Ukawa walitaka Bunge kuiwajibisha Serikali

>Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), umelitaka Bunge kuiwajibisha serikali ikiwa Rais Jakaya Kikwete atashindwa
Dar es Salaam. Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), umelitaka Bunge kuiwajibisha serikali ikiwa Rais Jakaya Kikwete atashindwa kutekeleza maazimio ya Bunge ikiwemo kumng’oa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
Akizungumza jana, Mwenyekiti wa Ukawa Profesa Ibrahim Lipumba akiwa na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Katibu Mkuu wa Chadema, Wilbrod Slaa, alisema Kikwete anasita kumuondoa Muhongo wakati Bunge lililishatoa maazimio ya kutaka aondolewe.
Profesa Lipumba alisema Bunge linalowakilisha wananchi zaidi ya milioni 45 liliazimia uteuzi wa Muhongo utenguliwe lakini rais anasema bado anachunguza.
Profesa Lipumba alisema kama Rais Kikwete atashindwa kumwajibisha Muhongo atakuwa ameshindwa kutekeleza moja ya maazimio ya Bunge na kwamba Ukawa litaliomba Bunge kuiwajibisha serikali.
Alisema moja ya njia ya kuiwajibisha serikali ni pamoja na wabunge kupiga kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu.
Profesa Lipumba alisema “ hivi rais anachunguza nini haliamini bunge, kama anavyoteua mawaziri  pia ana madaraka ya kutengua nafasi zao, sasa anasita nini wakati ni azimio la bunge limemwelekeza, ikumbukwe kuwa bunge kwa niaba ya wananchi ndilo lenye jukumu la kuisimamia serikali,” alisema Lipumba.
Alisema hotuba aliyoitoa Jumatatu wakati akiwahutubia wazee wa mkoa wa Dar es Salaam, haijakidhi matarajio ya wengi kwani kuna maazimio hayajatekelezwa.
Azimio ambalo halijatekelezwa na rais Kikwete ni lile linalotaka kutaifishwa kwa mitambo ya  IPTL na kutengua uteuzi wa Muhongo.
Mwenyekiti huyo alisema rais amekataa kutekeleza azimio la kutaka mitambo ya IPTL itaifishwe  na kutoa sababu ambazo hazina maana.
 “Tangu mitambo ya IPTL imefungwa taifa limepata hasara kubwa kwa sababu umeme unaouzwa na ni wa gharama kubwa kuliko mitambo yoyote ya umeme inayotumika katika bara la Afrika taifa limeingia hasara kubwa, rais aitaifishe,” alisema Profesa Lipumba.
Alisema katika hotuba hiyo rais alionyesha kuipendelea IPTL na kuikandamiza Tanesco wakati akielezea kuwa fedha za Escrow zilikuwa mali ya IPTL.
Hatua za kuchukua
Lipumba alisema kama rais atashindwa kutekeleza baadhi ya maazimio, Ukawa wataitisha maandamano nchi nzima ili kulaani ufisadi wa Tegeta Escrow na kushinikiza utekelezaji wa maazimio ambayo yatakuwa hayajatekelezwa.
Alisema hatua za kisheria zichukuliwe dhidi ya wote waliohusika na ufisadi wa akaunti ya Tegeta Escrow na wengine walionufaika nazo.
Sheria ya maadili itungwe upya ili iweke uwazi wa mtu yoyote kuona taarifa ya mali za viongozi.
Vyama vya siasa vya Ukawa  kwa kushirikiana na wabunge vitaendelea kuelimisha umma kuhusu ufisadi wa Akaunti ya Tegeta Escrow
Powered by Blogger.