Rais Kikwete: Uvamia wa polisi una dalili za ugaidi


Rais wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete
Dar es Salaam. Hatimaye Rais Jakaya Kikwete amedokeza kuwa matukio ya watu wasiojulikana kuvamia vituo vya polisi, kupora silaha na kuwashambulia askari kuwa, “yana sifa za ujambazi na mwelekeo wa kigaidi.”
Akizungumza katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi jana, Rais Kikwete alisema hali ya usalama nchini ni nzuri kutokana na matukio hayo pamoja na mengine ya mauaji ya albino.
“Matukio haya yana sura mbili. Yana sura ya ujambazi, lakini pia baadhi yake yana dalili za ugaidi. Vyombo vyetu vya usalama vinaendelea kufanya kazi yake ya uchambuzi wa kila tukio na kulipa nafasi yake stahiki,” alisema Rais Kikwete.
Matukio yenyewe
Katika hotuba hiyo ya maneno 3,362, Rais Kikwete alitoa orodha ya matukio ya kuvamiwa vituo vya polisi kuwa katika kipindi cha miezi 12 jumla ya bunduki 38 ziliporwa na askari polisi saba kuuawa.
Alivitaja vituo vya polisi vilivyovamiwa kuwa ni Newala mkoani Mtwara ambako bunduki tatu ziliporwa, Ikwiriri katika Wilaya ya Rufiji (bunduki saba), Kimanzichana, Wilaya ya Mkuranga (bunduki tano), mbili zikiwa za polisi na tatu za raia zilizokuwa zimezihifadhiwa hapo.
Alisema katika Kituo cha Ushirombo Wilaya ya Bukombe bunduki 18 ziliporwa, ingawa baadaye zilipatikana zote.
Kadhalika, alisema katika maeneo ya Pugu Machinjioni na Tanga, askari waliokuwa katika shughuli za ulinzi na doria walishambuliwa na kuporwa silaha tatu.
Askari waliouawa
Katika matukio hayo, Rais Kikwete alitaja idadi ya askari saba waliopoteza maisha mmoja akitoka katika kituo cha Newala, Kimanzichana mmoja, Ikwiriri wawili na Ushirombo watatu.
Hata hivyo, Kikwete alitumia nafasi hiyo pia kutoa pongezi kwa polisi na Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ) kwa kazi nzuri ya kupambana na uhalifu nchini.
“Silaha zote 18 zilizoporwa Ushirombo zimepatikana na watu 10 wanaotuhumiwa kuhusika na uhalifu huo wamekamatwa. Katika tukio la Tanga silaha moja kati ya mbili zilizoporwa imepatikana,”alisema Rais Kikwete.
Kadhalika katika operesheni hiyo, Rais Kikwete alisema watuhumiwa saba walitiwa mbaroni, wanne kati yao wakiwa ni wale waliokuwa wamejificha katika mapango ya Kiomoni katika Kitongoji cha Karasha-Mikocheni, kilichoko kijiji cha Mzizima wilayani Tanga.
Wito kwa wananchi
Kuhusu uhalifu, Rais Kikwete aliwataka wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama hasa Jeshi la Polisi ili kukomesha uhalifu huo na mwingine.
“Nawaomba mfanye mambo mawili: Kwanza, toeni taarifa polisi mnapozipata habari za vitendo viovu au nyendo za watu waovu wanavyokusudia kufanya wahalifu au taarifa za wale waliokwishafanya uhalifu,” alisema.
Kadhalika Rais Kikwete aliwataka Watanzania kuacha kushabikia uhalifu na kueneza taarifa potofu katika mitandao ya kijamii badala yake watumie mitandao hiyo kupinga fikra potofu na kuwafichua wahalifu.
Mauaji ya albino
Katika hatua nyingine, Rais Kikwete aliagiza watu wanaojihusisha na mauaji ya albino wasakwe, kufikishwa mahakamani na kuadhibiwa vikali pindi watakapopatikana na hatia.
“Lazima tulaani vikali mauaji ya ndugu zetu albino. Ni vitendo vya kinyama ambavyo havitegemewi kufanywa au kutokea katika jamii yoyote ya watu waliostaarabika, wanaomuabudu Mungu,” alisema.
Rais Kikwete alisema mauaji ya watu wa kundi hilo yanafedhehesha na kuharibu sifa ya Taifa na kusema kuwa Serikali imelipa uzito mkubwa suala la kudhibiti na kukomesha mauaji hayo.
Alisema tangu aingie madarakani Aprili 17, 2006, alianza kupambana na mauaji hayo na yalipungua kutoka 18, mwaka 2008 hadi sifuri mwaka 2011.
“Inawezekana kuwa matukio ya hivi karibuni yanaashiria kuwa uhalifu huu unataka kuibuka upya, hatutaacha hali iwe mbaya kama ilivyokuwa miaka ya nyuma. Tutatumia mbinu na maarifa tuliyoyatumia kukabili wimbi kubwa la mauaji lililokuwapo mwaka 2007 na 2008,”alisema Rais Kikwete.
Vilevile Rais Kikwete alisema ili kutokomeza kabisa matukio ya mauaji na ukataji wa viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi wananchi hawana budi kuachana na imani za kishirikina.
“Ni ujinga ulioje kwa mtu kuamini kuwa mafanikio yake hayatategemea juhudi zake na maarifa yake bali kuwa na kiungo cha mwanadamu mwenzake mwenye ulemavu wa ngozi,” alisema.
Alisema kinachochochea uovu huo ni imani potofu ya kuamini kuwa kiungo cha mtu mwenye ulemavu wa ngozi kinasaidia katika shughuli za biashara, uvuvi au uchimbaji wa madini.
“Serikali na jamii haitalazimika kushughulikia mambo haya ambayo siyo tu ni fedheha hata kumsimulia mtu, bali yanatisha na kusikitisha,” alisema.
Kukuta na chama cha albino
Pamoja na kulaani mauaji hayo, Rais Kikwete ameahidi kukutana na baadhi ya viongozi wa chama cha watu wenye ulemavu wa ngozi wiki hii ili kusikiliza maoni yao ya namna ya kumaliza tatizo hilo.
Kura ya maoni
Pamoja na mambo mengine, Rais Kikwete alizungumzia mchakato wa kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa na kuwataka Watanzania wawe na subira huku wakizingatia sheria ya kura ya maoni na kanuni zake.
Alisema kinachoendelea sasa ni matayarisho ya kufanyika kwa kura hiyo baada ya Bunge Maalumu la Katiba kutunga Katiba Inayopendekezwa na Rais kuichapisha na kutangaza siku ya kupiga kura ya maoni.
Katika mchakato wa kuelekea kupiga kura hiyo Rais alisema utekelezaji wa kuandikisha wapiga kura, kuchapisha na kusambaza Katiba Inayopendekezwa tayari vimeshaanza.
“Tayari Katiba Inayopendekezwa imetangazwa katika tovuti za Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo na katika tovuti ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Pia imechapichwa magazetini,” alisema.
Uandikishaji wapiga kura
Rais Kikwete pia alizungumzia zoezi la uandikishaji katika daftari la kudumu la wapiga kura kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya utambuzi wa alama za mwili (BVR).
Aliisifu teknolojia ya BVR na kusema kuwa itasaidia kuondoa kutoaminiana, manung’uniko na madai ya udanganyifu katika chaguzi nchini.
“Kuanza kutumika kwa teknolojia hii ni kielelezo cha utashi wa Serikali kuwa nchi yetu iwe na chaguzi zilizo huru, wazi na haki,” alisema.
Kadhalika aliwataka wananchi kutumia fursa iliyopo kujiandikisha kabla ya uchaguzi mkuu kwani hakutakuwapo na fursa nyingine baada ya hapo.
“Kama ilivyoelezwa na Tume na mimi kusisitiza mara kadhaa, watakaojiandikisha wakati huu ndio watakaopiga kura ya maoni kuhusu Katiba Inayopendekezwa na ndio watakaopiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu,” alisema.
Kuhusu kazi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Rais Kikwete alisema hatua iliyofikiwa na tume hiyo inatia moyo na kuondoa hofu iliyoanza kuingia kuwa huenda zoezi hili lisingefanikiwa.
Powered by Blogger.