MADA YA KWANZA: MAWASILIANO


                   

                   KIDATO    CHA KWANZA
                             MADA YA  KWANZA: MAWASILIANO
Katika mada hii unatarajiwa kuelewa fasili ya mawasiliano na jinsi mchakato wa mawasiliano unavyofanyika. Utaelewa dhana ya lugha na vipengele muhimu vinavyokamilisha fasili ya lugha. Utaelewa dhima kuu za lugha, matumizi na umuhimu wake. Vilevile katika mada hii utajifunza juu ya lafudhi na matamshi mbalimbali ya watumiaji wa lugha ya Kiswahili.

Lugha kama Chombo cha Mawasiliano
Mawasiliano ni mchakato wa kuhawilisha taarifa kwa njia ya ubadilishanaji wa mawazo, hisia, malengo, tabia, matarajio, mitazamo kupitia mazungumzo, ishara na maandishi. Ni ubadilishanaji wa taarifa unaoleta maana baina ya pande mbili au zaidi ambazo zinaweza kuwa viumbe hai au kinyume chake. Sasa hapa sisi tutajikita katika mawasiliano yanayofanywa baina ya viumbe wanaotumia lugha (ambao kimsingi ni binadamu).

Maana ya Mawasiliano
Lugha ni nyenzo muhimu sana katika mawasiliano ya binadamu. Ulishawahi kujiuliza kwamba mwasiliano yangekuwaje pasipokuwepo lugha? Mwalimu angekua anatumia mtindo gani kukufundisha darasani au wewe ungemwombaje kalamu rafiki yako? (Unasema ungewasiliana kama wanavyowsiliana watu wasiosikia au kuzungumza?) Hao pia wanawasiliana hivyo kwa sababu wana maarifa ya lugha.
Mafumbuzi ya kisayansi na teknolojia, yote haya yasingewezekana pasipo kutumia lugha, usingeweza kusogoa (kuchat) na marafiki zako kwenye facebook, usingeweza kumwandikia ujumbe rafiki yako kupitia simu yako na kadhalika.
Umeona sasa jinsi lugha ilivyo muhimu katika mwasiliano? Kabla hatujaona umuhimu huu hebu tuangalie fasili/maana ya lugha.
Kuna mitazamo mbalimbali juu ya fasili ya lugha lakini kwa ujumla lugha inaweza kufasiliwa kama mfumo wa sauti za nasibu zilizokubaliwa na watu au jamii ili zitumike katika mawasiliano yao ya kila siku ili kuelezea hisia, mawazo, matakwa na mahitaji yao.
Kulingana na fasili hii tunaweza kubainisha maneno ya msingi yanayojitokeza katika fasili ya lugha, maneno hayo ni pamoja na haya yafuatayo:

Lugha ni mfumo
Kila lugha ya mwanadamu imeundwa katika mifumo miwili mikuu; mfumo wa sauti na mfumo wa maana. Lugha huundwa kwa sauti ambazo huunganishwa kuunda neno au sehemu ya neno, maneno nayo huungana kuunda miundo mikubwa zaidi yenye maana kama virai, vishazi, sentensi na aya. Mfano; k+u+k+u – kuku
Mtoto + anatembea – mtoto anatembea
Katika muunganiko huu wa maneno na miundo mbali mbali, huwa kuna kanuni na sheria zinazodhibiti mfuatano wa kila kipashio. Kuna kanuni zinazodhibiti mfuatano wa sauti, mfuatano wa mofimu, mfuatano wa maneno na hata mfuatano wa sentensi. Kwa maana hiyo, lugha ya mwanadamu ni mfumo wenye kanuni, sheria na taratibu maalumu ambazo zikikiukwa basi kunakuwa hakuna utimilifu wa lugha husika. Sheria hizi zinazotawala mpangilio wa viunzi vya lugha hiyo ndizo zinazowawezesha watumiaji wa lugha fulani kuelewana.

Lugha ni mfumo wa sauti nasibu
Lugha ni ya nasibu kwa maana kwamba, hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya neno (kwa mfano jiwe) na kitu chenyewe tunachotumia katika ujenzi na matumizi mengine (maana na kirejelewa). Hii ina maana kwamba, maumbo ya ishara za kiisimu hayana uhusiano wowote au mfanano wowote na maana ambazo tunayapa. Kwa mfano neno “jiwe” hakuna watu waliokaa na kusema kuanzia leo hili litaitwa jiwe. Vile vile hakuna uhusiano wowote kati ya neno “jiwe” na umbo linalorejelewa. Uhusiano wake ni wa nasibu tu na hutofautiana kutokana na lugha moja na nyingine. Jiwe mnaliitaje katika lugha yenu? Basi huo ndio unasibu wa lugha.

Lugha ni maalumu kwa mwanadamu
Lugha ni chombo cha mawasiliano ambacho amejaliwa binadamu tu na kwamba hakuna kiumbe mwingine ambaye si binadamu mwenye uwezo wa kuzungumza na kutumia lugha. Hii ina maana kuwa kuna sifa fulani za lugha za binadamu ambazo hazipatikani kwa kiumbe mwingine yeyote yule isipokuwa mwanadamu. Ingawa ndege, mbwa, nyuki, tumbili wanaweza kuwasiliana, mawasiliano yao huwa ni ya sauti au ishara ambazo kimsingi siyo lugha, pia huwa yanadhibitiwa na hisia tu kama hofu, njaa, na ishara za kutoa taarifa. Binadamu ana uwezo wa kujifunza lugha mbalimbali na kuitumia katika mazingira yake na kitu ambacho wanyama hawawezi. Kwa mfano, ukimchukua paka wa china na kumleta Tanzania atatoa sauti ile ile sawa na paka wa Tanzania kwa kueleza shida ile ile au kutoa ishara ile ile.

Lugha ni mfumo wa ishara
Uishara wa lugha unamaanisha kuwa maneno huambatanishwa/huhusishwa na vitu, matendo,mawazo au hisia kwa makubaliano ya unasibu tu. Vile vile, yale tunayoyasoma katika maandishi ni ishara tu, maana zake lazima zipatikane katika muktadha wa mawasiliano. Hivyo basi, tunapojifunza lugha lazima tufahamu mfumo wa alama za lugha hiyo na kuelewa uhusiano uliopo kati ya ishara na vitu vinavyowakilishwa.

Lugha hutumia sauti
Sifa kuu ya lugha ni kutumia sauti ambazo hutengenezwa na ala za sauti. Pamoja na maendeleo ambayo mwanadamu ameyafikia kwa sasa katika uandishi na uwasilishaji wa taarifa kwa kutumia lugha sauti ndiyo msingi wa kila kitu. Hii ni kutokana na ukweli kwamba:
  1. Mtoto hujifunza kuzungumza kabla hajajifunza kusoma na kuandika.
  2. Mtoto hujifunza lugha moja kwa moja bila kufikiri kadiri anavyokuwa
  3. Maandishi yalikuja baada ya mazungumzo
  4. Maandishi huwasilisha yale yanayozungumzwa
  5. Watu kwa kawaida hutumia muda mwingi kuzungumza kuliko kuandika
Kuna mambo mengi ya muhimu katika sauti za lugha ambayo hayawezi kuwasilishwa vema kwa kutumia maandishi. Mambo hayo ni kama, kiimbo, toni, mkazo, kidatu; haya ni muhimu katika mawasiliano lakini hayawezi kuwasilishwa kisawasawa kwa kutumia maandishi

>>>>>>>INAENDELEA>>>>>>>>>>>>>
Powered by Blogger.