubeti wa kwanza kinatofautiana na kiitikio cha ubeti wa pili. Kwa mfano ubeti wa kwanza anatumia kiitikio kifuatacho;
Si mtafurahi Watanzania jamani? (ndiyo mzee)
Si ni kweli nakubalika jamani? (ndiyo mzee)
Basi mimi ni mkombozi wenu jamani (ndiyo mzee)...

Wakati katika ubeti wa mwisho anatumia kiitikio kingine na kinaimbwa na mtu mwingine (Juma Nature) anasema;
Je wananchi mmenisikia? (ndiyo mzee)
Kuwa huyu jamaa hatufai (ndiyo mzee)
Na inafaa kumchukia (ndiyo mzee)
Hatumtaki aondoke zake (ndiyo mzee)

Jambo lingine linalosisitizwa na mwanajadi katika mashairi ya kimapokeo ni kujitosheleza kwa kila ubeti. Abedi (kashatajwa,uk.4) anaona utoshelevu ni kipengele cha msingi katika shairi, anasema kuwa, kila ubeti ujitosheleze kadiri iwezekanavyo, yaani, uwe na maana kamili, na usingoje kutimizwa na ubeti mwingine. Jambo hili pia linajitokeza katika mashairi ya wasanii wa Hip Hop  na Bongo Fleva kila ubeti katika nyimbo zao huwa na maana inayojitosheleza. Ukiangalia mifano ya nyimbo tulizozitumia hapo juu ukichunguza kila ubeti utaona kuwa ubeti unajitosheleza na unatoa maana kamili. Labda kwa mfano mzuri tutumie wimbo wa msanii Jay Mo unaoitwa Story tatu Tofauti, katika wimbo huu kila ubeti umebeba kisa chake tofauti ambacho kimekamilika na unatoa maana, hebu hapa tuangalia ubeti wa tatu.
Mariam alikuwa mtoto aliyekuwa na uzuri wa peke yake,
Mi mwenyewe mmojawapo kati ya waliotaka ajiweke,
Ili anione mchumba wake,
Alisimama peke yake, alilinga kwa uzuri wake,
Tajiri familia yake, kama hanyi au hali,
Kwa jinsi alivyojisikia, na vile home kuna mali,
Kiburi alijijengea, hali iliyofanya wengi waliomjua kumchukia,
Tuliosoma naye hiyo tabia tulishaizoea,
Wazazi walisoma ndiyo maana maisha yao ya juu,
Yeye hilo hakuliona cha maana alichoona ni usister duu,
Pesa zikamtia udhaifu, za nyumbani akaona hazitoshi,
Shuleni akacheza rafu, masomo akashindwa pasi,
Alipata zero kitu ambacho wazazi hawakuamini,
Angekuwa mtoto wa kiume wangeshamfukuza nyumbani,
Wakaona siyo mbaya kama atarudia mtihani,
Kitu ambacho mariam hakikumuingia akilini,
Wakamuuliza anachotaka, akajibu computer,
Cheti akapata kwenye stashahada akachemsha,
Baada ya kupewa ujauzito, inasemekana na kizito,
Ambaye ana mke na pia nyumbani ana watoto,
Cha moto kikaanza nyumbani alipofukuzwa,
Kumbe yule kizito ana ngoma anafanya kuusambaza,
Hakumsikiliza Jose Mtambo alipoimba kizaazaa,
Yamemwaribikia mambo na mtoto bado hajazaa.

Katika ubeti huu, utaona kuwa umebeba kisa kizima kinachojitosheleza na ukisikiliza ubeti wa kwanza na wa tatu utaona kuwa kila ubeti una kisa chake kinachojitosheleza na kinachotoa maana iliyokamilika wala ahitaji ubeti mwingine ukamilishe wazo au maana ya shairi. Katika ubeti huu wa tatu msanii anaelezea tabia za Mariam, kutowasikiliza wazazi wake, kutozingatia elimu na kujikuta akipewa mimba na kuambukizwa virusi vya ukimwi.

Hitimisho.
Wasanii wa muziki wa kizazi kipya yaani Bongo Fleva na Hip Hop kama wamechota baadhi ya sifa katika ushairi wa  kimapokeo katika kutunga mashairi. Kipengele kikubwa ambacho wana-Hip Hop na Bongo Fleva wanaonekana kuathiriwa nacho ni kipengele cha matumizi ya vina katika tungo zao ambacho hasa wanajadi ndiyo wanaona kuwa ni roho ya ushairi. Lakini pamoja na hayo, pia usasa katika mashairi yao unajitokeza kwa kiasi fulani, kwa mfano yapo mashairi ya wasanii wa muziki huu ambayo hayazingatii vina lakini yanaimbika. Pia kutokuwa na idadi maalumu ya mistari katika beti za mashairi yao pia ni sifa za usasa katika utungaji wa mashairi.. Kwa ujumla hatuweza kusema wazi kuwa wanajadi ndiyo wamewaathiri wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva au la kwani ni jambo linalohitaji utafiti wa kina na mjadala mpana, tukiangalia hata namna muziki huu ulivyoingia nchini kwa kuiga nyimbo za wasanii wa Marekani na Ulaya ambazo nazo zinaonekana kuzingatia matumizi ya vina, vituo, kujitosheleza n.k. huenda wasanii hao ndiyo waliowaathiri zaidi. Lakini kwa mujibu wa mjadala wetu tunasema uwepo wa nduni za kijadi katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva hususani kipengele cha vina washairi hawa inaonekana na hapa tunasisitiza kuwa inaonekana kama wameathiriwa na wana jadi kwa kuwa jambo kubwa linalosisitizwa na wanajadi ni matumizi ya vina na mizani ambayo hata wana Hip Hop na Bongo Fleva nao husisitiza matumizi hayo kama tulivyoona hapo awali.
>>>>>>>>INAENDELEA>>>>>>>>>>>>

Powered by Blogger.